Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Prof. Haruni Mapesa amewataka Wanafunzi wa Mwaka wa Kwanza wa Chuo hicho kuhakikisha wanafuata Kanuni, Taratibu na Sheria za Chuo kama zilivyo na zinavyoelekezwa.


Prof. Mapesa ameyasema hayo leo wakati akizungumza na wanafunzi wa mwaka wa kwanza 2025/2026 kwenye kikao kilicholenga kuwakaribisha rasmi wanafunzi hao ambapo pamoja na mambo mengine alielezea historia ya Chuo, Mipango na Maendeleo ya Taasisi kwa Ujumla wake.



Mkuu huyo wa Chuo amewataka Wanafunzi kuwa na nidhamu kwa kufuata sharia na kanuni za ufanyaji wa mitihani, nidhamu katika Mavazi, kuheshimiana baina yao, lakini pia kuwa na nidhamu kwa Wafanyakazi wanaohudumu katika Taasisi hiyo.


Pia Prof. Mapesa amewasihi sana Wanafunzi wa Chuo hicho kujiepusha na matendo maovu ikiwemo kujihusisha na makundi yasiyofaa, kujiepusha na utumiaji wa dawa za kulevya, pamoja na kuhakiksiha changamoto walizonazo wanaziwasilisha sehemu husika ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati badala ya kufanya vurugu.


“ Jukumu lililowaleta Chuoni ni kusoma kwa bidii na kuhakikisha mnafaulu vyema mitihani kwani ndiyo kipimo cha uelewa wa kile ambacho mtakuwa mmefundishwa, lengo likiwa ni kufikia malengo na matarajio mliyojiwekea  katika kutimiza ndoto zenu mlizojiwekea katika maisha.”alisisitiza Prof. Mapesa.


Prof. Mapesa amewataka Wanafunzi hao kuzingatia na kuhakikisha wanakuwa na vitambulisho muda wote wanapokuwa Chuoni, kuhakikisha wanakamilisha Usajili, kutunza Mazingira pamoja na Miundombinu mbalimbali iliyopo Chuoni.



Kwa upande wake Rais wa Serikali ya Wanafunzi Magashi Magina  amewataka Wanafunzi wenzake kuzingatia yale yote yaliyoelekezwa na Mkuu wa Taasisi, ili kujiepusha na usumbufu usio wa lazima.


Kupitia kikao hicho, Wanafunzi walipata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali ambayo yalipatiwa majibu na viongozi kupitia kikao hicho,Kikao hicho kimehudhuriwa na Menejimenti ya Chuo, Serikali ya Wanafunzi, Wafanyakazi Waendeshaji na Wanataaluma.


Imetolewa na:


Kitengo cha Mawasiliano na Masoko


CHUO CHA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE


11.12.2025

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akizungumza na Viongozi Chipukizi wakati wa uzinduzi wa Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Sehemu ya Viongozi Chipukizi wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati akizindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Sehemu ya Viongozi Chipukizi wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati akizindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Wengine ni wageni waalikwa. Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (wakwanza kulia) akimsikiliza Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo (hayupo pichani) wakati akitoa maelezo ya awali kuhusu taasisi hiyo kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri huyo kuzindua rasmi Programu ya Mafunzo kwa Viongozi Chipukizi Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Sehemu ya Viongozi Chipukizi wakifurahia jambo wakati Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) alipokuwa akizindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza jijini Dar es Salaam. Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (wapili kutoka kulia) akiwa katika uzinduzi wa Programu ya Mafunzo kwa Viongozi Chipukizi Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo. Wengine ni Watendaji wa taasisi hiyo. Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (katikati waliokaaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi Chipukizi mara baada ya Naibu Waziri huyo kuzindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Sehemu ya Viongozi Chipukizi wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati akizindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi hao Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Wengine ni wageni waalikwa. Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Taasisi ya UONGOZI mara baada ya kuzindua Programu ya Mafunzo kwa Viongozi Chipukizi Awamu ya Kwanza yaliofanyika jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo.

Na Veonica Mwafisi-Dar es Salaam

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray ametoa wito kwa Viongozi kuendelea kujifunza siku kwa siku ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia na kitamaduni yatakayowezesha kubuni mikakati mbalimbali ya kuboresha utendaji kwa ustawi wa taifa.

Mhe. Qwaray ameyasema hayo leo tarehe 11 Disemba, 2025 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na Viongozi Chipukizi kabla ya kuzindua Programu ya Viongozi hao.

Amesema ili mtu aweze kuwa kiongozi mzuri, ni lazima aendelee kujifunza kila siku kwa lengo la kuweza kukabiliana na changamoto za kiuongozi ikiwemo kubuni mbinu mbalimbali za kusimamia mabadiliko ya kimfumo, kiutawala, kiuchumi, kiteknolojia na kitamaduni yanayojitokeza kila siku.

Mhe. Qwaray amewashukuru na kuwapongeza washirika kutoka Finland na HAUS kwa kukubali kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI kubuni na kuandaa programu hii maalumu kwa viongozi na taifa kwa ujumla kwani ina umuhimu wa pekee katika kuendeleza viongozi nchini Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Aidha, amewasisitiza Viongozi kushirikiana na watumishi walio chini yao kwa kuwaelekeza kazi badala ya kuwaacha na kuwaona ni tatizo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kiongozi usiwe mchoyo kufundisha walio chini yako, tuwafundishe, tunakua, tutengeneze viongozi wa baadae, tusishikilie madaraka, tutengeneze viongozi wengi kadri tuwezavyo, Kiongozi hutakiwi kushikilia kila kitu, shirikisha wenzio ili upate mawazo mapya, kuboresha utendaji na kufikia malengo mahususi yaliyowekwa kwa ustawi wa taifa, Mhe. Qwaray amesisitiza.

Amesema Tanzania inaendelea kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs 2030), Ajenda ya Maendeleo ya Afrika (Agenda 2063) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na malengo hayo yameweka bayana kuwa mabadiliko ya kiuongozi ni muhimu kwani ndiyo nguzo kuu ya kufikia malengo yaliyowekwa huku akitolea mfano Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kuwa imeweka malengo ya kuwa na uchumi wa dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050.

“Ni dhahiri hatuwezi kufikia lengo hili kama tusipojipanga na kuweka mikakati madhubuti ya kutuwezesha kufikia malengo yetu.”

Ametaja moja ya mikakati hiyo ni pamoja na kuwa na nguvu kazi yenye uwezo na motisha pamoja na kuwajengea uwezo viongozi kupitia mafunzo kama haya.

Programu hii ni muhimu sana kwani itasaidia Serikali kuwa na viongozi watakaotimiza matarajio ya wananchi.

“Nina imani kuwa maarifa na ujuzi utakaotolewa kwa washiriki wa programu hii utawapa msingi bora na utayari kuongoza na kutoa huduma bora kwa wanachi.

Mhe. Qwaray amewashauri viongozi kujifanyia tathmini ili kutambua uwezo na udhaifu wao kwani kwa kufanya hivyo itasaidia kuboresha utendaji hasa kwenye eneo la mapungufu.

Akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri kuzindua Programu hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo amesema Taasisi yao imekuwa ikitoa mafunzo mbalimbali ya uongozi ili kuwa na viongozi bora katika taifa.

“Kunaweza kukawa na mifumo mizuri lakini viongozi sio wazuri, hivyo mafunzo tunayoyatoa yanasaidia kuwajenga viongozi kuendana na mifumo mizuri iliyopo, Bw. Kadari ameongeza.

 

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amekutana na Balozi wa Falme za Kiarabu Saudi Arabia, Mhe. Yahya Bin Ahmed Okeish, ambapo wamejadili kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu pamoja na kuongeza fursa za skolashipu kwa vijana.

Prof. Mkenda ameishukuru Saudi Arabia kwa kuongeza nafasi za ufadhili masomo ya jelimu ya juu kutoka 90 hadi 127 kwa wanafunzi wa watanzania, na ameahidi kuwa Serikali itazitumia kikamilifu fursa hizo ili kuwawezesha vijana kupata elimu chini humo.

Ameeleza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha vijana wanapata elimu stahiki katika maeneo ya kimkakati, ikiwemo Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, Sayansi ya Takwimi na Akili Unde.

Kwa upande wake, Mhe. Okeish amesema Saudi Arabia inajivunia ushirikiano wake na Tanzania katika sekta ya elimu na itaendeleza ushirikiano huo katika kutekeleza mikakati ya kuendeleza elimu na ujuzi kwa vijana wa Kitanzania kulingana na vipaumbele vya taifa.

Aidha, ameipongeza Wizara ya Elimu kwa kuwa na Sera Bora ya Elimu na pia mipango yake ya kufanya ziara nchini Saudi Arabia kutembelea vyuo mbalimbali, kubadilisha a uzoefu na kupanua fursa za elimu kwa vijana wa mataifa yote mawili ikiwemo suala la kuimarisha ufundshaji lugha ya kiarabu.

   

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI na Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Disemba 11, 2025 wamekutana jijini Dodoma kujadili kwa pamoja mikakati ya kuimarisha ushirikiano katika kuwawezesha vijana wa Tanzania kupata fursa za elimu, ujuzi na ajira.

Kikao hicho kimeongozwa na Prof. Carolyne Nombo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, pamoja na Jenifa Omolo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana.

Viongozi hao wamejadili njia za kuhakikisha vijana wanapata taarifa sahihi kuhusu fursa za elimu na kuwezeshwa ili kukidhi mahitaji ya soko la ajira na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Prof. Nombo amesema kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya 2014 Toleo la 2023 pamoja na mitaala iliyoboreshwa vinaendelea kumwandaa kijana wa Kitanzania kupata ujuzi unaohitajika katika ulimwengu wa kazi.

Amesisitiza kuwa sera hiyo inatoa nafasi kwa vijana wote, wakiwemo walioacha shule awali, kurejea na kupata elimu kupitia mfumo rasmi na usio rasmi, ikiwemo programu ya IPOSA.

Aidha, Prof. Nombo amebainisha kuwa Serikali inaendelea kupanua fursa za ufundi na mafunzo ya ufundi stadi, mikopo ya elimu, pamoja na ufadhili kupitia Samia Skolashipu, ili kuongeza wigo wa vijana kupata elimu na ujuzi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Jenifa Omolo, ameipongeza Wizara ya Elimu kwa kuanzisha programu nyingi zinazolenga kuwawezesha vijana kujitegemea na kushindana katika soko la ajira. Amesema programu hizo ni muhimu katika kuchochea ushiriki wa vijana katika uchumi wa taifa.

Katika kikao hicho, viongozi hao wamekubaliana kuimarisha upatikanaji wa taarifa za fursa mbalimbali kwa vijana, kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia mafunzo mahususi, pamoja na kuratibu programu zitakazowaunganisha vijana na viwanda ili kupata mafunzo kwa vitendo.

Na; OWM (KAM) - DODOMA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu ameupongeza Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa hatua kubwa ilizochukua katika kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, hususan utoaji wa fidia kwa wafanyakazi wanaokumbana na madhila ya ajali ama ugonjwa unaotokana na kazi.

Na; OWM (KAM) - DODOMA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu amepongeza Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa hatua kubwa ilizochukua katika kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, hususan wafanyakazi wanaokumbana na madhira ya ajali ama ugonjwa unaotokana na shughuli za kazi.

Pongezi hizo zimetolewa Desemba 10, 2025 Jijini Dodoma alipokutana na Menejimenti ya WCF kwa lengo la kujua majukumu ya mfuko huo sambamba na kutoa maelekezo ya kiutendaji yanayolenga kuongeza tija na ufanisi kuendana na maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mhe. Sangu amesema hatua hizo zimechangia kuimarisha imani ya wananchi kwa Mfuko, ambapo wafanyakazi wanaopatwa na madhara kazini wamekuwa wakipatiwa huduma kwa wakati na kwa kiwango kinachostahili, jambo ambalo limeongeza ufanisi na kupunguza usumbufu kwa wafanyakazi waliokuwa na changamoto kazini.

Katika hatua nyingine, Waziri Sangu ameitaka Menejimenti ya WCF kuendeleza ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yao, ikiwemo kubuni mifumo mipya ya kidijitali, kuboresha mbinu za utoaji huduma na kuongeza matumizi ya teknolojia ili kufikia wananchi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Awali, akizungumza, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo, amehamasisha Menejimenti ya Mfuko huo kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu na huduma zinazotolewa na mfuko, ili kuongeza uelewa na kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Aidha, amesisitiza WCF kuimarisha kampeni za uhamasishaji kupitia majukwaa ya kijamii, vyombo vya habari na mikutano ya wadau ili kuhakikisha taarifa sahihi zinawafikia waajiri, wafanyakazi na jamii kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma amesema WCF imejipanga kuendelea kuboresha mifumo ya utoaji huduma ili kuhakikisha madai ya fidia yanashughulikiwa kwa uharaka, uwazi na ufanisi zaidi.

 


Na Oscar Assenga, TANGA

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) umesema kwamba maboresho makubwa yaliyofanywa katika Bandari ya Tanga umepelekea wastani wa kuhudumia meli moja kwa siku tatu kutoka siku saba za awali kutokana na kuongezeka kwa ufanisi mkubwa.

Hayo yalisemwa na Mwakilishi wa Meneja wa Bandari ya Tanga Peter Milanzi wakati wa upokeaji aina mpya ya mzigo wa Lami kupitia Kampuni ya Wakala wa Usafirishaji ya Amura unaosafirishwa kwenda nchi jirani ya Malawi ambao wameamua kutumia Bandari hiyo kutokana na ufanisi wake

Alisema kwamba kutokana na ufanisi huo umepelekea kuvutia wateja wengi kuitumia Bandari hiyo kupitisha shehena mbalimbali za mizigo ikiwemo magari na mizigo mbalimbali ambazo zinakwenda nchi mbalimbali.

“Bandari ya Tanga tumeendelea kufanya vizuri kutokana na maboresho yaliyofanywa na Serikali kupitia Rais Dkt Samia Suluhu na hivyo kuvutia wateja wengi na leo tunapokea aina mpya ya mzigo wa Lami kwa wenzao wa Kampuni ya Amoue wameamua kuitumia Bandari ya Tanga kutokana na ufanisi ambao wanao kwa majaribio wameamua kupitisha makontena sita na kila moja lina mapipa 110 inaenda nchi ya Malawi”Alisema

Alisema kwamba hiyo ni ishara kubwa ya kuaminiwa na wafanyabiashara na watu mbalimbali hivyo wanawaambia wateja waendele kuitumia Bandari hiyo kutokana na wao wanaendelea kuwahudumia kwa ufanisi na kutoa huduma bora kama wenzao Amoura.

“Bandari ya Tanga ni salama na itaendelea kuwa samana na kutoa huduma ya ushushaji wa mizigo na kwa wale waliokwama kwenye Bandari nyengine njooni Tanga mtahudumiwa kwa ufanisi mkubwa na kwa muda mfupi”Alisema Milanzi.

Hata hivyo alisema kwamba kuanzia mwezi Julai mwaka huu wa Fedha 2025/2026 walipangiwa kuhudumia Tani milioni 1.6 ,sasa wastani wa kuhudumia tani laki 137,000 lakini tokea mwezi Julai mwaka huu wamekuwa wakivuka malengo walianza na tani laki 152,000 na baadae wakapanda tani 157,000 na mwezi Septemba –Octoba wamefikisha tani 200,000 kila mwezi.

Alieleza kwamba wanaona malengo ambao wamewekewa watayafikia hayo yote yamekua kutokana na ufanisi wao kwenye kazi na hivyo wateja wameongezeka hatua inayoonyesha watavuta malengo waliopangiwa kutokana na m.

Awali akizungumza mara baada ya mara baada ya kushushwa kwa Shehena hiyo ya Lami –Mwakilishi wa Kampuni ya  Amura ya Dar ,Zakaria Mohamed Nanimuka alisema kwamba kutokana na ufanisi wa Bandari ya Tanga wanategemea kuingiza kontena nyengine 20 zitazohudumiwa kwenye Bandari hiyo.

“Sisi kama Kampuni Amura tumefurahishwa na ufanisi wa Bandari ya Tanga na hakuna malalamiko wala changamoto zozote zile tunashukuru Serikali kwa kuwekeza hapa na sasa sisi wasafirishaji tutaendelea kuitumia katika kuingiza shehena mbalimbali”Alisema

Zakari alisema kwamba wamekuja Tanga kupokea shehena ya mzigo wa Lami kutoka Iran na kushukia Bandari ya Tanga kontena sita zenye tani 125 na kilo 430 ambapo kontena moja lina kuwa na pipa 110 kwa kontena

Alisema kwamba wanashukuru kwa namna walivyohudumiwa wamefanya kazi vizuri na wala hakukuwa na changamoto za aina yoyote ile mzigo wao umeweza kushughulikiwa wamepita scana kwa wakati hivyo wanamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu kwa maboresho makubwa yaliyosaidia kuongeza ufanisi.