NA ANDREW CHALE, KILIMANJARO

KUFUATIA maboresho mbalimbali katika Sekta ya Afya hapa Nchini Hospitali ya Rufaa ya Mawenzi ya Mkoa  wa Kilimanjaro imeweza kufanya upasuaji wa kuondoa ukungu wa jicho kwa wagonjwa 640.

Akizungumza na waandishi wa habari pamoja na Timu ya Maafisa Habari wa Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Kaimu Mganga  Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dkt. Jumanne Kiria alisema kuwa utoaji wa huduma  umeimarishwa kufuatia uwepo wa vifaa tiba pamoja na wataalam katika maeneo mbalimbali.

Amesema kuwa katika uboreshaji wameongeza vitanda hadi kufikia 300  hali ambayo imefanya wagonjwa wote kulazwa kwenye vitanda pamoja na kupunguza vifo vya wajawazito  kwa asiliamia 100.

Dkt.Kiria amesema katika kipindi cha miaka minne ya Dk.Magufuli hospitali hiyo imefanikiwa kufanya upasuaji wa  kuondoa ukungu wa jicho kwa wagonjwa 640 pamoja na kupandikiza kioo cha jicho kwa wagonjwa watatu.

“Hospitali imepunguza rufaa mbalimbali kwa wagonjwa ikiwa ni serikali kuwekeza kwa vifaa na mashine za kisasa hii kwetu imetufanya kuendelea kutoa huduma bora za afya kwa wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro na maeneo mengine”amesema Dkt. Kiria.

Dkt. Kiria amesema kuwa serikali katika uwekezaji imejenga jengo la kisasa lililogharimu sh.milioni 800 kwa ajili ya magonjwa ya mlipuko ambapo liko katika hatua za mwisho ya kuanza kutumika hali ambayo itasaidia kuboresha huduma za afya kwa magonjwa mbalimbali ya mlipuko.

Amesema tangu kuingia kwa serikali ya awamu ya Tano upatikanaji wa dawa katika hospitali hiyo ni asilimia 90 lakini tutafikia asilimia 100 kutokana na mikakati ya serikali ya uwekezaji kwenye sekta ya afya.

Aidha amesema serikali imejenga jengo la mama na mtoto pamoja na huduma zote zitakuwa katika jengo hilo hali ambayo   kwani hakuna mgonjwa anaweza kukosa dawa .

Mwisho.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: