Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia) akikiri kuupokea Mwenge wa Uhuru wa mwaka 2019 baada ya kukabidhiwa na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brigedia. Jenerali. Mstaafu Nicodemus Mwangela (kushoto).
Mwenge wa Uhuru wa Mwaka 2019 utakaokimbizwa katika wilaya tatu na Halmashauri Nne za Mkoa wa Rukwa unategemewa kuweka Mawe ya Msingi, kukagua na kuzindua miradi 35 ya maendeleo pamoja na vikundi 11 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ambapo miradi hiyo ina thamani ya Shilingi Bilioni 45,404,104,489.59.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo baada ya kukabidhiwa mwenge wa Uhuru na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brigedia. Jenerali. Mstaafu Nicodemus Mwangela mara tu baada ya kuvuka daraja la mto Momba mbao ndio mpaka wa Mkoa wa Rukwa na Songwe katika Kijiji cha Kilyamatundu, Wilayani Sumbawanga.
Mkuu wa Mkoa amesema kuwa Mwenge wa uhuru ukiwa katika Mkoa wa Rukwa utakimbizwa umbali wa jumla ya Kilomita 832.5 kuanzia tarehe 7 hadi 11, April, 2019 nahatimae kuwakabisdi majirani Mkoa wa Katavi, ambao utakuwa mkoa wa tatu tangu kuwashwa kwake katika mkoa wa Songwe mapema mwezi huu.
Wakati akifafanua michanganuo ya uchangiaji wa miradi hiyo Mh. Wangangabo alisema “Wananchi Shilingi 244,524,500.00 sawa na asilimia 0.5 ya gharama zote.Halmashauri Shilingi 619,611,106.00 sawa na asilimia 1.4, Serikali Kuu Shilingi 16,426,480,402.00 sawa na asilimia 36.2, Wadau wa maendeleo Shilingi 759,489,800 sawa na asilimia 1.7 Aidha, kuna mradi wa uchimbaji makaa ya mawe ambao unathamani ya Shilingi 27,353,998,681.59 mradi huu utakaguliwa, ambao una wastani wa asilimia 60.2 ya gharama zote.”
Kwa upande wake Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2019 aliupongeza uongozi wa mkoa wa Rukwa kwa mapokezi mazuri aliyoyapata na kuwaahidi kutowaangusha wananchi katika ukaguzi wake wa miradi ambayo Mwenge wa Uhuru utaipitia.
Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2019 ni Maji ni haki ya kila Mtu, tutunze vyanzo vyake na tukumbuke kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa”

Share To:

Post A Comment: