Na Munir Shemweta, WANMM KILIMANJARO
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amelipongeza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kuweza kukamilisha ujenzi wa miradi ya jengo la ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Hai lililopo Bomang’ombe na ofisi pamoja na nyumba za Watumishi wa Wakala wa huduma za Misitu (TFS ) zilizopo kwenye shamba la Miti la Kilimanjaro Kaskazini maarufu Rongai wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro.
Dkt Mabula alitoa pongezi hizo jana alipotembelea miradi ya ujenzi wa majengo ya ofisi na nyumba hizo akiwa katika ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa pamoja na kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi kwenye mkoa wa Kilimanjaro.
Alisema, Shirika la Nyumba la Taifa kwa sasa linapaswa kupongezwa kutokana na juhudi kubwa inayofanya katika kutekeleza miradi yake ya ujenzi wa majengo ya ofisi na nyumba katika maeneo  mbalimbali nchini ikiwemo ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Hai na zile za Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) ambapo alieleza kuwa ofisi hizo zimejemgwa katika viwango vinavyotakiwa.
Naibu Waziri Mabula alisema, hivi sasa NHC imeaminiwa na Serikali kwa kupatiwa miradi mbalimbali ya ujenzi ikiwemo ujenzi wa majengo ya ofisi na nyumba za Wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) nchi nzima sambamba na ujenzi wa hospitali za Rufaa za mikoa ya Mara na Mtwara.

‘’Tunapaswa kumshukuru Mhe Rais John Pombe Magufuli kwa kuamua kutoa fedha za ujenzi wa majengo ya ofisi na nyumba za Wakala wa huduma za Misitu kwenye mikoa mbalimbali, Raisi anataka watumishi wafanye kazi katika mazingira mazuri’’ alisema Dkt Mabula.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri, Shirika hilo la Nyumba la Taifa kwa sasa imeaminiwa na serikali hivyo linapaswa kuhakikisha miradi yote inayokabidhiwa inakamilika kwa wakati sambamba na ujenzi wake kukidhi viwango na ubora unaotakiwa ili kujenga imani kwa wananchi na serikali kwa ujumla.
Akielezea utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa jengo la Ofisi na nyumba za watumishi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Kilimanjaro Juma Kiaramba alisema mradi huo ambao mpaka sasa umetumia TZSh 639,494,580.18 ulianza Septemba mwaka jana na tayari kazi za ndani kwa majengo yote 4 umekamilika kwa asilimia mia moja na kusisitiza kuwa Shirika lake linatarajia kukamilisha zilizobaki za nje katika kipindi cha muda mfupi ujao.
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Shamba la Miti la Kilimanjaro Kaskazini Joel Naasi  alimueleza Naibu Waziri Mabula kuwa TFS kupitia shamba la Miti la Kilimanjaro Kaskazini Wakala umefanikiwa kukusanya maduhuli kiasi cha fedha 3,688,849,489.68 hadi kufikia Mei mwaka huu wa fedha.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amezitaka ofisi za halmashauri na wilaya nchini kuzitumia ofisi za ardhi za mikoa zilizoanzishwa hivi karibuni katika kushughulikia masuala ya ardhi ili kuleta ufanisi katika sekta ya ardhi.
Akizungumza na Watendaji wa sekta ya ardhi wa ofisi ya ardhi mkoa wa Arusha pamoja na wale wa halmashauri za mkoa huo ikiwemo jiji la Arusha, Dkt Mabula alisema uamuzi wa kuanzisha ofsi za ardhi za mikoa ni kutaka kuondoa kero za ardhi sambamba na kusogeza huduma za sekta hiyo karibu na wananchi.

Alisema, ofisi za wilaya na halmashauri katika mikoa zinapaswa kuwatumia wataalamu waliopo ofisi za ardhi za mikoa katika kushughulikia masuala ya upimaji, uthamini na mipango miji ili kuwa na miji iliyopangika na wakati huo wananchi kumilikishwa maeneo yao.
Akielezea suala la upungufu wa watumishi wa sekta ya ardhi kwa baadhi ya halmashauri, Naibu Waziri Mabula alisema kwa sasa wizara yake iko katika mchakato wa kuwapanga upya watumishi wa sekta hiyo baada ya kukamilika zoezi la kupeleka watumishi wa ofisi za ardhi za katika ofisi za mikoa.  
Share To:

Post A Comment: