Kushoto ni Afisa Lishe Mradi wa ENRICH unaotekelezwa na Shirika la World Vision , Stella Mbuya  na Afisa Jinsia na Utetezi wa Shirika la World Vision kupitia mradi wa ENRICH, Magreth Mambali wakionesha alama ya Usawa wa Kijinsia.
Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Wanawake wajawazito wamekumbushwa umuhimu wa kuhudhuria Kliniki angalau mara nne katika kipindi chote cha ujauzito ili waweze kupata huduma zote za msingi ili wajifungue salama kupunguza vifo vya uzazi vya mama na mtoto. 

Rai hiyo imetolewa na Afisa Lishe Mradi wa ENRICH unaotekelezwa na Shirika la World Vision katika mikoa ya Shinyanga na Singida, Stella Mbuya wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika Machi 8,2020 katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga. 
Mbuya alisema endapo mama mjamzito atahudhuria kliniki itamsadia kupata huduma zote za msingi katika kipindi chote cha ujauzito ili aweze kujifungua salama ili kupunguza vifo vya uzazi na mtoto ambavyo pia husababishwa na Lishe duni. 
“World Vision kupitia mradi wetu wa ENRICH,tunahamasisha akina mama kula vyakula kwa kuzingatia mlo kamili unaoundwa na makundi matano ya chakula ili kuimarisha afya ya uzazi na lishe kwa mama na mtoto aliyepo tumboni”,alisema Mbuya. 
“World Vision pia tunaendelea kuwahamasisha matumizi ya maziwa ya mbuzi kwa sababu maziwa ya mbuzi yana uwiano wa virutubishi/viini lishe vilivyopo kwenye maziwa ya mbuzi yanakaribiana sana na maziwa ya binadamu tofauti na wanyama wengine ama maziwa ya kopo”,alisema Mbuya. 
Mbuya aliwakumbusha akina mama wajawazito kutumia vidonge vya madini chuma na Asidi ya Foliki ‘Folic acid sambamba na viazi lishe na mboga za majani yakiwemo matembele kwa ajili ya kuongeza damu mwilini ili kukabiliana na vifo vinavyotokana na upungufu wa damu. 
Kwa upande wake,Afisa Jinsia na Utetezi wa Shirika la World Vision kupitia mradi wa ENRICH unaofadhiliwa na serikali ya Canada, Magreth Mambali aliwataka wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu 2020. 
“Tunapoelekea kwenye uchaguzi Mkuu,World Vision tunasisitiza kumpa mwanamke nafasi katika nyanja zote ikiwemo kiuchumi na kisiasa.Tunapenda mwanamke ashiriki katika ngazi za maamuzi kuanzia ngazi ya familia mpaka taifa kwa sababu wanawake tunaweza na tumeshuhudia wanawake wengi wanafanya vizuri katika masuala ya uongozi. Mfano Mzuri ni mama yetu Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan”,alieleza Mambali. 
Mambali aliitaka jamii kuwalinda watoto wa kike dhidi ya mimba na ndoa za utotoni na kutomaliza masomo shuleni akibainisha kuwa mlinzi wa kwanza wa mtoto wa kike ni jamii inayomzunguka. 
Katika hatua nyingine alifafanua kuwa,World Vision kupitia mradi wa ENRICH inatekeleza afua zake kwa kuunda vikundi mbalimbali ikiwemo vikundi vya ‘Baba wanaojali’ ambao wamepata mafunzo ya kuwa baba wanaojali familia zao na kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto. 
Alivitaja vikundi vingine kuwa ni VICOBA kwa wanawake,klabu za afya ya uzazi kwa vijana katika shule za msingi na sekondari na vikundi vya Sauti ya Umma na Utendaji ambavyo vinajihusisha na utoaji elimu kwa wanawake juu ya umuhimu wa kuhudhuria kliniki na kujifungulia katika vituo vya afya. 
Kwa upande Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Shinyanga, Tedson Ngwale aliwapongeza World Vision kwa kuendelea kushirikiana na serikali kuhamasisha wanawake kuzingatia lishe ili kupunguza vifo vitokanavyo na lishe duni. 
Naye Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) alitoa wito kwa wazazi na walezi kupeleka watoto shule na kutowaozesha wangali wadogo huku akiwahamasisha wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu 2020. 
Kauli mbiu ya Maadhimisho ya siku ya wanawake duniani Machi 8,2020 ni “Kizazi cha Usawa kwa Maendeleo ya Tanzania ya sasa na ya baadae”.
ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (katikati) akipokea maandamano ya wadau mbalimbali wa haki za wanawake na watoto wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika Machi 8,2020 katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.Kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Mhe. Hoja Mahiba. Kushoto ni Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Kaimu ni James Bwana. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakiwa wamebeba bango lenye ujumbe wa ' Mlinde Mtoto wa kike, Mpe Mwanamke Nafasi' na Kauli Mbiu ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2020 ' “Kizazi cha Usawa kwa Maendeleo ya Tanzania ya sasa na ya baadae”.


Askari polisi wanawake wakiwa kwenye maandamano wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akizungumza kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga ambapo alitoa wito kwa wazazi na walezi kupeleka watoto shule na kutowaozesha wangali wadogo.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akizungumza kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga na kuwahamasisha wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu 2020. 
Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Shinyanga, Tedson Ngwale akilipongeza shirika la World Vision kwa kuendelea kushirikiana na serikali kuhamasisha wanawake kuzingatia lishe ili kupunguza vifo vitokanavyo na lishe duni. 
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakiwa na  matembele na viazi lishe,wameshikilia vipeperushi kwenye banda lao la maonesho kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakiwa wameshikilia vipeperushi kwenye banda lao la maonesho kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Viazi Lishe vikiwa kwenye banda la World Vision kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga
Afisa Lishe Mradi wa ENRICH unaotekelezwa na Shirika la World Vision katika mikoa ya Shinyanga na Singida, Stella Mbuya akionesha mboga za majani 'matembele' ambayo akina mama wajawazito wanashauriwa kutumia ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa damu.
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakiwa na mbuzi kwenye bando lao la maonesho wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakionesha alama ya Usawa wa Kijinsia wakati Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Maafisa kutoka Shirika la World Vision kupitia Mradi wa ENRICH wakionesha alama ya Usawa wa Kijinsia wakati Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoa wa Shinyanga yaliyofanyika katika kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Share To:

msumbanews

Post A Comment: