Na Azmala Said - Dar es salaam
Mkuu wa Wilaya  ya Ilala Mhe. Sophia Mjema amewataka wafanyabiashara wa soko la Buguruni waliohama katika vizimba na kufanya biashara nje ya soko kwa kigezo cha kuwa na Kitambulisho cha Ujasiriamali warudi mara moja.

Agizo hilo amelitoa Oktoba 30/2019 katika ziara yale kufuatia malalamiko ya baadhi ya wafanyabiashara wa soko hilo ambapo amesema wale watakaokaidi watachukuliwa hatua za kisheria.

Aidha katika kuona suala hilo linafanyiwa kazi, amemuagiza Afisa masoko,Ally Baruani , kufanya kikao na wafanyabiashara hao mara baada ya ziara kumalizika ili kuwarudisha ndani ya soko kwani kitendo hicho kinainyima Manispaa mapato. 

Mkuu huyo wa wilaya amesema soko hilo lipo kwa ajili ya manufaa ya wafanyabiashara wote na sio kwa watu wachache.

"Kwa hili sitowasamehe, mnawaumiza wenzenu, kwaninni mkwepe ushuru wakati wenzenu wanalipa, nataka mrudi haraka na wasiotaka tunawachukulia hatua, " amesema Mjema.

Aidha amesema kutumia vitambulisho vya Mjasiriamali ni kosa kubwa kwani mfanyabiashara yeyote anayefanya sokoni kwa kupangiwa kizimba anapaswa kulipa ushuru kwa mujibu wa sheria za soko na utaratibu, kwani kutofanya hivyo kunaikosesha serikali mapato.

Amesema anatambua wote wafanya biashara lakini kila mfanyabiashara anatambulika kwa mujibu wa sheria na kanuni , hivyo wanaostahili vitambulisho vya Mjasiriamali na mlipa ushuru sifa zao zinatofautiana.

Mbali na wakwepa ushuru amewataka madalali wa biashara waache kuwakandamiza wafanyabiashara badala yake watumie mikataba katika makabidhiano yao ya kibiashara.

Aidha amesema wale madalali watakaoonekana wanakiuka Sheria wataondolewa katika soko hilo.



Kwa upande wa Mkurugenzi Manispaa ya Ilala Mhe. Jumanne Shauri, ameshauri kuwepo kwa mikataba maalumu ya kisheria kati ya mfanyabiashara na dalali ili kila mmoja kuweza kunufaika

Share To:

msumbanews

Post A Comment: