Mkoa wa Rukwa umejidhihirisha kwa kasi kama kitovu kipya cha kimataifa cha biashara ya madini, hatua inayojengwa na utajiri mkubwa wa rasilimali, miundombinu bora, usalama ulioboreshwa na mifumo rafiki ya Serikali katika usimamizi wa sekta hiyo. Hali hii imeufanya Mkoa huo kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.


Akizungumza Desemba 04, 2025, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Joseph Kumburu, amesema Serikali imeweka mazingira madhubuti ya kuongeza uwekezaji kupitia mabadiliko makubwa katika utoaji wa leseni, usimamizi wa masoko ya madini na kuimarisha miundombinu ya kusafirisha bidhaa ndani na nje ya nchi. 


Amesisitiza kuwa Rukwa sasa inatambulika kimataifa kutokana na aina mbalimbali za madini pamoja na hatua za Serikali kuimarisha utawala bora na kupunguza urasimu katika mchakato mzima wa uwekezaji.


Kwa mujibu wa Mhandisi Kumburu, zaidi ya leseni 480 za madini tayari zimetolewa katika Mkoa wa Rukwa na maombi mengine zaidi ya 600 yanaendelea kushughulikiwa kupitia mifumo ya kidigitali ya Tume ya Madini, hatua iliyoongeza uwazi na kasi ya utoaji wa leseni. Takwimu zinaonesha kwamba kwa mwaka wa fedha 2024/2025, jumla ya tani 337.6 za madini mbalimbali ziliuzwa katika masoko na vituo rasmi vya Rukwa, zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 264, huku Serikali ikikusanya zaidi ya shilingi milioni 18 kupitia mrabaha, ada za ukaguzi na vibali vya usafirishaji.


Aidha, Ofisi ilikusanya jumla ya kiasi cha shilingi milioni 656.2 sawa na asilimia 87.5 ya makusanyo yote kwa mwaka wa fedha 2024/2025.


Rukwa inajivunia aina nyingi za madini ikiwemo dhahabu, shaba, makaa ya mawe, madini ya viwandani, vito na madini ya kimkakati kama helium na rare earth elements. Aidha, kijiografia Mkoa una faida ya pekee kutokana na kupakana na Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), pamoja na kuwa na Bandari ya Ziwa Tanganyika inayorahisisha biashara ya kimataifa na usafirishaji wa vifaa vya uchimbaji.


Kwa upande wa wachimbaji wadogo, Serikali inaendelea kutenga na kupima zaidi ya hekta 13,000 zitakazotumika kuendeleza shughuli za uchimbaji mdogo, ambapo maeneo hayo yanatarajiwa kutoa zaidi ya leseni 700. Mahitaji makubwa ya vifaa vya ujenzi kutokana na miradi ya kimkakati pia yamefungua milango kwa wawekezaji kuanzisha mitambo ya kuzalisha mazao kama kokoto, mchanga, kifusi na mawe.


Mhandisi Kumburu amesema mpango wa Mkoa unalenga kuimarisha masoko ya madini, kupanua masoko mapya ndani na nje ya nchi, kuwaunganisha wachimbaji na taasisi za kifedha pamoja na kuongeza ulinzi na matumizi ya teknolojia kupambana na utoroshaji wa madini. 


Amesema Serikali imewekeza nguvu kubwa katika kuongeza uwazi kwenye mnyororo wa thamani wa madini ili kuvutia wawekezaji na kulinda maslahi ya Taifa.


Aidha, Mhandisi Kumburu ametoa wito kwa vijana wa Mkoa wa Rukwa na mikoa ya jirani kuchangamkia fursa hizo, hasa katika maeneo mapya yanayofunguliwa na Serikali. 


Amesema pia Rukwa kwa sasa imeandaa mkakati wa kuweka kituo cha Mradi mkubwa wa madini ya shaba (Copper Industrial Park) katika Wilaya ya Nkasi ambapo majadiliano yanaendelea kati ya Mkoa na wawekezaji kutoka China baada ya wawekezaji kutembelea nchini na kujiridhisha na uwepo wa madini ya shaba katika Mkoa wa Rukwa na mikoa ya jirani.


“Rukwa imefunguka na sasa ni wakati wa wawekezaji kuchangamkia fursa hizi. Mazingira ya uwekezaji yameboreshwa na rasilimali zipo kwa wingi. Tunawakaribisha wote kuwekeza kwa manufaa ya Rukwa na Taifa kwa ujumla,” amesema.


Kwa ujumla, Rukwa inaendelea kupanda ngazi katika ramani ya uwekezaji Tanzania, ikiwa kama kitovu cha biashara, teknolojia na uchimbaji endelevu wa madini, huku mifumo dhabiti ya usimamizi na fursa nyingi ikiuweka Mkoa huo katika nafasi ya kipekee kwa wawekezaji wanaotafuta mazingira salama na yenye tija.

 


Na Mwandishi Wetu, Banjul

Afrika imeanza sura mpya ya mageuzi katika sekta ya misitu na wanyamapori baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Misitu na Wanyamapori Afrika (AFWC25), Prof. Dos Santos Silayo, kukabidhi rasmi uenyekiti kwa Mr. Ebrima Jawara wa Serikali ya Gambia, hatua iliyoweka mwelekeo mpya wa bara katika kukabiliana na changamoto za karne ya sasa.

Akizungumza katika kikao cha 25 cha AFWC, kilichofanyika Banjul, Prof. Silayo alionya kwamba bara la Afrika liko kwenye shinikizo kubwa linalotokana na kasi ya mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la migongano ya binadamu na wanyamapori, pamoja na mahitaji mapya ya kijamii na kiuchumi yanayoathiri rasilimali asilia. Alisisitiza kwamba Afrika haiwezi tena kutegemea mbinu za kale katika usimamizi wa misitu na wanyamapori.

“Mabadiliko ya tabianchi yamebadilisha mazingira, tabia za watu zimebadilika, na mienendo ya wanyama imebadilika pia. Hatuwezi kuendelea kwa mazoea; tunahitaji ubunifu jumuishi unaotumia sayansi na unaowajibika,” alisema.

Alibainisha kuwa sekta inaweza kuimarika tu ikiwa mataifa yatawekeza katika modeli sahihi za kaboni, teknolojia za kisasa za ufuatiliaji wa misitu, tafiti za mwingiliano wa maji na misitu, mbinu za kisasa za kupunguza uharibifu wa misitu, pamoja na kuimarisha taasisi za jamii ambazo ndizo msingi wa shughuli za uhifadhi.

Katika uchaguzi uliofanyika kwenye kikao hicho, Mr. Ebrima Jawara, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mazingira ya Gambia, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti mpya wa AFWC25. Akipokea wadhifa huo, Jawara alitoa hotuba ya shukrani, akiahidi kuendeleza mageuzi yaliyowekwa na mtangulizi wake na kusisitiza kwamba mustakabali wa uhifadhi wa Afrika unahitaji dira ya pamoja, uongozi unaotegemea ushahidi wa kisayansi, na ushirikiano wa kikanda.

Aidha, viongozi kutoka Rwanda, Chad na Botswana waliteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Tume, uteuzi uliopongezwa na wajumbe kama ishara ya uwakilishi mpana na mshikamano wa kikanda. Wajumbe pia walimhakikishia Jawara ushirikiano wa karibu, wakisema, “Tupo nyuma yako. Tuendelee kulinda rasilimali zetu na kuimarisha sera zetu.”

“Tunategemea ushirikiano wa viongozi wa nchi na wadau wote. Mwenyekiti Jawara na timu yake wana jukumu la kuimarisha usimamizi wa misitu na uhifadhi wa wanyamapori barani Afrika kwa njia endelevu na ya kisayansi,” alisema Katibu wa AFWC, Edward Kilawe, akisisitiza umuhimu wa uongozi mpya katika kuendeleza ajenda za kikanda.

Katika hatua nyingine, wajumbe kutoka nchi mbalimbali walimpongeza Prof. Silayo kwa uongozi wake katika kipindi kilichokabiliwa na changamoto za tabianchi, ongezeko la shinikizo la ardhi na mahitaji mapya ya kiuchumi.

AFWC25 ni kikao cha kikanda cha wakuu wa sekta ya misitu na wanyamapori barani Afrika, kilichokutana kwa mwaka wa 25 mfululizo kujadili changamoto, kushirikiana mbinu za kisayansi, na kuboresha sera za uhifadhi. Kikao cha mwaka huu, kilichoanza Desemba 1 hadi 5, 2025, kilihusisha wajumbe kutoka nchi zote za Afrika, wakijadili mwelekeo wa usimamizi wa misitu, migongano kati ya binadamu na wanyamapori, na mbinu za kuendeleza mageuzi endelevu ya sekta hiyo.



Tanzania, kupitia Wakala wa Huduma za Misitu (TFS), imeungana na nchi nyingine za Afrika katika warsha ya kimataifa iliyojadili mbinu mpya za kupima na kufuatilia kiwango cha hewa ukaa kinachofyonzwa na miti inayoota nje ya misitu, maarufu kama Trees Outside Forests (TOF).

Warsha hiyo ya siku mbili, Desemba 2 hadi 3, 2025 imefanyika katika Hoteli ya Sigelege, Salima nchini Malawi chini ya uratibu wa Michigan State University (MSU), kwa kushirikiana na vyuo na taasisi za utafiti kutoka Malawi, Senegal na Marekani.

Tanzania inawakilishwa na wahifadhi wawili kutoka TFS, Rogers Nyinondi na Jameseth Lazaro, walioalikwa kutokana na nafasi ya TFS kuratibu utekelezaji wa mpango wa kitaifa wa kurejesha uoto wa asili kupitia African Forest Landscape Restoration Initiative (AFR100). Kupitia mpango huo, Tanzania imeahidi kurejesha takribani hekta milioni 5.2 za maeneo yaliyoharibika ifikapo 2030.

Kwa mujibu wa Mkufunzi Mkuu kutoka Michigan State University (MSU), Prof. David L. Skole, warsha hiyo imetoa hatua kubwa ya kiufundi katika ufuatiliaji wa hewa ukaa kwa kutumia teknolojia za high-resolution satellite remote sensing, deep machine learning na allometric scaling models, mbinu zinazowezesha kutambua na kupima miti mmoja mmoja katika maelfu ya hekta. 

Skole alisema mafunzo hayo, ambayo yamemalizika leo, yamelenga kusaidia nchi wanachama kuimarisha mifumo ya uthibitishaji wa taarifa za urejeshaji mazingira na kuweka msingi thabiti wa usimamizi wa ardhi barani Afrika.

Kwa upande wa Tanzania, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Rogers Nyinondi, alisema ushiriki wa Tanzania umeongeza uelewa wa kitaalamu kuhusu mchango wa miti nje ya misitu, ikiwemo kilimo mseto katika kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi. Huku akibainisha kuwa mbinu mpya walizopatiwa zitaboresha ukusanyaji wa takwimu za kaboni, kuimarisha upangaji wa sera na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya urejeshaji ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Warsha hiyo imewaleta pamoja wanasayansi na wataalamu kutoka Rwanda, Kenya, Tanzania, DRC, Senegal, India na Malawi, pamoja na wadau wa AFR100, kujadili maendeleo ya mradi wa kimataifa unaofadhiliwa na MSU.

 


Mkoa wa Katavi umeendelea kuwa kivutio cha wawekezaji kufuatia maboresho makubwa ya miundombinu, usalama na kasi ya utoaji leseni katika Sekta ya Madini. 

Afisa Madini Mkazi wa mkoa huo, Mhandisi Andrew Mwalugaja, ametoa wito kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuchangamkia fursa zinazopatikana katika dhahabu, shaba, risasi, fedha, nikeli, manganese na madini ya ujenzi.

Amesema kuwa ofisi yake imeongeza kasi ya utoaji leseni, ikiwemo leseni tatu za utafiti na zaidi ya leseni 300 za uchimbaji mdogo na wa kati ndani ya miezi minne. Katika biashara ya madini, leseni 82 tayari zimetolewa kati ya Julai na Oktoba 2025, hatua inayodhihirisha mwamko mkubwa wa uwekezaji.

Serikali imeanzisha masoko mawili ya madini Mpanda na Karema ili kuhakikisha wachimbaji, hususan vijana, wanapata soko la uhakika na kufanya shughuli zao kwa uwazi zaidi. Hadi sasa, mkoa umefanikiwa kuongeza makusanyo ya maduhuli hadi Shilingi bilioni 3.80 ndani ya miezi minne tu.

Wachimbaji na wawekezaji wamesema maboresho ya mazingira ya uwekezaji, matumizi ya teknolojia za kisasa na ushirikiano mzuri na Serikali yameongeza uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali. Kampuni ya Jiuxing Tanzania Mining Company imeeleza kuwa ushirikiano na wataalam pamoja na teknolojia ya froth flotation umeongeza tija, usalama na ujuzi kwa vijana wa Mpanda.

  


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amefanya ziara ya kushtukiza katika huduma ya mabasi ya mwendokasi ya Gerezani - Kimara, ili kujiridhisha na utoaji wa huduma mara baada ya Serikali kuelekeza huduma hiyo irejee katika jiji la Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kusikiliza malalamiko ya wananchi wanaotumia usafiri wa Mwendokasi, ambapo wamelalamika juu ya uchache wa mabasi ya mwendokasi hatua iliyopelekea Prof. Shemdoe kumpigia simu na kumuelekeza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) Bw. Pius Andrew Ng’ingo kuongeza mabasi ya mwendokasi ili yawahudumie wananchi.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe kutembelea huduma ya mabasi ya mwendokasi imepokelewa vizuri na wananchi wanaotumia mabasi hayo, ambapo wamempongeza kwa kitendo chake cha kufanya ufuatiliaji ili kujiridhisha na huduma inayotolewa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe mara baada ya kuapishwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais ya kuwaletea wananchi tabasamu, hivyo ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya kuhakikisha wananchi wanapata tabasabu kupitia huduma zitolewazo na mabasi ya mwendokasi.

 


Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde leo Desemba 2, 2025 amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mkuu wa Fedha wa Kampuni mama ya Perseus na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga, Bi. Lee-Anne de Bruin ambao ni wawekezaji kwenye mgodi wa uchimbaji wa dhahabu wa Nyanzaga uliopo Wilayani Sengerema. Bi. Lee-Anne de Bruin aliongozana na Bw. Matt Cavedon, Meneja Mkuu na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga na Bw. Isaac Lupokela, Afisa Mkuu wa Fedha wa Mradi wa Nyanzaga.

Mazungumzo hayo yaliangazia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika utekelezaji wa uanzishwaji wa mgodi huo ambao unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi wa Nchi yetu na wananchi wa Sengerema.

Aidha, Waziri Mavunde aliwahakikishia wawekezaji wa Perseus kuwa Wizara itaendelea kuwa bega kwa bega na wawekezaji katika kufanikisha uendelezaji wa Mgodi wa dhahabu wa Nyanzaga ili uweze kuleta mafanikio kwenye uchumi wa Tanzania na kusaidia upatikanaji wa Ajira kwa Watanzania wengi.









Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Wenyeviti wa Serikali za Mitaa pamoja na Watendaji wa Mitaa katika Halmashauri ya Mji Handeni wamepatiwa mafunzo maalum ya uongozi na utawala bora, yanayolenga kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao, hususan usimamizi wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika Desemba 1, 2025, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka viongozi hao kutumia kikamilifu ujuzi walioupata ili kuboresha utendaji katika maeneo wanayosimamia.

Amesema viongozi wa mitaa wana nafasi muhimu katika kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa ubora unaotakiwa, kwa kuzingatia maslahi mapana ya wananchi na matumizi sahihi ya rasilimali.

Mhe. Nyamwese amesisitiza pia umuhimu wa kudumisha amani ya nchi, akibainisha kuwa ni urithi wenye thamani mkubwa uliopatikana kupitia juhudi za viongozi wa kizazi kilichotangulia, hivyo ni wajibu wa kizazi cha sasa kuithamini, kuilinda na kuikuza kwa ustawi wa taifa.

Awali, akifunga mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amewataka Wenyeviti na Watendaji wa Mitaa kutumia mafunzo hayo kuongeza ufanisi na kuleta matokeo yenye tija katika maeneo yao ya kazi.

Aidha, amewahimiza kuzingatia weledi, uwajibikaji na uadilifu katika usimamizi wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa wananchi wana matarajio makubwa kutoka kwao katika kusukuma agenda za ustawi wa jamii.

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka wananchi wa wilaya hiyo kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (iCHF) ili kunufaika na matibabu nafuu na kupunguza mzigo wa gharama za huduma za afya katika ngazi ya familia.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika Kata ya Msasa, Mhe. Nyamwese amesema kujiunga na bima hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, ambao ni miongoni mwa ahadi alizoahidi kuzitekeleza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya siku 100 baada ya kuchaguliwa kwake.

Amesema iCHF imeendelea kuwa mkombozi kwa wananchi wengi kutokana na kuwezesha upatikanaji wa huduma bora kwa gharama nafuu, hivyo kutoa nafasi kwa familia kupanga matumizi mengine ya kimaendeleo.

“Afya bora ni nguzo muhimu ya uzalishaji. Kila kaya inapaswa kuwa na bima ili huduma za matibabu zipatikane kwa wakati bila kuathiri uchumi wa familia,” amesema.

Awali, akiwasilisha taarifa ya mapambano dhidi ya Ukimwi wilayani humo, Mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Joyce Gideon, amesema halmashauri inaendelea kufanya vizuri katika kuwafikia wananchi wanaoishi na VVU.

Amesema watu 205 waliobainika kuwa na maambukizi wameanza dawa za kufubaza virusi, huku asilimia 99 ya watu wanaoishi na VVU wakijua hali zao. Aidha, aliongeza kuwa asilimia 98 ya wanaotumia dawa hizo wana kiwango kidogo sana cha virusi mwilini, ishara ya mafanikio makubwa ya matibabu.

Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani 2025 yamefanyika yakiwa na kaulimbiu: “Imarisha Mwitikio, Tokomeza UKIMWI”.

 




Na Oscar Assenga,MKINGA

WAKULIMA wa Mwani Katika Maeneo ya Boma Subutini Kata ya Boma wilayani Mkinga mkoani Tanga wameitaka Serikali kuona namna ya kuzibiti uvuvi wa kokoro ambao ndio chanzo kikubwa cha kuathiri viumbe hai wa bahari na mazao ya mwani.

Walitoa wito huo mwishoni mwa wiki katika mdahalo wa wavuvi na wakulima wa mwani katika Kata ya Boma wilayani Mkinga ikiwa ni muendelezo wa mradi wa kujenga uwezo kwa matumizi ya rasilimali za bahari ngazi ya kata.

Mradi huo unaendeshwa na Shirika la Umoja wa Wasaidizi wa Sheria wilayani Mkinga (Uwashem) ukifadhiliwa na Shirika la 4H Tanzania pamoja na We World ambapo kwa sasa utasaidia kuwaweka kwenye hali ya amani ili waweze kushirikiana kwa pamoja kufanya kazi bila kuwepo mvutano wowote.

Akizungumza katika mdahalo huo Mwaita Miraji alisema kwamba uvuvi wa kutumia kokoro umekuwa kikwazo kikubwa kwa ustawi wa viumbe vya baharini lakini pia kuharibu zao la mwani jambo ambalo linapelekea kuwarudisha nyuma kimaendeleo.

Alisema kwamba wanaishukuru Serikali kwa kuzibiti na kutokomeza uvuvi haramu katika maeneo mbalimbali hapa nchini lakini hivi sasa wanawaomba waelekeze nguvu kwenye kutekeleza uvuvi wa kokoro ambao nao umekuwa ukileta athari kubwa.

“Tunaiomba Serikali itumie mbinu walizotumia kutokomeza uvuvi haramu wautumie kutokomeza wa Kokoro ambao umekuwa ukileta athari kubwa hususani katika mazao ya mwani yaliyopo baharini”Alisema

Aidha alisema kwamba uvuvi wa kokoro sio mzuri kutokana na kwamba unachangia kuharibu mazalia ya bahari pamoja na kuadhimia kwa pamoja uvuvi huo unaathiri ustawi wa viumbe wa bahari na hivyo kupelekea mazao ya bahari kuadimika .

“Tunaomba ikiwezekana uvuvi wa kokoro ubadilishwe jina na kuitwa uhalifu wa Kokoro lengo likiwa kuhakikisha unatokomezwa kwenye jamii lakini Serikali iwekeze nguvu zake katika mapambano ya kutokomeza uvuvi huo “Alisema

Naye kwa upande Gonda Mwaita ambaye ni mkulima wa mwani alitaka Serikali iweke sheria kali za kuwadhibiti wavuvi wanaokamatwa wakivua kupitia kokoro kutokana na kwamba umekuwa ukichangia kuharibu mazalia ya bahari ikiwemo mashamba ya mwani na hivyo kurudisha nyuma juhudi za wakulima hao.

“Lakini pia kuwepo na faini kubwa mtu akikamatwa analipa laki tano kama faini wakati huo tayari unakuwa umeshaharibu mashamba ya mwani baharini huo ni uhalifu hivyo iongezwe kwa lengo la kudhibiti uendelee”Alisema

Awali akizungumza katika mdahalo huo Afisa Mtendaji wa Kata ya Boma Hadija Mganga alisema uwepo wa elimu hiyo itawasaidia wakulima wa mwani kwani wamekuwa hawana amani na ukulima wao unakuwa wa kuzorota kutokana na kuathiriwa na uvuvi wa kokoro na kupelekea mtu mmoja moja kushindwa kujimudu katika uchumi.

Alisema kwamba jambo hilo wakishirikiana na watendaji wa vijiji na kata kusimamia kwa kupewa nguvu ili kuweza kuwatoa kwenye hilo jambo kwa sababu Kata ya Boma ndio kitovu cha shughuli za Mwani na uwepo wa kiwanda kidogo cha ukaushaji wa mwani ili kudhalisha.

Hadija alisema kwamba kwa kuharibu mazao hayo kunarudisha nyuma na kuwavunja moyo hivyo wanalishukuru shirika la uwashem kutoa elimu na wananchi wametoa mapendekezo ya Kamati za BMU zijengewe uwezo na zisimamie hasa majukumu yao.

Alisema mwingiliano wa wavuvi na wakulima wa mwani yakitokea wakibishana na kugombana mwisho wa siku wanaumizani na mwisho wa wiku sio jambo nzuri kwa Taifa na Kamati ngazi ya kata wapo tayari kushirikiana na vyombo vya ulinzi kuweza ktoa taarifa za kina kuhusu hali hiyo chanzo ni nini na wanaamini wakishirikiana kwa pamaoja na kuwa agenda yao kubwa kwenye vikao vyao na hivyo kuweza kupiga vita vitendo hivyo.

Hata hivyo alisema kwa upande wake Mratibu wa Uwashemu Salehe Sokoro alisema kwamba anaamini changamoto ambazo zimeelezwa katika mdahalo huo zimechukuliwa na zitakwenda kufanyiwa kazi ili kukomesha vitendo vya namna hiyo kwenye maeneo husika
Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu-ADEM umepanga kufanya mbio maalumu za marathon zitakazohusisha wadau mbalimbali wa elimu, mashirika na taasisi yanayojihusisha na usimamizi wa elimu, wanachuo wa vyuo mbalimbali katika Mkoa wa Pwani na wananchi wote zikilenga kuhamasisha umoja, amani na utulivu katika Taasisi za kielimu pamoja na kuchangisha fedha kwa ajili ya kuboresha miundo mbinu katika Chuo cha ADEM kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani.

Pichani: Washambuliaji wa Timu ya EWURA (wenye jezi za bluu) wakishambulia timu pinzani wakati wa mchezo huo leo.

MOROGORO.

 Timu ya Mpira wa Wavu kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kung’ara katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMMUTA) baada ya kuichakaza timu ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa seti mbili mfululizo.

Katika mchezo huo uliochezwa leo mkoani Morogoro, EWURA ilipata pointi 25 katika seti zote mbili, huku NEMC ikijitahidi lakini ikibaki na pointi 23 kwenye seti ya kwanza na 17 katika seti ya pili.

Mchezo huo uliovuta hisia za mashabiki ulitawaliwa na kasi, nidhamu na uchezaji wa kimkakati kutoka kwa EWURA, ambao washambuliaji wao walionekana kuwa imara zaidi dhidi ya ngome ya NEMC.

Pichani: Washambuliaji wa Timu ya EWURA (wenye jezi za bluu) wakishambulia timu pinzani wakati wa mchezo huo leo.