Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, akitoa maelekezo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Tanzanite, jijini Dar es Salaam.

Mhandisi wa Madaraja Lulu Dunia, akifafanua jambo kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa,wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Tanzanite, jijini Dar es Salaam.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, akikagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Tanzanite, jijini Dar es Salaam
Kazi za ujenzi wa Daraja la Tanzanite unaohusisha daraja lenye urefu wa KM 1.03 pamoja na barabara za maingilio zenye urefu wa KM 5.02 zikiendelea jijini Dar es Salaam.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, ameitaka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kupitia Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) kutengeneza kanzi data ya wataalamu wake walioshiriki ujenzi wa madaraja yote makubwa nchini.

Hatua hiyo itawezesha kuwashirikikisha mara kwa mara watalaamu hao ili kupata ujuzi na uzoefu wa kutosha wa kazi hizo hivyo kuliwezesha Taifa kuwa na hazina ya wataalamu wa ujenzi wa madaraja makubwa watakao simamia ukarabati wake pamoja na kujenga mapya siku za usoni.

Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa Daraja la Tanzanite Waziri Mkuu amepongeza hatua iliyofikiwa na kuwataka kuongeza kasi ya ujenzi ili daraja hilo likamilike kwa wakati.

“Kazi yenu ni nzuri hakikisheni daraja hili linakamilika kwa wakati, ili watanzania waweze kunufaika na hivyo kuongeza fursa za utalii hapa nchini”, amesema Waziri Mkuu Majaliwa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa ameutaka uongozi wa Manispaa ya Jiji la Dar es salaam kuhakikisha sehemu barabara iliyobaki yenye urefu wa  kilometa tatu (3) nje ya mradi huo inajengwa kwa kiwango cha  lami ili kurahisisha usafiri katika ukanda huo wa fukwe ya Bahari ya Hindi.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, amemhakikishia Waziri Mkuu Majaliwa kuwa mradi wa ujenzi wa Daraja la Tanzanite utakamilika kwa wakati.

Ameongeza kuwa ujenzi wa daraja hilo umetoa fursa za ajira za moja kwa moja kwa watanzania zaidi ya 500 na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi.

Mradi wa ujenzi wa Daraja la Tanzanite unahusisha daraja lenye urefu wa KM 1.03 pamoja na barabara za maingilio zenye urefu wa KM 5.02 unatarajiwa kukamilika mwezi Disemba mwakani.

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: