Kamanda wa polisi mkoa wa Iringa Juma Bwire
...........
Jeshi la polisi mkoa wa Iringa linawashikilia raia wawili wa China kwa kutuhumiwa kutapeli madini wachimbaji wadogo wa wilaya ya Ludewa mkoani Njombe madini yao na kutoroka nayo .
Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Iringa ACP Rienada Milanzi alimweleza mwandishi wa habari hizi jana kuwa watuhumiwa hao Lin Fangquo (55) na Wei Sical (34) walikamatwa majira ya saa 6.30 mchana katika eneo la Mazombe Mji wa Ilula wilaya ya Kilolo katika barabara kuu ya Iringa – Dar es Salaam disemba 31 mwaka jana wakijaribu kutoroka .
Milanzi alisema kuwa kukamatwa kwa raia hao wa China kulikuja baada ya kuwepo kwa taarifa za kipolisi zilizokuwa zikiwatafuta watuhumiwa hao ambao walikuwa wanatafutwa na jeshi la polisi mkoa wa Njombe kwa tuhuma za kuwatapeli wachimbaji wadogo madini yao bila kuwalipa .
“ Jarada la kesi ya watuhumiwa hao lipo wilaya ya Ludewa mkoa wa Njombe ambapo walikuwa wakitafutwa kwa jarada namba LDW/IR/548/2019 jeshi la polisi limefanya kuwakamata kutokana na RB hiyo ila undani wa tuhuma zao upo mkoani Njombe “ alisema
Kuwa watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa na viroba vitatu vyenye mawe yenye uzito mbali mbali mifuko mitatu mmoja ukiwa na Kilo 43.40 za mawe yanayodhaniwa ni madini ya kopa na mfuko wenye kilo 7.25 na mfuko wa tatu ulikuwa na kilo 9.5 ilikuwa na mawe yanayodhaniwa kuwa na madini ya makaa ya mawe .
Alisema kuwa sambuli za mawe hayo zimepelekwa kwa wataalamu wa madini ili kuchunguzwa Zaidi kabla ya kusafirishwa kwenda mkoani Njombe kwa ajili ya kufikishwa mahakamani kwa tuhuma zinazowakabili .
Kamanda wa polisi wa mkoa wa Njombe Hamisi Issa alipopigiwa simu na mwandishi wa habari hizi ili kujua undani wa tukio hilo na thamani ya madini ambayo wachimbaji wadogo Ludewa walidai kutapeliwa alisema kuwa bado wapo kwenye uchunguzi Zaidi ili kujua suala hilo kwa kina kamanda huyo alisema wachina hao wamekuwa wakijishughulisha na ujenzi wa barabara.
Post A Comment: