Na John Walter-Manyara

Ili kuondoa kilio kwa wakulima  juu ya mbegu feki za Mahindi, Chama kikuu cha Ushirika mkoani Manyara yaani  Rift Valley Co-operative Union Ltd (RIVACU) kwa msimu wa mwaka 2019-2020 kimeamua kusambaza mbegu tani 12  kwa wanachama wake hatua inayotajwa kusaidia kudhibiti  ubora.


Akizungumza na kituo hiki Kaimu meneja wa RIVACU Pendoeli Valentino, amesema  kwa kipindi hicho wamefanikiwa kusambaza mbegu hizo kwa wanachama wao zaidi ya 3,000 waliopo mkoani Manyara na mkoa wa Arusha katika wilaya ya Karatu na Ngorongoro na kuonyesha mafanikio makubwa.


Meneja huyo amesema changamoto hiyo ilikuwa ikiwakumba sana wakulima kwa sababu ya kutokujua mahali sahihi pa kununulia mbegu ambayo ina viwango vinavyohitajika.


Amesema Wakulima kutoka vyama vya msingi wanavyovihudumia mara nyingi wamekuwa wakitoa malalamiko juu ya changamoto wanazokutana nazo ikiwemo mbegu zisizo na viwango kwa sababu zinakuwa zimekaa dukani muda mrefu au zingine hazistahimili katika maeneo yao hivyo kwa sasa wanawafikishia mbegu hizo wakulima katika maeneo yao.


Kwa upande wake Afisa Kilimo wa chama hicho Vivian Makuto amesema kama ulivyo mlengo wa chama ni wa kuwahudumia wakulima kuanzia wanapoanza kulima hadi kuvuna kwa kuwapatia ushauri na mbinu za kufanya kilimo chenye tija na mtandao wa masoko.
Ameeleza kuwa katika kuhakikisha mbegu hizo zinawafikia wananchi kama ilivyokusudiwa, zinapofika wanazipokea na kuzihifadhi kwenye ghala lao kuu kisha kuzisambaza katika vyama vya Msingi.


Amesema katika kuhakikisha ubora huo unazingatiwa, wameingia mkataba na kampuni mbili zinazosambaza mbegu ambazo ni East Africa Seeds na Meru ambao ni rahisi kuwabana endapo mbegu zao zitabainika kuwa na viwango duni.
Share To:

Post A Comment: