Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani wakiangalia jinsi mfumo wa umeme wa moyo wa mgonjwa unavyofanya kazi kabla ya kumwekea kifaa maalum cha kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri (Implantable cardioverter defibrillator – ICD) katika kambi ya matibabu kwa wagonjwa wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo. 
Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani wakiandaa vifaa vitakavyotumika katika upasuaji mdogo wa kumuwekea mgonjwa kifaa maalum cha kuusaidia moyo kufa nya kazi vizuri (Implantable cardioverter defibrillator – ICD) katika kambi ya matibabu kwa wagonjwa wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo. 

Na Genofeva Matemu na Salome Majaliwa 

17/08/2018 Jumla ya wagonjwa 22 wenye matatizo ya moyo yatokanayo na mfumo wa umeme wa moyo usiofanya kazi sawasawa wamefanyiwa upasuaji mdogo na kuwekewa vifaa maalum vitakavyousaidia moyo kufanya kazi vizuri. 

Matibabu hayo yamefanyika katika kambi maalum ya siku saba iliyofanyika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa mgonjwa kufanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab. 

Akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Magonjwa ya moyo ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Moyo Peter Kisenge alisema kambi hiyo inafanywa na madaktari wa Taasisi ya Moyo kwa kushirikiana na wenzao wa nchini Marekani kutoka Shirika la Madaktari Afrika. 

Dkt. Kisenge alisema kambi hiyo ni maalumu kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo ambao mapigo yao yako chini kwa asilimia hamsini kwa dakika kwa kuwawekea kifaa maalum akinachosaidia mapigo ya moyo kuongezeka (Pacemaker). 

“Kazi ya kifaa hiki maalum cha mfumo wa umeme wa moyo ni kuwasaidia wagonjwa wasipoteze maisha ghafla, kwani mara nyingi wagonjwa wenye matatizo ya mapigo ya moyo ambayo yako chini hufa vifo vya ghafla”, alisema Dkt. Kisenge. 

Kuhusu matibabu waliyopatiwa wagonjwa katika kambi hiyo Dkt. Kisenge alisema zoezi limeenda vizuri na kwa ufanisi mkubwa kwa wagonjwa kuwekewa vifaa vya pacemaker na ICD (Implantable cardioverter defibrillator – ICD) kwa wagonjwa ambao mapigo yao ya moyo yako chini ya asilimia 30. 

Kwa upande wake Prof. Matthew Sackett kutoka Madaktari Afrika alisema kambi hiyo ilienda sambamba na utoaji wa elimu kwa madaktari na wataalam wengine wa afya ambao baada ya mafunzo hayo wataweza kuwawekea wagonjwa kifaa cha ICD ambapo kabla ya hapo hawakuwa wanaweza kufanya hivyo. 

“Wiki hii imekuwa ni wiki ya mafanikio kwetu, tumetibu wagonjwa na nimetoa elimu ya namna ya kumuwekea mgonjwa kifaa cha ICD kwa madaktari na wataalam wengine wa afya, kila nitakapopata nafasi nitakuja kutoa huduma kwa wagonjwa na elimu kwa wafanyakazi”, alisema Prof. Sacckett
Share To:

msumbanews

Post A Comment: