Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama (kulia) akieleza jambo alipokuwa akikagua kitalu nyumba kilichopo Nangara, Mjini Babati. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Babati Bi. Elizabeth Kitundu. 
Baadhi ya vijana wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipowatembelea vijana hao kukagua maendeleo ya mafunzo waliyopatiwa kupitia kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia ya kitalu nyumba.

Mkuu wa Wilaya ya Babati, Bi. Elizabeth Kitundu (kushoto) akieleza jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (wa tatu kutoka kushoto) alipofanya ziara mkoani humo kukagua mafunzo waliyopatiwa vijana kupitia kilimo ha kisasa.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (katikati) akitoa maelekezo kwa viongozi wa Mkoa wa Manyara alipokuwa akikagua maendeleo ya mafunzo ya kilimo cha kisasa kupitia teknolojia ya kitalu nyumba, Mkoani Manyara.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (wa pili kutoka kushoto) akiangalia bustani iliyotengenezwa na vijana alipokuwa akikagua mafunzo ya kilimo cha kisasa wanayopatiwa vijana hao. Kushoto ni Mbunge  wa Babati Vijijini Mhe. Virajilal Jituson.


Afisa Kilimo, Bi. Mary Temu (wa tatu kutoka kushoto) akitoa maelezo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama namna wanavyohifadhi mbolea katika madumu kabla ya kuwekwa kwenye kitalu nyumba “Greenhouse”.


Mbunge Mstaafu wa Babati Vijijini Mhe. Virajilal Jituson akieleza jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama alipofanya ziara katika Mkoa huo kukagua maendeleo ya mafunzo ya kilimo cha kisasa yanayotolewa kwa vijana kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu.


Muonekano wa Kitalu Nyumba “Greenhouse” iliyopo Matufa katika Kata ya Magugu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama (kushoto) akizungumza na viongozi wa mkoa wa Manyara alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mafunzo ya kilimo cha kisasa wanayopatiwa vijana kupitia teknolojia ya kitalu nyumba “Greenhouse”, Mkoani Manyara.


Na; Mwandishi Wetu – Manyara

Vijana walionufaika na mafunzo ya Kilimo cha Kisasa kupitia teknolojia ya Kitalu Nyumba “Greenhouse” wamehimizwa kutumia ujuzi huo ili waweze kujikwamua kiuchumi kwa kujiajiri na kuajiri wenzao.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama alipokuwa akikagua maendeleo ya Mafunzo ya kilimo cha kisasa yanayotolewa kwa vijana kupitia teknolojia ya kitalu nyumba, Mkoani Manyara.

Alieleza kuwa Serikali katika kuwezesha vijana nchini ilianzisha Programu maalum ya kukuza ujuzi ambayo inalenga kuimarisha nguvukazi kupata ujuzi unaotakiwa katika soko la ajira, vilevile kuwasaidia vijana waondokane na changamoto ya ajira kwa kujiajiri na kuajiri wenzao kupitia ujuzi waliopatiwa.

“Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imetoa ujuzi huu wa mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa teknolojia ya kitalu nyumba katika Halmashauri 84 za mikoa 12 ikiwemo mkoa wa Manyara ambao vijana wake pia wameweza kunufaika na mafunzo hayo,” alisema Mhagama

“Hakika tumeshuhudia namna Serikali ya Awamu ya Tano ambavyo imekuwa mstari wa mbele katika kushughulikia masuala mbalimbali ya vijana ikiwemo kuwapatia mafunzo ya ufundi stadi yaliyowawezesha kujiajiri na kuajiri wenzao tofauti na hapo awali,” alieleza Mhagama

Alieleza kuwa, Tangu serikali ya awamu ya tano iingie madarakani mafanikio mbalimbali yamepatika katika eneo la ajira na ukuzaji ujuzi. Jitihada hizo zimejidhihirisha katika sekta za kipaumbele kama vile Viwanda, Kilimo, Madini, Utalii pamoja na miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali.

“Natumaini wote mlimsikiliza Mhe. Rais wakati akihutubia na kufunga Bunge la 11 alielezea juu ya namna serikali katika kipindi cha miaka mitano imeendelea na jitihada za kukuza ajira ambapo jumla ya ajira 6,032,299 zimezalishwa,” alieleza Mhagama

Aliongeza kuwa, ujuzi huo waliopatiwa vijana kwa ufadhili wa serikali yao imekuwa ni fursa iliyowawezesha kujiajiri katika sekta ya kilimo ambacho ni bora na wanauhakika wa mazao wanayopata ni endelevu na kipato wanachopata kinafaida.

Aidha, Waziri Mhagama alitoa maagizo kwa viongozi wa mkoa huo kuhakikisha wanasimamia vizuri mradi huo na pia kuwajengea vijana ujuzi wa masoko ili watambue mbinu za uuzaji na kutafuta soko la kupeleka bidhaa watakazokuwa wakizalisha kulingana na mahitaji ya wanunuzi.

“Hapa manyara mnahoteli nyingi za kitalii ambazo mkiweza kuwaunganisha vijana, wataweza kupeleka bidhaa mbalimbali watakazokuwa wakizalisha kwenye kitalu nyumba ambapo mtakuwa mmewakomboa vijana kwa hatua kubwa sana,” alisema Mhagama.

Sambamba na hayo aliwahimiza vijana wa mkoa huo kuchangamkia fursa ya mikopo inayotolewa na halmashauri ili waweze kujenga vitalu nyumba vyao binafsi ambavyo vitawawezesha waajiri vijana wenzao.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Bw. Said Mabie alieleza kuwa halmashauri zote za mkoa wa manyara zimepata fursa ya kujengewa vitalu nyumba na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu ambapo jumla ya vijana 602 wameweza kunufaika na mafunzo hayo ya kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia kitalu nyumba.

“Mafunzo hayo ya Kilimo cha Kisasa kwa kutumia teknolojia ya Kitalu Nyumba yamewapa vijana hamasa, hivyo uongozi wa mkoa umekuwa pia ukishirikiana na wadau kama TAHA ambapo hadi sasa vitalu nyumba 22 vimeweza kujengwa na wakulima binafsi na kwenye shule kutokana na kupata hamasa ya kilimo cha aina hiyo,” alieleza Mabie

Naye Mwakilishi wa Vijana walionufaika na Mafunzo hayo, Bw. Paulo Mwaluko aliishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo hayo ambayo yamewapa hamasa vijana wengi wa mkoa huo kutambua manufaa yaliyopo kwenye kilimo na wameahidi kuendeleza ujuzi huo katika mkoa huo ili bidhaa watakazokuwa wakizalisha ziwasaidie kuwakomboa kiuchumi.
Share To:

Post A Comment: