Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce
Ndalichako ameupongeza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) kwa
kutenga kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuwawezesha
wanataaluma kufanya tafiti zaidi hasa zinazogusa jamii moja kwa moja.
Waziri Ndalichako ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam
wakati akifunga maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha
Dar es Salaam ambapo amesema tafiti ni muhimu katika kuleta maendeleo
kwa kujenga na kukuza uchumi wa viwanda nchini.
Prof. Ndalichako amesema serikali ya Awamu ya Tano
imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda lengo likiwa kuhakikisha kunakuwa
na viwanda ambavyo vinatumika kuzalisha bidhaa na kutoa huduma
zitakazotosheleza jamii ya Kitanzania na kusaidia kuongeza ajira kwa
vijana.
Akizungumzia Wiki ya Utafiti Waziri Ndalichako amesema
inawapa wadau wa utafiti na ubunifu jukwaa la kufahamu shughuli za
utafiti zinazofanyika; sehemu gani kuna mapengo na changamoto; na
mikakati gani ya kimipango inahitajika ili kuziba mapengo pamoja na
kutatua changamoto zilizobainika.
"kama taifa, tuna wajibu mkubwa na fursa nyingi za kuweza
kutumia utafiti, ubunifu na ujasiriamali hususan kupitia sekta ya elimu
ili kuongeza kasi ya maendeleo ya viwanda nchini.
Kufanya hivyo,
kutawezesha kutekeleza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya Mheshimiwa
Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Dira ya Taifa ya 2015, ya kuhakikisha
kuwa Tanzania inafikia uchumi wa kati kupitia viwanda." Amesisitiza
Waziri NdalichaKo
Post A Comment: