Na Emmanuel Mbatilo



Shirika la Viwango Tanzania TBS, limetoa vyeti na leseni 177 kwa Wazalishaji wa bidhaa na wajasiriamali wadogo ambao bidhaa zao zimethibitishwa ubora baada ya kukidhi matakwa ya viwangokwa kipindi cha mwezi Julai hadi Septemba 2020.


Akizungumza katika hafla hiyo Mkurugenzi Mkuu TBS, Dkt.Athuman Ngenya amesema vyeti na leseni 177 zilizotolewa kati ya hizo,  leseni 1 ni ya mfumo wa usimamizi ubora na leseni, 146 za alama ya ubora na 30 ni vyeti kwa bidhaa zisizo na viwango vya Tanzania.


“Kati ya leseni na vyeti vilivyotolewa, 88 ni vya wajasiriamali wadogo. Vyeti na leseni hizo ni za bidhaa za vyakula, vipodozi, vifaa vya ujenzi, vilainishi, vitakasa mikono, vifaa vya umeme, vifaa vya makenika, magodoro, vibebeo pamoja na vifungashio”. Amesema Dkt.Ngenya.


Aidha, Dkt.Ngenya amesema kuwa majengo ya kuzalisha, kuhifadhi au kuuzia chakula na vipodozi pamoja na vyombo vinavyobeba bidhaa hizo (Mfano: magari ya kubebea vyakula) ni lazima visajiliwe na TBS ndipo viruhusiwe kutumika.


“Kwa kipindi cha kuanzia mwezi Julai mpaka Septemba mwaka huu tumekwisha sajili majengo 2139 ya biashara na ya kuhifadhia bidhaa za vyakula na vipodozi. Pia kwa kipindi hicho tumeweza kusajili jumla ya bidhaa 533 za vyakula na vipodozi”. Amesema Dkt.Ngenya.


Pamoja na hayo Dkt.Ngenya amewaasa wadau hao wa viwango kuendelea kuzalisha bidhaa zinazokidhi matakwa ya viwango kwa mustakabali wa afya na mazingira ya watumiaji kwa ujumla.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: