Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ali Hapi amemsimamisha kazi mwanasheria wa manispaa ya Kinondoni, Anord Kinyaiya.

Kinyaiya amesimamishwa kazi jana Jumanne Julai 24, 2018 kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwakumbatia watu wanaolalamikiwa na wananchi.

Hapi amechukua uamuzi huo baada ya wananchi kutoa kero zao katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kinondoni Shamba, wakiwemo wafanyakazi 13 wa kampuni ya kuzoa taka ya Total West Solution walioeleza jinsi wanavyozungushwa kulipwa kiasi cha Sh15milioni wanazodai.

Mmoja wa wafanyakazi wa kampuni hiyo,  Ridhiwan Hussen amesema waliwasilisha malalamiko yao kwa mkuu huyo wa wilaya na kutakiwa kwenda kwa mwanasheria huyo ili wapitie madeni wanayoidai kampuni hiyo.

Amedai walipofika kwa Kinyaiya aliwazungusha na kuwatamkia wazi kuwa Hapi hana mamlaka ya kushughulikia suala lao.

“Binafsi ninadai mshahara wa miezi 11, watu wote 13 tunadai Sh15milioni,  hata tunapokwenda ofisini kwa mwanasheria, meneja wa kampuni nae hatokei na wamekuwa na utaratibu wa kuwasiliana wao wenyewe, kwa kweli inatupa shaka sana,” alisema Hussein.

Alisema anashangazwa na Kinyaiya kuwapendelea  wenye fedha badala ya wananchi wanyonge wanaodai haki yao.

“Ninakusimamisha kazi na sitaki kukuona katika ofisi yangu. Ninataka wakuchunguze hayo mambo unayolalamikiwa na ikibainika utachukuliwa hatua za kisheria,” alisema Hapi.

“Polisi mkamateni huyu meneja popote atakapokuwepo na awekwe ndani kwa saa 48 na baadaye achukuliwe hatua za kisheria ili awalipe vijana hawa mishahara yao.”
Share To:

msumbanews

Post A Comment: