Na Raisa Said

Mbunge wa jimbo la Korogwe vijijini Timotheo Mzava ameihoji serikali sababu za kushindwa kulimega shamba la mkonge la Mwakinyumbi Estate kwa ajili ya kuwgawia wananchi kufanyia shughuli za kilimo.

Mbunge Mzava alitoa kauli hiyo,wakati akiuliza maswali mawili madogo ya nyongeza akimtaka waziri wa ardhi kuandamana naye hadi kwenye shamba hilo kumaliza kilio cha wananchi wa Korogwe

Mzava amesema wilaya ya Korogwe imezungukwa na mashamba ya Mkonge na Chai na kwamba kwa sasa wananchi hawana maeneo ya kilimo wakati kwenye mashamba hayo maeneo makubwa yameshindwa kuendelezwa.

Mbunge huyo aliitaka serikali kukaa na wawekezaji wa mashamba hayo ili wakubaliane namna wanavyoweza kuipata ardhi ya maeneo ya mashamba hayo ,kumaliza kilio cha vijana ambao ndio wahanga wakubwa wanaokosa maeneo ya kufanyia shughuli zao za kuichumi.

Akijibu maswali hayo Waziri wa Ardhi nyumba na Maendeleo ya Makazi Willium Lukuvi alikiri kilio cha Mbunge huyo kuwa cha muda mrefu huku akiahidi kufikia kwenye utatuzi wa kero hiyo mara tu baada ya kumalizika vikao vya Bunge.

Waziri Lukuvi amesema uchunguzi wa ndani uliofanywa umebaini kuwa shamba hilo limetelekezwa na hakuna uendelezaji wowote uliofanyika huku likidaiwa pango la ardhi kiasi cha shilingi milioni 174 hadi sasa kodi na malimbikizo kwa muda wa miaka 17 kuanzia mwaka 2005 hadi mwaka huu wa 2021.

Kutokana na hali hiyo serikali ilianza kubadilisha miliki ya shamba husika kwa kutuma ilani ya ubadilisho kwa mmiliki ndani ya siku tisini na mmiliki hakuweza kujibu chochote dhidi ya ilani hiyo.

Lukuvi amesema baada ya kufikia hatua hiyo serikali kwasasa inaendelea na hatua yaubadilisho akitaja hatua hiyo kuwa ni pamoja na kuandika barua kwa Mh. Rais ambaye ndiye kisheria mwenye nguvu ya kufuta umiliki wa shamba hilo.

Hata hivyo lukuvi amesema ufutaji wa hati za mashamba yasiyoendelezwa na zoezi endelevu kwa mujibu wa sheria likiwa na lengo la kulinda maslahi ya Taifa wananchi na wawekezaji.
Share To:

Post A Comment: