Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) ametoa onyo kwa Meneja wa Wakala wa MajiSafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Chato Mhandisi Andrew Kilembe kwa kushindwa kutatua kwa wakati kero ya ubovu wa mita za maji zilizowekwa katika mradi wa maji wa Imalabupina Inchwankima na kusababisha wananchi wa eneo hilo kukosa maji kwa siku kadhaa.

Ametoa onyo hilo baada ya kupokea malalamiko toka kwa wananchi wakati akikagua mradi huo unahohudumia wakazi wa vijiji hivyo.

Amesema wananchi wanakosa huduma ya maji kwa sababu ya viongozi kufanya kazi kwa mazoea na kushindwa kutatua kero zinazojitokeza kwa wakati.

“Natoa onyo na naomba fuatilieni hilo tatizo linalosababisha wananchi wasipate maji kwa wakati maeneo mengine yanatoa maji, na hakikisheni hizo mita zinazosumbua zinabadilishwa haraka ili kuondoa kero hiyo na wananchi hawa wapate maji”, amesema Mhandisi Mahundi na kusisitiza kezo zote ikiwemo matatizo ya umeme yasisubiri viongozi.

Aidha, amempongeza Meneja huyo wa RUWASA Chato kwa kuamua kutumia shilingi milioni 311 kukarabati miundombinu ya mradi wa maji Kasenga ambao ulichakaa na kuacha kutoa maji kwa muda mrefu.

Katika ziara yake ya kukagua miradi ya maji mkoani Geita Naibu Waziri alikagua pia mradi wa maji wa Katoro Buseresere ambao utekelezaji wake unaendele vizuri na mradi huo ukikamilika utahudumia wananchi 20,000 wa kata ya Buseresere, Katoro, Ludete na Nyamigota
Share To:

Post A Comment: