Na Tito Mselem, Dodoma


Imeelezwa kuwa, ukuaji wa Sekta ya Madini nchini umeendelea kuimarika mwaka hadi mwaka na hivyo kupelekea kuongezeka kwa mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa.


Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Madini, Prof. Shukrani Manya alipofanya kikao na baadhi ya watumishiwa Tume ya Madini katika Ukumbi wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) uliopo jijini Dodoma.


Akizungumza kwenye kikao hicho, Prof. Manya amesema, kwa mwaka 2017 mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa ulikuwa asilimia 4.4 na uliendelea kuongezeka ambapo kufikia mwaka 2019 ulifikia asilimia 5.2.


“katika kudhibiti biashara haramu ya madini nchini Serikali imerahisisha biashara ya madini kwa wachimbaji wadogo pamoja na wafanyabiashara wa madini nchini kwa kuanzisha masoko 41 ya madini pamoja na vituo vya ununuzi wa madini vipatavyo 41,” alisema Prof. Manya.


Prof. Manya amesema, uwepo wa masoko hayo umesaidia kupunguza matukio ya utoroshaji wa madini nchini ikiwa ni pamoja na kuimalisha makusanyo ya maduhuli yatokanayo na rasilimali madini.


Aidha, Prof. Manya amemtaka Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madin,i Mhandisi Yahaya Samamba kuhakisha fedha nyingi inaelekezwa kwenye maeneo yanayotoa matokeo mazuri kwenye ukusanyaji wa maduhuli ya serikali pamoja na maeneo yanayosimamiwa vizuri shughuli za uzalishaji madini.


Naye, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof. Idris Kikula, amempongeza Prof. Manya kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Madini ambapo amesema ni jambo la kushukuru kuteuliwa mtu kutoka miongoni mwa watendaji wa Tume hii inaonesha nijinsi gani kazi nzuri ifanyika.


Pia, Prof. Kikula, ameahidi kwamba, Tume ya Madini itaendelea kusimamia kwa uweledi utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo ili kuhakikisha kuwa sekta ya Madini inaendelea kuwa na manufaa katika uchumi na maendeleo ya nchi kwa ujumla.


Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, amewasisiza watumishi wote kuhakikisha kila mmoja kwa nafasi yake anachapa kazi na kueleza hatomuangusha Prof. Manya kwani atahakikisha shughuli zote zinazofanya na Tume ya Madini zinafanyika tena kwa ufanisi mkubwa.

Share To:

Post A Comment: