Watu 27 waliofanyiwa uchunguzi kama wameambukizwa ugonjwa wa corona, akiwepo dereva wa taxi ambaye alimbeba mgonjwa wa kwanza Isabella Mwampamba wamebainika hawana virusi vya ugonjwa huo.

Hayo yamesemwa na mkurugenzi msaidizi wa kitengo cha ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko katika Wizara ya Afya, Dk Janeth Mghamba akiwa na mtaalam wa majanga wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Faraja Msemwa. 

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Arusha, maafisa hao wa Wizara ya Afya nchini Tanzania, wamesema watu hao 27 walichukuliwa sampuli baada ya kubainika kuwa walikutana na dereva wa teksi ambaye alimbeba mgonjwa wa kwanza wa  Corona nchini Tanzania.

"Watu hawa walikuwa karibu na dereva na baada ya kuchukuliwa vipimo na kupelekwa maabara kuu iliyopo jijini Dar es Salaam wamebainika hawajaambukizwa." Amesema Dk Mghamba. 

Pamoja na hayo amesema kuwa watu hao, wataendelea kufuatiliwa hadi vitakapofanyika vipimo vya mara tatu kama ambavyo Shirika la Afya Duniani WHO imeagiza.
Share To:

Post A Comment: