Na. James Timber, Mwanza

Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela imepokea kiasi cha shilingi bilioni 1.5 kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya Mradi wa Upimaji wa Viwanja katika eneo la Nyamadoke, ambapo  michoro yenye jumla ya viwanja 1706 vya matumizi mbalimbali vimeandaliwa katika eneo hilo pamoja na vigingi 750 vimeandaliwa.

Katika taarifa yake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela Bw. Shukrani Kyando kwa Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ilieleza kuwa katika kusimamia sheria ya Ardhi Namba 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya Mipango Miji Na 8 ya Mwaka 2007 Halmashauri imeshaingiza kwenye mfumo wa usimamizi wa kodi za ardhi viwanja 58,000 vilivyofunguliwa majalada ya umiliki ambayo ni sawa na asilimia 69 ya viwanja vyote.

Kyando alibainisha kuwa ukaguzi wa viwanja 15,874 visivyoendelezwa na waliobadilisha utaratibu ulifanyika, ambapo viwanja 4,569 vilibainika kutoendelezwa kww mujibu wa sheria na Kata ya Nyamhongoro inaongoza kuwa viwanja 1915 ambavyo havijaendelezwa ikifuatiwa na Buswelu 1200, Nyasaka 528, Kiseke 460, Kirumba 375, Nyakato 40, Buzuruga 21, Mecco 17, na Kitangiri 13.

"Wamiliki wa 1914 tumewapa onyo la kusudio la kufuta miliki zao hadi sasa wamiliki 243 wameshapewa ilani za ubatilisho wa miliki zao kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya mwaka 1999," alisema Kyando.

Kyando alieleza kuwa katika kuthibiti ukuaji holela wa miji na ujenzi usiofuata taratibu za mipango miji halmashauri imeendelea na kasi ya upangaji na upimaji wa maeneo mapya na kuandaa michoro ya ya mipango miji na kupima viwanja katika Mtaa wa Nyafula kata ya Sangabuye, huku upimaji ukiwa umekamilika katika eneo la Mhonze ambapo jumla ya viwanja 5861vimepimwa na kuidhinishwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Upimaji Kanda ya Ziwa na ukaguzi wa wamiliki husika umekamilika.

Aidha Naibu Waziri Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angeline Mabula aliiagiza halmshauri hiyo kuhakikisha wanatoa elimu katika mikutano ya hadhara ikiwemo na kuwahimiza wananchi uchangiani wa zoezi la urasimishaji Makazi husani kulipia gharama za umilikishaji katika mitaa mbalimbali.

Hata hivyo Waziri aliongoza zoezi la ugawaji wa Hati miliki za Viwanja 400 kwa Halmashuri za Nyamangana na Ilemela ambapo alisikiliza na kutatua migogoro mbalimbali ardhi na kuwaomba wananchi kutoa ushiriakiano na halmshauri hasa kwenye zoezi la urasimishaji makazi pamoja na kulipia kodi ya pango la ardhi kwa maendeleo ya taifa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: