Na Eliud Rwechungura – Wizara ya Viwanda na Biashara.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent Bashungwa amezielekeza FCC, EWURA, WMA kufanya ukaguzi na kuwachukulia hatua wafanyabiashara na waagizaji wa mafuta wanaoficha bidhaa hiyo kwa lengo la kuyauza kwa bei ya juu yatakapoadimika au kupanda bei.

Waziri Bashungwa aliyasema Juni 17, 2020 jijini Dar es salaam katika kikao kazi na Watendaji wa Mamlaka za Tume ya Ushindani (FCC), Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Wakala wa Vipimo (WMA), Mamlaka ya Bandari (TPA) pamoja na TRA kwa lengo la kufanya mapitio na marekebisho ya utaratibu wa kanuni ya bei elekezi ya mafuta kwa bidhaa za petroli zinazoingizwa nchini kupitia bandari za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga, kwa nia ya kuwezesha manufaa ya punguzo la bei kuwafikia wananchi sa mikoa yote nchini kwa usawa.

‘‘Katika kipindi cha mapambano ya Covid-19, moja ya fursa tulizozipata kama nchi ambayo pia tulipata maambukizi ni kushuka kwa bei ya mafuta, na sisi kwa sababu tunaingiza mafuta kutoka nje ya nchi, kushuka kwa bei ya mafuta duniani sisi tumenufaika lakini pamoja na kunufaika huku kwa kushuka kwa bei ya mafuta kuna baadhi ya mikoa bado bei ipo juu”

Aidha, Bashungwa ametoa onyo kali kwa wafanyabiashara wote ambao bado wana tabia za kuficha bidhaa mbalimbali pindi zinaposhuka bei au kuadimika kwa lengo la kujipatia kipato kikubwa, ameielekeza taasisi ya Tume ya Ushindani na Ewura kufanya msako mkali kama ulifanywa kwenye sukari ili kuwabaini na kuwachukulia hatua wafanyabiashara wote wanaoendeleza tabia hizo

"Wafanyabiashara tunajua bei ambazo wananunulia mafuta na kipindi cha COVID-19, mfanyabiashara yoyote ambaye amenunua mafuta kwa bei ya punguzo lakini punguzo hilo halijaenda moja kwa moja kwa mlaji kwa maana ya mwananchi maeneo yote nchini ambayo wafanyabiashara hawa wanaingiza mafuta na kusambaza, tutatumia taasisi zetu ya Tume ya Ushindani na Ewura kuhakikisha kote nchini tunafatilia na kama kuna mfanyabiashara yoyote wa mafuta ambaye ana hodhi mafuta ili kupata faida tutatumia sheria kumchukukulia hatua kali kama tulivyofanya kwenye sukari,"


Waziri Bashungwa amesisitiza kuwa kuwa mapendekezo ya wataalamu katika kikao kazi hicho yatapelekwa kwa Waziri mwenye dhamana ya Nishati na Madini baada ya kukamilika leo hii ili kumshauri kuhusu namna ya kuweka uwiano sawa wa bei elekezi kwa bidhaa husika, huku akisisitiza kuwa wafanyabiashara watakaobainika kukiuka taratibu za leseni walizopatiwa na EWURA na wanaokiuka kanuni, sheria na taratibu za Ushindani watachukuliwa hatua za kisheria, ikiwamo kunyang'anywa leseni za kufanya biashara ya bidhaa za petrol

Awali, Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Mhandisi Godfrey Chibulunje amesema kuwa “Mafuta yanayouzwa nchini yanapokelewa kupitia bandari za Dar es salaam, Tanga na Mtwara. Katika kukokotoa bei ya mafuta, mikoa ya Kaskazinini (Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara) hupangiwa bei zao kulingana na gharama ya mafuta yanayopokelewa kupitia bandari ya Tanga. Mikoa ya kusini (Mtwara, Lindi na Ruvuma) hupangiwa bei kulingana na gharamaya mafuta yanayopokelewa kupitia bandari ya Mtwara. Mikoa mingine yote hupangiwa bei zao kulingana na gharama ya mafuta yaliyopokelewa kupitia bandari ya Dar es salaam.

Sambamba na hayo Mhandisi Godfrey amesoma mapendekezo ambayo yataleta mabadiliko ya kanuni za kukokotoa bei za mafuta ambayo ni;
Kuweka usawa wa premium kwa bandari zote na hivyo kuwa na bei za mafuta zenye ushindani na watumiaji wa mafuta kununua kwa bei ambayo ina usawa, kuweka kanuni za kubadilisha gharama za mafuta kila mwezi kulingana na mabadiliko ya soko la dunia, kuendelea kuwepo kwa nafasi ya ushiriki wa kampuni za wazawa katika zabuni za BPS.
Share To:

Post A Comment: