Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera, akifungua Semina ya mafunzo kwa wadau wa usafirishaji (hawapo pichani), kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika kwa siku moja jijini Mbeya


Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Dkt Rashid Chuachua, Akimkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera, kufungua Semina ya mafunzo kwa wadau wa usafirishaji, kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika kwa siku moja jijini Mbeya


Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Mbeya, Mhandisi Peter Mkolwa akisoma taarifa yake kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera (hayupo pichani), kuhusu Semina ya Mafunzo ya Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika Jijini Mbeya.


Baadhi ya washiriki wa semina ya mafunzo ya Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 wakimsikiliza mgeni rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya (hayupo pichani), wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo yanayofanyika kwa siku moja jijini Mbeya.


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera, (aliyeketi katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa semina ya mafunzo kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 kwa wadau wa usafirishaji, inayofanyika kwa siku moja jijini Mbeya.


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera (aliyeketi katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Watoa Mada wa Semina ya Mafunzo kwa wadau wa usafirishaji kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 jijini Mbeya.


Mhandisi Joseph Rwihura, ambae ni Mhandisi Mkuu Matengenezo ya Mizani kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), akitoa elimu kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 kwa wadau wa usafirishaji jijini Mbeya.

PICHA NA WUU

..........................................................................................

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera, ameutaka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kuwajengea uwezo watendaji wa mizani zote nchini ili waweze kutoa huduma bora kwa wadau wa usafirishaji wanaotumia mizani hiyo.

Ameyasema hayo wakati akifungua semina ya mafunzo kwa wadau wa usafirishaji kuhusu Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika kwa siku moja katika ukumbi wa BEACO mkoani Mbeya.

“Elimu hii ya Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018, itolewe pia kwa watendaji wote wa TANROADS walio kwenye vituo vyote vya mizani nchini ili iwe rahisi kwao kuendelea kuwaelimisha wadau wa usafirishaji wanaotumia huduma za mizani nchini.

“Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, imetenga fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu bora ya barabara za mikoa, mijini na vijijini, hivyo ni jukumu la kila mtanzania kulinda na kusimamia matumizi bora na sahihi ya miundombinu ya barabara nchini kwa maendeleo ya taifa letu”, amesema Homera.

Mkuu wa Mkoa huyo ameongeza kuwa msukumo wa mafunzo hayo unatokana na ukweli kuwa, wadau wengi wa usafirishaji nchini hawana uelewa wa kutosha juu ya sheria hiyo ya Uzibiti Uzito wa Magari inayotumiwa na nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki, hali inayopelekea changamoto za mara kwa mara hasa inapotokea chombo cha usafiri kinapopimwa na mizani ya TANROADS na kukutwa kimezidisha uzito, hivyo elimu hiyo itasaidia kuondoa changamoto hizo.

Awali, akisoma taarifa yake kwa mgeni rasmi, Kaimu Meneja wa TANROADS mkoa wa Mbeya Mhandisi Peter Mkolwa, amesema kuwa mafunzo hayo ni muendelezo wa utoaji elimu ya Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 ambayo yamekuwa yakitolewa kwa wadau wa usafiri wa barabara nchini tangu mwaka 2018 kabla ya kuanza kutumika rasmi kwa sheria hiyo mwezi Machi mwaka 2019.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, mafunzo haya yanalenga kuongeza uelewa wa pamoja baina ya wasafirishaji nchini na Serikali ambayo ndiyo inasimamia sheria hii, na hivyo elimu hii itaendelea kutolewa kwa watumishi wote wa mizani ili kuwajengea uwezo wa kutoa huduma ya upimaji uzito wa magari kwa ufanisi sambamba na kuendelea kuwaelimisha wadau wa usafirishaji juu ya sheria hii wanapokuwa kwenye vituo vya mizani,” amesema Mhandisi Mkolwa.

Nao wadau wa usafirishaji jijiniwa Mbeya wanaohudhuria mafunzo hayo, wameitaka Serikali kutilia mkazo upatikanaji wa elimu hiyo, kwa kuandaa mabango na vipeperushi mbalimbali ambavyo vitawaongezea uelewa juu ya sheria hiyo ya Uzibiti uzito wa Magari inayotumiwa na nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwani kwa kufanya hivyo wataepukana na makosa wanayoyafanya mara kwa mara kwasababu ya kukosa uelewa.

Semina ya Mafunzo ya Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018 inayofanyika kwa siku moja jijini Mbeya, inashirikisha wadau wa usafirishaji kutoka jiji la Mbeya pamoja na mkoa jirani wa Songwe.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: