Mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa Umefikia asilimia 7.7


Lengo la Serikali ni kuifanya Tanzania kuwa Kitovu cha Madini Afrika


Katika miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara mchango wa Sekta ya Madini katika Pato la Taifa umeongezeka hadi kufikia asilimia 7.7 kutoka asilimia 3.4 Mwaka 2014 kitu ambacho kinaonesha dhahiri kwamba ifikapo mwaka 2025 mchango wa Sekta ya Madini katika Pato la Taifa utafikia asilimia 10.


Hayo yamebainishwa leo Novemba 5, 2021 na Waziri wa Madini Doto Biteko wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari akielezea Mafanikio na Maendeleo ya Sekta ya Madini kabla na baada ya Uhuru kuelekea Maadhimisho ya Miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo jijini Dodoma.


Waziri Biteko amesema, mapinduzi makubwa yamefanyika tangu uhuru mpaka sasa ambapo Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha watanzania wananufaika na rasilimali madini huku wakishuhudia ongezeko la ukuaji katika Sekta ya Madini.


“Mwaka 2009 Serikali ilitunga upya Sera ya Taifa ya Madini na kufuatiwa na Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, baada ya kuonekana kuwepo kwa changamoto kadhaa, Serikali ilifanya mapitio ya Sheria ya Madini 2010 kwa lengo la kuimarisha uwezo wa Serikali kuisimamia Sekta ili iweze kuongeza mchango wake katika Pato la Taifa, na pia kwa lengo la kuimarisha ushiriki wa wananchi kwenye shughuli za madini, kuinua sekta ndogo ya uchakataji madini na vilevile kwa lengo la kufungamanisha Sekta ya Madini na Sekta nyingine za uchumi kwa maendeleo ya Taifa,” amesema Waziri Biteko.


Waziri Biteko amesema, Mwaka 2017 yalifanyika marekebisho makubwa katika Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 kupitia Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali Namba 7 ya Mwaka 2017. Pamoja na malengo mengine ya marekebisho hayo kuliwekwa masharti yatakayowezesha wananchi na Taifa kunufaika zaidi na maliasili ya madini kupitia dhana ya “Permanent Sovereignty over Natural Resources”.


 Waziri Biteko amesema, Mabadiliko hayo pia yalilenga kutambua haki ya ushiriki wa Serikali (Government participation) katika shughuli zote za uchimbaji, uchakataji na uchenjuaji wa madini na umiliki wa hisa kwa asilimia 16 (16% non dilutable free carried interest) katika makampuni ya uchimbaji na Serikali kuwa na uwezo wa kuongeza umiliki mpaka kufikia asilimia 50 kupitia thamani ya vivutio vya uwekezaji na kikodi alivyopewa mwekezaji. 


“Miaka iliyopita kabla ya kufanyika kwa mabadiliko ya Sheria ya Madini Mwaka 2017, ushiriki wa watanzania katika uchumi wa madini umeongezeka, mathalan, katika kipindi cha Mwaka 2020/2021 jumla ya kampuni za watoa huduma kwenye migodi 961 sawa na asilimia 66 zilikuwa ni za kitanzania na idadi ya kampuni za kigeni zilikuwa 506 sawa na asilimia 34,” amesema Waziri Biteko.


Waziri Biteko amesema yapo mafanikio mengi ambayo kama Taifa linajivunia kupitia Sekta ya Madini ikiwemo; kupandisha uchumi wa Taifa, kuongeza ufanisi wa sekta kupitia marekebisho ya Sheria, kuanzishwa kwa masoko ya madini, kuongeza uwazi na ushiriki wa watanzania katika Sekta ya Madini.


Ndani ya kipindi cha miaka 60 ya Uhuru Serikali ilisaini Mikataba ya Ubia na Kampuni ya LZ Nickel ya nchini Uingereza na kuanzisha Kampuni ya Tembo Nickel Corporation Limited yenye Kampuni tanzu mbili ambazo ni Kampuni ya Uchimbaji wa Madini ya Tembo Nickel Mining Company Ltd na Kampuni ya Usafishaji wa Madini ya Tembo Nickel Refinery Company Ltd. 


“Lengo letu kama Serikali kupitia Wizara hii ya Madini ni kuifanya Tanzania kuwa Kitovu cha Madini Afrika na hatimaye duniani. Uwezo na sababu hizo tunazo kutokana na wingi wa rasilimali madini tulizonazo ikiwemo usimamizi madhubuti wa sekta ambao unaongozwa na Sheria zetu,” amesema Waziri Biteko.

Share To:

Post A Comment: