Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Bakari Msulwa (katikati) akizungumza  na Wafanyabiasha wa mkoa huo jana wakati akifungua mafunzo ya  siku mbili ya kutoa elimu kwa wakazi wa mkoa huo kuhusu huduma zinazotolewa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA)


Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Bakari Msulwa (katikati) akisisitiza wakati akifungua mafunzo hayo.  


 Wakazi wa Mkoa wa Morogoro wakiwa kwenye mafunzo hayo.



Na Mwandishi Wetu, Morogoro


MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Bakari Msulwa ametoa wito kwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) kuweka mkakati wa kuwafikia wagunduzi na wabunifu mbalimbali katika maeneo yao ili kuweza kuwapa elimu ya Usajili.

Msulwa aliyasema hayo jana wakati akifungua zoezi la siku mbili la kutoa elimu kwa Wakazi wa Mkoa huo kuhusu huduma zinazotolewa na BRELA katika Ukumbi wa Midland Inn Hotel, Morogoro.

Alisema kwamba kuna Watanzania wengi wanafanya juhudi mbalimbali za kugundua vitu vipya ni vyema kukawa na mpango wa kuwafikia hao na kuwasaidia  katika masuala ya kulinda kazi zao.

Katika hatua nyingine Wafanyabiashara wa Mkoa wa Morogoro wameishukuru BRELA kwa kutoa elimu katika Mkoa wao ambayo imewapa mwanga na dira mpya katika urasimishaji wa biashara zao.

Paulina Mbawala ambaye ni Mfanyabiashara mkoani Morogoro amesema kwamba kabla ya mafunzo kuna vitu vingi walikua hawajui na hivyo kupata Ugumu katika urasimishaji wa biashara zao.

“Kabla ya mafunzo haya hatua za usajili wa Kiwanda tuliziona ni ngumu, lakini kupitia elimu tuliyopata hapa tumefahamu ni namna gani tunaweza kusajili Kiwanda kikubwa, cha kati au kidogo na jinsi ya kukuza biashara kutoka hatua moja kwenda nyingine kwa manufaa yetu Wajasiriamali na Taifa kwa ujumla”alisema Mbawala.

Mfanyabiashara Novatus John, aliyeshiriki mafunzo hayo kwa siku ya kwanza, amebainisha kwamba kupitia elimu hii sasa wamefahamu ni kwa jinsi gani wanaweza kuingia katika fursa nyingine ilikuweza kukuza biashara zao zaidi.

“Kupitia elimu hii tumeweza kufahamu namna ya kupata masoko, kuzitambulisha bidhaa zetu sokoni lakini pia kupitia Dirisha la Taifa la biashara (the Tanzania National Business Portal) tumejifunza kuwa Mfanyabiashara anaweza kufahamu taratibu za usafirishaji nje ya nchi, uingizaji nchini na upitishaji wa mazao na bidhaa mbalimbali nchini.”  alisema John.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ufunguzi wa mafunzo hayo,  Afisa Leseni Mwandamizi kutoka BRELA, Abbas Cothema alisema, katika sehemu walizopita wakitoa mafunzo wamegundua wafanyabishara wengi wamekua wakitumia majina ya biashara kabla ya kuyasajili na badae yanaleta shida katika usajili.

“Mpaka sasa tumetoa elimu kwa Wafanyabiashara wa Mkoa wa Singida, Dodoma na sasa tupo hapa Morogoro changamoto inayojirudia ni kufanya biashara bila kurasimisha. Mfanyabiashara anaanzisha biashara leo anakuja kusajili miaka mitano badae, kwa wakati huo kama alikua anatumia jina la biashara mathalani lisiposajiliwa itamlazimu kubadili jina na kuanza kujitangaza upya”. alisema Cothema.


Share To:

Post A Comment: