Mkoa wa Katavi umeendelea kuwa kivutio cha wawekezaji kufuatia maboresho makubwa ya miundombinu, usalama na kasi ya utoaji leseni katika Sekta ya Madini. 

Afisa Madini Mkazi wa mkoa huo, Mhandisi Andrew Mwalugaja, ametoa wito kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuchangamkia fursa zinazopatikana katika dhahabu, shaba, risasi, fedha, nikeli, manganese na madini ya ujenzi.

Amesema kuwa ofisi yake imeongeza kasi ya utoaji leseni, ikiwemo leseni tatu za utafiti na zaidi ya leseni 300 za uchimbaji mdogo na wa kati ndani ya miezi minne. Katika biashara ya madini, leseni 82 tayari zimetolewa kati ya Julai na Oktoba 2025, hatua inayodhihirisha mwamko mkubwa wa uwekezaji.

Serikali imeanzisha masoko mawili ya madini Mpanda na Karema ili kuhakikisha wachimbaji, hususan vijana, wanapata soko la uhakika na kufanya shughuli zao kwa uwazi zaidi. Hadi sasa, mkoa umefanikiwa kuongeza makusanyo ya maduhuli hadi Shilingi bilioni 3.80 ndani ya miezi minne tu.

Wachimbaji na wawekezaji wamesema maboresho ya mazingira ya uwekezaji, matumizi ya teknolojia za kisasa na ushirikiano mzuri na Serikali yameongeza uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali. Kampuni ya Jiuxing Tanzania Mining Company imeeleza kuwa ushirikiano na wataalam pamoja na teknolojia ya froth flotation umeongeza tija, usalama na ujuzi kwa vijana wa Mpanda.

  


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amefanya ziara ya kushtukiza katika huduma ya mabasi ya mwendokasi ya Gerezani - Kimara, ili kujiridhisha na utoaji wa huduma mara baada ya Serikali kuelekeza huduma hiyo irejee katika jiji la Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kusikiliza malalamiko ya wananchi wanaotumia usafiri wa Mwendokasi, ambapo wamelalamika juu ya uchache wa mabasi ya mwendokasi hatua iliyopelekea Prof. Shemdoe kumpigia simu na kumuelekeza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) Bw. Pius Andrew Ng’ingo kuongeza mabasi ya mwendokasi ili yawahudumie wananchi.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe kutembelea huduma ya mabasi ya mwendokasi imepokelewa vizuri na wananchi wanaotumia mabasi hayo, ambapo wamempongeza kwa kitendo chake cha kufanya ufuatiliaji ili kujiridhisha na huduma inayotolewa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe mara baada ya kuapishwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais ya kuwaletea wananchi tabasamu, hivyo ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya kuhakikisha wananchi wanapata tabasabu kupitia huduma zitolewazo na mabasi ya mwendokasi.

 


Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde leo Desemba 2, 2025 amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mkuu wa Fedha wa Kampuni mama ya Perseus na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga, Bi. Lee-Anne de Bruin ambao ni wawekezaji kwenye mgodi wa uchimbaji wa dhahabu wa Nyanzaga uliopo Wilayani Sengerema. Bi. Lee-Anne de Bruin aliongozana na Bw. Matt Cavedon, Meneja Mkuu na Mkurugenzi wa Bodi ya Mradi wa Nyanzaga na Bw. Isaac Lupokela, Afisa Mkuu wa Fedha wa Mradi wa Nyanzaga.

Mazungumzo hayo yaliangazia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika utekelezaji wa uanzishwaji wa mgodi huo ambao unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi wa Nchi yetu na wananchi wa Sengerema.

Aidha, Waziri Mavunde aliwahakikishia wawekezaji wa Perseus kuwa Wizara itaendelea kuwa bega kwa bega na wawekezaji katika kufanikisha uendelezaji wa Mgodi wa dhahabu wa Nyanzaga ili uweze kuleta mafanikio kwenye uchumi wa Tanzania na kusaidia upatikanaji wa Ajira kwa Watanzania wengi.









Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Wenyeviti wa Serikali za Mitaa pamoja na Watendaji wa Mitaa katika Halmashauri ya Mji Handeni wamepatiwa mafunzo maalum ya uongozi na utawala bora, yanayolenga kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao, hususan usimamizi wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika Desemba 1, 2025, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka viongozi hao kutumia kikamilifu ujuzi walioupata ili kuboresha utendaji katika maeneo wanayosimamia.

Amesema viongozi wa mitaa wana nafasi muhimu katika kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa ubora unaotakiwa, kwa kuzingatia maslahi mapana ya wananchi na matumizi sahihi ya rasilimali.

Mhe. Nyamwese amesisitiza pia umuhimu wa kudumisha amani ya nchi, akibainisha kuwa ni urithi wenye thamani mkubwa uliopatikana kupitia juhudi za viongozi wa kizazi kilichotangulia, hivyo ni wajibu wa kizazi cha sasa kuithamini, kuilinda na kuikuza kwa ustawi wa taifa.

Awali, akifunga mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amewataka Wenyeviti na Watendaji wa Mitaa kutumia mafunzo hayo kuongeza ufanisi na kuleta matokeo yenye tija katika maeneo yao ya kazi.

Aidha, amewahimiza kuzingatia weledi, uwajibikaji na uadilifu katika usimamizi wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa wananchi wana matarajio makubwa kutoka kwao katika kusukuma agenda za ustawi wa jamii.

Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka wananchi wa wilaya hiyo kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (iCHF) ili kunufaika na matibabu nafuu na kupunguza mzigo wa gharama za huduma za afya katika ngazi ya familia.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika Kata ya Msasa, Mhe. Nyamwese amesema kujiunga na bima hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, ambao ni miongoni mwa ahadi alizoahidi kuzitekeleza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya siku 100 baada ya kuchaguliwa kwake.

Amesema iCHF imeendelea kuwa mkombozi kwa wananchi wengi kutokana na kuwezesha upatikanaji wa huduma bora kwa gharama nafuu, hivyo kutoa nafasi kwa familia kupanga matumizi mengine ya kimaendeleo.

“Afya bora ni nguzo muhimu ya uzalishaji. Kila kaya inapaswa kuwa na bima ili huduma za matibabu zipatikane kwa wakati bila kuathiri uchumi wa familia,” amesema.

Awali, akiwasilisha taarifa ya mapambano dhidi ya Ukimwi wilayani humo, Mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Joyce Gideon, amesema halmashauri inaendelea kufanya vizuri katika kuwafikia wananchi wanaoishi na VVU.

Amesema watu 205 waliobainika kuwa na maambukizi wameanza dawa za kufubaza virusi, huku asilimia 99 ya watu wanaoishi na VVU wakijua hali zao. Aidha, aliongeza kuwa asilimia 98 ya wanaotumia dawa hizo wana kiwango kidogo sana cha virusi mwilini, ishara ya mafanikio makubwa ya matibabu.

Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani 2025 yamefanyika yakiwa na kaulimbiu: “Imarisha Mwitikio, Tokomeza UKIMWI”.

 




Na Oscar Assenga,MKINGA

WAKULIMA wa Mwani Katika Maeneo ya Boma Subutini Kata ya Boma wilayani Mkinga mkoani Tanga wameitaka Serikali kuona namna ya kuzibiti uvuvi wa kokoro ambao ndio chanzo kikubwa cha kuathiri viumbe hai wa bahari na mazao ya mwani.

Walitoa wito huo mwishoni mwa wiki katika mdahalo wa wavuvi na wakulima wa mwani katika Kata ya Boma wilayani Mkinga ikiwa ni muendelezo wa mradi wa kujenga uwezo kwa matumizi ya rasilimali za bahari ngazi ya kata.

Mradi huo unaendeshwa na Shirika la Umoja wa Wasaidizi wa Sheria wilayani Mkinga (Uwashem) ukifadhiliwa na Shirika la 4H Tanzania pamoja na We World ambapo kwa sasa utasaidia kuwaweka kwenye hali ya amani ili waweze kushirikiana kwa pamoja kufanya kazi bila kuwepo mvutano wowote.

Akizungumza katika mdahalo huo Mwaita Miraji alisema kwamba uvuvi wa kutumia kokoro umekuwa kikwazo kikubwa kwa ustawi wa viumbe vya baharini lakini pia kuharibu zao la mwani jambo ambalo linapelekea kuwarudisha nyuma kimaendeleo.

Alisema kwamba wanaishukuru Serikali kwa kuzibiti na kutokomeza uvuvi haramu katika maeneo mbalimbali hapa nchini lakini hivi sasa wanawaomba waelekeze nguvu kwenye kutekeleza uvuvi wa kokoro ambao nao umekuwa ukileta athari kubwa.

“Tunaiomba Serikali itumie mbinu walizotumia kutokomeza uvuvi haramu wautumie kutokomeza wa Kokoro ambao umekuwa ukileta athari kubwa hususani katika mazao ya mwani yaliyopo baharini”Alisema

Aidha alisema kwamba uvuvi wa kokoro sio mzuri kutokana na kwamba unachangia kuharibu mazalia ya bahari pamoja na kuadhimia kwa pamoja uvuvi huo unaathiri ustawi wa viumbe wa bahari na hivyo kupelekea mazao ya bahari kuadimika .

“Tunaomba ikiwezekana uvuvi wa kokoro ubadilishwe jina na kuitwa uhalifu wa Kokoro lengo likiwa kuhakikisha unatokomezwa kwenye jamii lakini Serikali iwekeze nguvu zake katika mapambano ya kutokomeza uvuvi huo “Alisema

Naye kwa upande Gonda Mwaita ambaye ni mkulima wa mwani alitaka Serikali iweke sheria kali za kuwadhibiti wavuvi wanaokamatwa wakivua kupitia kokoro kutokana na kwamba umekuwa ukichangia kuharibu mazalia ya bahari ikiwemo mashamba ya mwani na hivyo kurudisha nyuma juhudi za wakulima hao.

“Lakini pia kuwepo na faini kubwa mtu akikamatwa analipa laki tano kama faini wakati huo tayari unakuwa umeshaharibu mashamba ya mwani baharini huo ni uhalifu hivyo iongezwe kwa lengo la kudhibiti uendelee”Alisema

Awali akizungumza katika mdahalo huo Afisa Mtendaji wa Kata ya Boma Hadija Mganga alisema uwepo wa elimu hiyo itawasaidia wakulima wa mwani kwani wamekuwa hawana amani na ukulima wao unakuwa wa kuzorota kutokana na kuathiriwa na uvuvi wa kokoro na kupelekea mtu mmoja moja kushindwa kujimudu katika uchumi.

Alisema kwamba jambo hilo wakishirikiana na watendaji wa vijiji na kata kusimamia kwa kupewa nguvu ili kuweza kuwatoa kwenye hilo jambo kwa sababu Kata ya Boma ndio kitovu cha shughuli za Mwani na uwepo wa kiwanda kidogo cha ukaushaji wa mwani ili kudhalisha.

Hadija alisema kwamba kwa kuharibu mazao hayo kunarudisha nyuma na kuwavunja moyo hivyo wanalishukuru shirika la uwashem kutoa elimu na wananchi wametoa mapendekezo ya Kamati za BMU zijengewe uwezo na zisimamie hasa majukumu yao.

Alisema mwingiliano wa wavuvi na wakulima wa mwani yakitokea wakibishana na kugombana mwisho wa siku wanaumizani na mwisho wa wiku sio jambo nzuri kwa Taifa na Kamati ngazi ya kata wapo tayari kushirikiana na vyombo vya ulinzi kuweza ktoa taarifa za kina kuhusu hali hiyo chanzo ni nini na wanaamini wakishirikiana kwa pamaoja na kuwa agenda yao kubwa kwenye vikao vyao na hivyo kuweza kupiga vita vitendo hivyo.

Hata hivyo alisema kwa upande wake Mratibu wa Uwashemu Salehe Sokoro alisema kwamba anaamini changamoto ambazo zimeelezwa katika mdahalo huo zimechukuliwa na zitakwenda kufanyiwa kazi ili kukomesha vitendo vya namna hiyo kwenye maeneo husika
Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu-ADEM umepanga kufanya mbio maalumu za marathon zitakazohusisha wadau mbalimbali wa elimu, mashirika na taasisi yanayojihusisha na usimamizi wa elimu, wanachuo wa vyuo mbalimbali katika Mkoa wa Pwani na wananchi wote zikilenga kuhamasisha umoja, amani na utulivu katika Taasisi za kielimu pamoja na kuchangisha fedha kwa ajili ya kuboresha miundo mbinu katika Chuo cha ADEM kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani.

Pichani: Washambuliaji wa Timu ya EWURA (wenye jezi za bluu) wakishambulia timu pinzani wakati wa mchezo huo leo.

MOROGORO.

 Timu ya Mpira wa Wavu kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kung’ara katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMMUTA) baada ya kuichakaza timu ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa seti mbili mfululizo.

Katika mchezo huo uliochezwa leo mkoani Morogoro, EWURA ilipata pointi 25 katika seti zote mbili, huku NEMC ikijitahidi lakini ikibaki na pointi 23 kwenye seti ya kwanza na 17 katika seti ya pili.

Mchezo huo uliovuta hisia za mashabiki ulitawaliwa na kasi, nidhamu na uchezaji wa kimkakati kutoka kwa EWURA, ambao washambuliaji wao walionekana kuwa imara zaidi dhidi ya ngome ya NEMC.

Pichani: Washambuliaji wa Timu ya EWURA (wenye jezi za bluu) wakishambulia timu pinzani wakati wa mchezo huo leo.


 Na Mwandishi wetu- Dar es salaam


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amewahimiza Watu Wenye Ulemavu kuwa mabalozi wazuri wa kudumisha amani nchini.


Mhe. Nderiananga alieleza hayo wakati wa kikao chake na Wajumbe wa Bodi ya Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) kilichofanyika mwishoni mwa wiki  katika Ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu uliopo Magogoni jijini Dar es salaam.

Alisema kwamba, ili shughuli za kiuchumi ziweze kufanyika ni lazima iwepo amani kwani wananchi watakuwa na uhuru wa kufanya shughuli zao bila vurugu zozote hatua itakayochagiza ukuaji wa uchumi wao binafsi  hata taifa.

“Tunafahamu yanapotokea madhara watu wa kwanza kuathirika ni watu wenye ulemavu basi tunawashukuru kwa umoja wenu nasi tunawaahidi kuendelea kushirikiana,” alisema Mhe. Nderiananga.


Pia, aliongeza kwamba ipo haja ya Viongozi wa dini kukutana na wakundi ya watu wenye ulemavu kuendelea kuwajenga imani hatua itakayodumisha upendo na mshikamano kama  taifa.

Kwa upande wake Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi alisema, Ofisi hiyo imedhamiria kuwahudumia watu wenye ulemavu pamoja na kusikiliza kero zao ili kuzitafutia ufumbuzi.


“Ofisi ya Waziri Mkuu ni ya utekelezaji wa shughuli za serikali  hivyo niwakaribishe katika familia hii naamini tutaendelea kushirikiana na kuhakikisha kila mmoja wetu anafaidika na hadhi ya kuwa mtanzania bila kujali hali yake,”alieleza Dkt. Yonazi.

Naye Makamu Mwenyekiti  wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) Bi. Tungi Mwanjala  aliipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna inavyojali watu wenye ulemavu.

Aidha Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi Wasiiona (TASODEB) Bw. David Shaba ambaye pia ni mmoja wa wajumbe wa bodi hiyo  alishauri watu wenye ulemavu kutokubali kutumiwa na watu wenye nia ovu akisema mahali popote zinapotokea vurugu kundi hilo huathirika kwa kiasi kikubwa kutokana na kukosa msaada wa haraka.

“Niwaombe wenye ulemavu wenzangu tuwe makini sana tusishawishike hovyo, haya mambo ni ya hatari sana tuzingatie hali zetu hatuwezi kukabiliana na fujo vitakapotokea vita  sisi ndio tutaathirika sana zaidi ya hao wanaotuchochea tuwe na msimamo,” alieleza Mwenyekiti huyo.


MWISHOOO