Na Mwamvua Mwinyi, Pwani

JESHI la polisi kitengo cha Usalama Barabarani kwa kushirikiana na kamati ya usalama barabarani mkoa wa Pwani,limetoa elimu kwa kundi la wanafunzi namna ya kutumia vivuko,maeneo ya pundamilia kuvuka kwa usalama wao na kujiepusha na ajali.

Aidha wananchi pamoja na madereva wameaswa kuacha tabia ya kutumia simu katika maeneo ya vivuko ili kuweka umakini kwenye maeneo ambayo ni hatarishi.

Akitoa elimu kwa wanafunzi wa shule ya msingi Mkoani na Kambarage wilayani Kibaha, juu ya umuhimu wa vivuko ili kuvuka kwa usalama ,katika barabara kuu ya Morogoro-Dar es salaam, mkuu wa kitengo cha Usalama Barabarani mkoa wa Pwani,Edson Mwakihaba alisema, zoezi hilo ni endelevu.

Alieleza wameshaanza kutoa elimu ya Usalama Barabarani kwa makundi mbalimbali madereva ,wa Bajaj na pikipiki, wananchi na sasa kundi la wanafunzi.

Hata hivyo Mwakihaba alisema,wapo kwenye maandalizi ya wiki nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Pwani na wanatarajia kuendelea kutoa elimu mbalimbali ili kupunguza ajali za barabarani Mkoani humo.

Akielezea kuhusiana na ukaguzi wa stika aliwataka madereva kujitokeza kupeleka vyombo vyao vya moto katika vituo vya polisi na vituo vya ukaguzi ili kununua stika kwa kufuata bei elekezi na kukaguliwa gari kama ni zima ndipo liingie barabarani.

"Magari yatakaguliwa na kama gari halina sifa halitoruhusiwa kuingia barabarani"Natoa wito madereva wote mfuate sheria za usalama barabarani na kupeleka magari yakakaguliwe"alisisitiza Mwakihaba.

Nae mwenyekiti wa kamati ya usalama barabarani mkoa wa Pwani, Josephine Protas alitoa wito madereva wafuate sheria za usalama barabarani na kufuata michoro ili kuepusha ajali zembe.

Alikemea matumizi ya earphone na simu wakati wa kuvuka kwenye vivuko ili kuweka umakini wakati wa kuvuka.

Protas aliwataka wananchi kushirikiana na kitengo cha Usalama Barabarani kufichua madereva hasa wa magari makubwa ya abiria wanaoendesha kwa mwendo kasi ili wachukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kulipia faini.

Kwa upande wake,mwanafunzi wa darasa la tano shule ya msingi Kambarage,Elia Alex alieleza,mafunzo waliyoyapata watakwenda kuwa mabalozi wa jeshi la polisi kupitia kitengo cha Usalama Barabarani.

Alifafanua awali walishuhudia ajali zinazotokea kwenye matuta na vivuko vya pundamilia licha ya kuwa maeneo yaliyochorwa kisheria kujilinda na ajali.

Elia alisema sasa wamejifunza kuwa makini na kuwakemea madereva wasiofuata sheria za usalama barabarani wakiwemo madereva pikipiki.



Share To:

Post A Comment: