Wananchi wa Kijiji cha Lorbene, Kata ya Msitu wa Tembo, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara wakiwa kwenye picha ya pamoja na mfadhili aliyewachimbia kisima kirefu, Said Nassoro maarufu mzee Mwarabu (mwenye fulana ya mistari miekundu katikati). Ni baada ya wananchi hao kuandamana hadi Kitongoji cha Nyorinyori wakitokea Kijiji cha Lorbene, kama ishara ya kutoa shukrani kwa kupata kisima hicho kilichogharimu sh. milioni 30. (Picha na Yusuph Mussa).



Na Yusuph Mussa, Simanjiro


WANANCHI wa Kijiji cha Lorbene katika Kata ya Msitu wa Tembo, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara wamesema sasa shughuli za maendeleo zitakwenda kwa kasi baada ya wananchi hao kupatiwa maji ya kisima kirefu kilichogharimu sh. milioni 30.


Katika kuonesha furaha yao ya kupata maji, viongozi wa jamii ya kimasai maarufu kama Laigwanani wa kijiji hicho, wamefunga safari kwenda kumpa shukrani mwekezeji Said Nassoro anaechimba madini Kitongoji cha Nyorinyori katika Kijiji cha Lorbene, kwa msaada wa kuwachimbia kisima cha maji wananchi wa eneo hilo.


Viongozi hao wa jamii ya kimasai wametoa shukrani hizo hivi karibuni kwa mwekezaji huyo baada ya kutatua changamoto ya maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo yao ambapo kabla ya msaada huo, wananchi hao walikuwa wakipata maji kwa kusafiri zaidi ya kilomita 20, kwenda kwenye vyanzo vilivyopo milimani, jambo ambalo iliwabidi akinamama kuamka saa 10 usiku na kusafiri kwa usafiri wa punda na kurudi nyumbani usiku wa manane kesho yake. 


"Tunashukuru kwa msaada huu wa kuchimbiwa kisima cha maji, kwani tulikuwa tunasafiri umbali mrefu zaidi ya kilomita 20 kutafuta maji. Wake zetu walikuwa wanasafiri na punda kwenda milimani, wanaondoka usiku wanarudi kesho usiku, hivyo tunamshukuru mzee Mwarabu kwa kisima hiki" alisema Kipara Simangu, Laigwanani wa Lorbene


Simangu, mbali na kutoa shukrani hizo, viongozi hao wa kimasai wametoa wito kwa wawekezaji wengine kuiga moyo huo wa upendo aliouonesha Nassoro  kwa kusaidia jamii kwa hiari yake mwenyewe.


Naye Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Lorbene, Elisha Njaram alisema changamoto ya maji kwenye kijiji hicho ilikuwa kubwa, lakini sasa wananchi wataachana na kutafuta maji mbali, na kujikita kwenye shughuli nyingine za maendeleo.


Mwekezaji Nassoro maarufu kama mzee Mwarabu, alisema ataendelea kutoa misaada ya kuchimba visima vya maji kwa jamii zinazozunguka eneo hilo linalokaliwa na jamii za wafugaji wa kimasai kadri atakavyoweza kwa kuangalia mahitaji muhimu ya binadamu hasa kwa jamii zilizo mbali na miundombinu ya maji. 


Aidha, Nassoro ambae ni mkazi wa Arusha, pia ameweza kuchimba visima viwili vyenye urefu wa zaidi ya mita 180 vilivyogharimu sh. milioni 60 kwenye Kijiji cha Kitwai wilayani Simanjiro kwa ajili ya wananchi na kuvikabidhi kwa Serikali ya kijiji.


Wilaya ya Simanjiro ambayo ni miongoni mwa wilaya zenye maeneo makubwa zaidi kijiografia nchini, imekuwa ikikabiliwa na uhaba wa maji hasa katika maeneo mengi ambayo hukaliwa na jamii za wafugaji pamoja na wanyama pori.

MWISHO.
Share To:

Post A Comment: