Wananchi wakipita kwa shida eneo lenye mafuriko 
Mkuu wa wilaya Songwe Samweli Jeremiah akiangalia barabara iliyoharibiwa vibaya na mvua


Na Esther Macha, Songwe

MADEREVA  magari ya mazigo ya zaidi ya 30  wamekwama kuendelea na safari kwa muda wa Siku sita sasa  kufuatia kipande cha barabara ya Chang'ombe kwenda Mkwajuni wilayani Chunya Mkoa wa Songwe yenye urefu wa kilometa 2.3  kusombwa na mafuriko .

Wakizungumza na Msumba News jirani na kijiji cha kanga  jirani na eneo ambayo mafuriko yametokea  baadhi ya madereva walisema kuwa mvua kubwa ilinyesha ijumaa ya wiki iliyopita na hivyo kusababisha mafuriko baada ya mto lupa kuvunja kingo za Mto na hivyo maji kukosa mwelekeo .

 Leo Siku ya sita  na tulikuwa hatujui kama kulitokea mafuriko tunahofia mizigo tunayosafirisha kuharibika lakini tangu Jana tumepata matumaini kuna kampuni ya Madini ya Shanta imeleta vifaa na kuanza kumwaga vifusi vya mawe kuziba maeneo yaliyosombwa na maji lakini kimsingi hali ni mbaya sana kwetu sisi madereva kwani kuna baadhi ya magari yamekwama kwenye tope na yana mizigo." alisema dereva Raphael Mwambaje.

Aliongeza kuwa" Hapa madereva wengi wameenda mjini na magari wameecha hapa kwani hakuna huduma hata za chakula na eneo ambalo tumekwama ni polini kabisa lakini tunashukuru serikali inaonyesha ina ushirikiano mzuri na wawekezaji na ndio maana tunaona kazi inaendelea"alisema.

Abiria Aziza Mwanjala mfanyabishara na Mkazi wa Mkoa wa Songwe, alisema kuwa ana Siku ya tatu sasa wamekwama kuendelea na safari na kwamba alikuwa akipeleka bidhaa mnadani  amepata hasara kwani mizigo haijaingia kwenye mzunguko


Mkuu wa Wilaya ya Mbozi  Samwel Jeremiah ambaye amefika eneo la tukio, amesema kutokana na hali ilivyo sasa barabara hiyo itafungwa kwa Siku mbili kuanzia leo Februari 9  ili kupisha matengenezo yanayofanywa na Kampuni ya uchimbaji madini ya Shanta kwa kushirikiana na Wakara wa Barabara (TANROAD) Mkoa wa Songwe.


Alisema awali baada ya kutokea mafuriko hali ilikuwa mbaya wakalazimika kuwashirikisha wadau wa kampuni ya Shanta ambao wameungana na serikali na kufika eneo la tukio na kuanza kazi ya kuleta vifaa na kumwaga mawe ya kuziba mashimo ambapo kwa Siku mbili  ambayo tumefunga barabara nadhani  kazi itakwisha na magari yataanza kusafiri.

"Tunashukuru Sana hii kampuni ya Shanta kwa msaada mkubwa wa kutengeneza barabara maana hali ilikuwa mbaya tunaomba wasichoke "alisema.


Meneja Utawala wa Kampuni  madini ya Shanta, Saimon Rweyemamu ,alisema kwa sasa watahakikisha kazi inakamilika leo ili kuwezesha wananchi kupata huduma ya usafiri ikiwa ni pamoja na magari ya mizigo zaidi ya 30 yaliyokwama kwa siku tano sasa lengo ni kusaidiana na serikali kutatua changamoto za wananchi.

Lengo letu ni kusaidiana na serikali ktk kuhakikisha wananchi wanatatua changamoto zao "alisema meneja huyo.

Mhandisi Matengenezo wa Tanroad Mkoa wa Songwe, Nyembo Mhaga alisema kuwa mafuriko hayo yalisabishwa na kingo za mto Lupa kubomoka kutokana na kuzidiwa na maji na hivyo kusababisha kipande cha barabara chenye urefu wa kilometa 2.3 kusombwa na maji.

Alisema kwa sasa wanatafuta mwarobaini wa kuthibiti mafuriko katika eneo hilo na kwamba hata mwaka jana yalitokea na waliweza kuthibiti lakini mvua za mwaka huu zimeleta madhara makubwa na kwamba kwa ushirikiano uliopo kazi ya kuziba mashimo itakamilika na magari yataanza kupita .

Mwisho
Share To:

Francis Godwin Mzee wa matukiodaima

Post A Comment: