Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Katikati) akizungumza wakati akizindua Baraza la wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya TANAPA Jijini Dodoma leo Tarehe 12 Machi 2020. Wengine pichani ni Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Ndg Gerald Kusaya (Kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Mhandisi  Marko Ndonde. (Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akizungumza wakati akizindua Baraza la wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya TANAPA Jijini Dodoma leo Tarehe 12 Machi 2020. 
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Ndg Gerald Kusaya akisisitiza jambo wakati akizungumza kwenye Baraza la wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya TANAPA Jijini Dodoma leo Tarehe 12 Machi 2020. 
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb), Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Ndg Gerald Kusaya akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Baraza la wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya TANAPA Jijini Dodoma leo Tarehe 12 Machi 2020. 

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma

Serikali imeiagiza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kuanisha eneo halisi la umwagiliaji na kulifanyia upya uhakiki ili serikali iwe na Takwimu sahihi za eneo la umwagiliaji nchini.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ametoa agizo hilo leo Tarehe 12 Machi 2020 wakati akizindua Baraza la wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya TANAPA Jijini Dodoma.

Pamoja na agizo hilo kadhalika, Waziri Hasunga ameagiza kuwa kila Afisa Umwagiliaji wa Mkoa na Wilaya awe na orodha ya miradi inayofanya vizuri, na isiyofanya vizuri na ukubwa wa eneo linalofaa kwa umwagiliaji katika Mkoa au Wilaya anayoisimamia.

Pia ameaiagiza Tume hiyo kuweka  utaratibu wa kuandika maandiko ya miradi angalau mawili kila Mwezi kwa ajili ya kutafuta rasilimali fedha kwa wawekezaji wa kutoka ndani na nje ya nchi.

Katika Hotuba yake Waziri Hasunga ameutaja Ujenzi wa mabwawa kuwa ni lazima uwe kipaumbele katika miradi mipya ambayo Tume inatarajia kuianzisha pamoja na kuainisha Taarifa  ya Mabwawa mangapi Tume imepanga kuyajenga.

Katika hatua nyingine Mhe Hasunga amewakanya watumishi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kuacha haraka majungu badala yake kutilia msisitizo katika utendaji kazi.

Kadhalika, amesema kuwa Baraza hilo limehudhuriwa na Wakuu wote wa Idara, Vitengo, Watumishi kutoka ofisi za Umwagiliaji Mikoa na wajumbe wa TUGHE Taifa, Wajumbe kutoka Ofisi za Umwagiliaji za Mikoa, na mjumbe mmoja mmoja mwakilishi wa Wafanyakazi kutoka kila Idara, Vitengo na Ofisi za Mikoa hiyo ni  ishara ya wazi kuwa mkutano huo umekidhi matakwa ya Sheria ya Majadiliano katika Utumishi wa Umma Na. 19 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2005 pamoja na Mkataba wa makubaliano ambao umeafikiwa na pande zote mbili ambazo ni Menejimenti ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji  na Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya Tanzania (TUGHE). 

Amelitaja Baraza la Wafanyakazi kuwa ni chombo muhimu sana ambacho kimepewa nguvu kisheria ili kuwapa watumishi nafasi ya kushiriki katika maamuzi ya masuala mbalimbali yanayohusu utendaji na ufanisi wa Taasisi ili kuongeza tija mahali pa kazi.

MWISHO
Share To:

Post A Comment: