Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba (Mb) akijibu swali bungeni leo tarehe 17 Aprili 2019 wakati wa mkutano wa kumi na tano wa Bunge la Bajeti Jijini Dodoma. (Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)


Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma

Katika mpango kabambe wa Tanzania wa kufanya kilimo cha umwagiliaji kuwa kipaombele kikuu yaani ASDP II kauli ya kuwa kilimo ni maji inajipambanua zaidi kwani inazingatia matumizi bora ya ardhi na maji.

Katika kuongeza ufanisi na tija katika kilimo kupitia umwagiliaji Serikali imejipanga vyema kuimarisha sekta ya kilimo kupitia mbinu bora za kilimo cha kisasa ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji.

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba (Mb) ameyasema hayo bungeni Jijini Dodoma leo tarehe 17 Aprili 2019 wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe Rehema Juma Migila aliyetaka kufahamu Serikali ina mpango gani wa kuendeleza Kilimo cha Umwagiliaji katika Manispaa ya Tabora, kwa kutumia maji kutoka Bwawa la Igombe baada ya ujio wa maji kutoka Ziwa Victoria kufika Tabora.

Mhe Mgumba alisema kuwa wakati wa kupanga matumizi ya maji kutoka katika chanzo, utunzaji wa mazingira na matumizi ya jamii hupewa umuhimu zaidi kabla ya matumizi mengine.

Ujenzi wa miundombinu ya kutoa maji kutoka Ziwa Victoria umelenga zaidi katika kupunguza upungufu wa maji uliopo kwenye Manispaa ya Tabora ambayo kwa sasa inahudumiwa na Bwawa la Igombe. Maji hayo ni kwa ajili ya matumizi ya kijamii tu kwani hayatatosha kwa kilimo cha umwagiliaji.

Alisema kwa kutambua umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo kwa tija na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Wizara ya kilimo kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ina Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji unaotekelezwa kuanzia 2018/2019 hadi 2035/2036 ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo katika Manispaa ya Tabora, mpango huo umejumuisha uboreshaji na ujenzi wa skimu za umwagiliaji za Imalamihayo, Inala, Magoweko na Bonde la Kakulungu.

Aliongeza kuwa rasilimali maji ni muhimu katika jamii na kama itawekwa vizuri matumizi yake katika kila hatua huleta manufaa makubwa kwa kilimo  kupitia umwagiliaji  na kupata nishati ya umeme kwenye maporomoko.

MWISHO
Share To:

Post A Comment: