Na. Angela Msimbira CHAMWINO

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo ameridhishwa na kasi ya ujenzi unaoendelea katika Hospitali ya Uhuru inayojengwa  katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma.

Waziri Jafo ameyasema hayo leo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua  miradi ya maendeleo ya ujenzi  wa Hospitali  ya Uhuru ambayo inatarajiwa kukamilika  ifikapo Mei, 2020.

Waziri Jafo amesema   pamoja na changamoto zote zilizojitokeza  za mvua ambayo  imeathiri  kazi  kwa kiasi kikubwa  lakini bado SUMA JKT imeendelea kufanyakazi usiku na mchana kuhakikisha kazi inakamilika kwa muda uliyopangwa.

“Nimeridhika na kasi ya ujenzi unaoendelea katika Hospitali ya Uhuru na hasa nimefurahishwa  na  utekelezwaji wa  maagizo yangu  niliyoyatoa  ya kuongeza  nguvukazi, sasa naona  kuna nguvukazi ya watu 300 ambao ni  tofauti na awali walikuwepo 100” ameeleza Waziri Jafo.

Ameutaka uongozi wa Suma JKT kuhakikisha wanasimamia ujenzi wa Hospitali hiyo ili kuweza kukamilisha kazi hiyo kwa wakati uliopangwa.

Waziri Jafo  ameuagiza  uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino  kuhakikisha vifaa vya ujenzi vinanunuliwa kwa wakati ili mkandarasi asipate  shida ya kukamilisha ujenzi wa Hospitali hiyo  katika kipindi kilichopangwa.

Naye Mhandisi wa SUMA JKT Omary Kabalangu amesema kuwa tayari wameongeza kikosi kazi kwa ajili kuongeza nguvu ya ujenzi na watahakikisha wanafanyakazi usiku na mchana ili kukamilisha  ujenzi huo katika muda uliopangwa na Serikali.

Aidha mradi wa Hospitali ya uhuru inajengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Mkoani Dodoma na unagharimu shilingi bilioni 3.99. Fedha za ujenzi zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli, Fedha ambazo zilitakiwa kutumika katika sherehe za maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanganyika Desemba, 9 mwaka 2018ambazo zilitolewa na kammpuni ya simu ya Airtel kama gawio
Share To:

msumbanews

Post A Comment: