Na John Walter-Manyara
MAMLAKA
ya Mapato Tanzania(TRA) imetolea ufafanuzi masuala mbalimbali yahusuyo
kodi hiyo ya majengo ikiwamo mkanganyiko kuhusu ulipaji wa kodi hiyo
kwenye nyumba zenye hadhi tofauti, nyumba zilizoezekwa kwa nyasi
hazihusiki kwenye tozo hiyo.
TRA wametoa ufafanuzi kwenye mjadala
na wafanyabiashara katika mji wa Babati kuhusu ulipaji kodi ya majengo
kwa njia ya ‘luku’ ya umeme uliofanyika katika ukumbi wa River Nile
mjini Babati.
Afisa Elimu na huduma kwa mlipakodi kutoka TRA
makao makuu Lazaro Mafie, alisema utaratibu wa kulipia kodi ya majengo
kwa njia ya mfumo wa luku umeanza Agosti 20,2021 na utakuwa ukitekelezwa
kwa njia hiyo ukimhusu mwenye nyumba na sio mpangaji.
Amesema
tozo hiyo inatozwa mara moja katika mwezi kwa maana mteja akishalipa
hata umeme unapoisha katikati, hatakatwa tena hadi mwezi mwingine.
Kwa
makato hayo inamaanisha kwamba kwa kipindi cha mwaka mmoja mlipaji
atakuwa anatozwa Sh 12,000 ambayo ndiyo kodi ya jengo kwa nyumba za
kawaida.
Aidha Mafie amesema Kodi hiyo haihusu nyumba za vijijini, nyumba za nyasi na udongo na zile zilizojengwa kwa vifaa visivyodumu.
Amesema
jengo la ghorofa lililo kwenye mji, manispaa na jiji, kila sakafu
inatozwa kwa mwezi kwenye luku Sh 5,000 ili ndani ya mwaka mlipaji awe
amelipa Sh 60,000 ambayo ndicho kiwango cha kodi kwa nyumba ya mtindo
huo.
Aidha nyumba ya ghorofa zilizopo wilayani, halmashauri na
mikoani zitalipa Sh 12,000 kama nyumba za kawaida bila kuja idadi ya
sakafu zilizopo katika jengo hilo la ghorofa.
Alisema wastaafu,
wazee wenye umri kuanzia miaka 60 na kuendelea wako kwenye kundi la
msamaha na wataendelea kupata msamaha huo wa kodi ya majengo kwenye
nyumba za makazi wanayoishi wenyewe.
Alisema utaratibu wa kupata
msamaha bado unaendelea na ni wa mtu yeyote aliyekidhi vigezo vya
msamaha wa kodi ya majengo kwa mujibu wa sheria,nyumba za ibada na
nyumba za serikali.
Aidha amewataka wateja waliokatwa kimakosa
kwenye luku watoe taarifa ofisi za TRA akiwa na nyaraka na kiasi
kilichokatwa kitaingizwa kwenye umeme wa luku yake.
Kwa upande wa
nyumba zisizo na umeme ambazo zipo kwenye kundi la kulipa kodi,
zinapaswa kulipa na mmiliki ana wajibu wa kufuata ankara ya malipo TRA.
Kuhusu
nyumba moja yenye mita zaidi ya moja, Mafie alieleza kuwa kodi hiyo
italipiwa kupitia luku moja na ikiwa mteja ametozwa kwenye mita zaidi ya
moja atapaswa kuwasilisha taarifa TRA ili makato yaelekezwe kwenye
moja.
Kuhusu kiwanja kimoja kuwa na nyumba zaidi ya moja, alisema kila nyumba inapaswa kulipiwa kodi ya jengo.
Kaimu
Meneja wa TRA mkoa wa Manyara amesema wataendelea kuwaelimisha wateja
wao kuhusu sheria hiyo huku akiwahimiza kulipa kodi zao kwa wakati na
kwa usahihi pamoja na kutumia mashine za kielektroniki wakati wote kama
sheria inavyowataka.
Mfanyabiashara kutoka mjini Babati Isack
Mushi (POLEPOLE) ameunga mkono utaratibu huo wa Serikali na kushauri
elimu Zaidi iendelee kutolewa kwa wananchi.
Hivi karibuni Shirika
la Umeme Tanzania (Tanesco) lilielekeza wanaotaka kununua umeme kuanzia
mwezi Agosti wahakikishe wananunua wa zaidi ya Sh 2,000 waweze kulipa
kodi ya majengo ambayo imeanza kukatwa kupitia mfumo wa luku za umeme.
Home
Unlabelled
Tozo ya Majengo kupitia Luku yapokelewa Manyara
Post A Comment: