Mbunge
wa Itilima, Njalu Silanga (CCM), ameitaka serikali kutengeneza mfumo
mpya wa kuhakikisha zao la pamba linafanya vizuri sokoni.
Aidha,
amelalamikia uendeshaji wa vyama vya ushirika ambapo amesema ushirika
uliopo sasa uko hoi kwani hata maghala yao yalishauzwa.
Akichangia
mjadala wa bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka 2018/19, Silanga
amesema bei ikiwa nzuri na kukiwa na pembejeo za kutosha watazalisha
kilo milioni 2.4 kwa mwaka.
“Kwa
sababu mikoa inayolima pamba ni 17 na tunazo wilaya 56, utaona tu
kwamba hata uzalishaji kwa mwaka huu umepiga hatua ukigawanya wastani
wake ni kama kila wilaya imezalisha tani 10, ambapo tukisimamia jukumu
hili tukalibeba wote tutafanikiwa,” amesema.
Pamoja
na mambo mengine, Silanga amesema hivi karibuni, Waziri Mkuu alitoa
agizo kwa wakuu wa mikoa na wilaya kuunda vikundi lakini kilichofuatia
ni Mrajisi kutengeneza ushirika wake wa miaka 20 ambao wakulima
wanauchukia kiasi kwamba hata sasa hivi ukisema ushirika wanakimbia.
“Mheshimiwa
Waziri, katika bajeti yako umesema umeamua kutoa mfuko wa wakfu katika
zao la pamba lakini kwenye kikotoo huku umeandika Sh 100, sasa ungetupa
majibu tunafanya kitu gani.
“Tukiweka
uzalishaji mzuri na usimamizi mzuri, wakulima wetu wa pamba hawasukumwi
kwa sababu ni wajibu wao na ni biashara yao lakini kadri tunavyotaka
kwenda tunaweza tukatengeneza mazingira ya kuua zao la pamba na itafia
hapa Dodoma.
“Tunarajia kuvuna kilo milioni moja mwaka 2020 na kuendelea, lakini kwa mwendo huu wakulima watakataa kulima na wataacha kulima.
“Nakuomba
waziri tafuta mfumo mzuri na hasa zaidi hili jambo, sisi kule kwetu
tulikuwa na Chama Kikuu cha Ushirika kinaitwa Shirecu, lakini baada ya
Ofisi ya Mrajisi kuingia pale alitengeneza madudu hadi na maghala yetu
yakauzwa ambayo yalikuwa makubwa pale Dar es Salaam.
“Lakini
leo mrajisi huyu amerudi tena na mfumo ule ule ambao umewatesa wakulima
wetu na imewakatisha tamaa. Ningeomba jambo hili tulichulue kwa umakini
mkubwa wenye tija na tujaribu kuweka mifumo ambayo itakuwa rafiki kwa
wakulima ambao wanazalisha kwa moyo mmoja na wanapata fedha zaidi,”
amesema.
Post A Comment: