KIUNGO wa Yanga, Thabani Kamusoko, amesema Azam walistahili ushindi kwenye mchezo wao wa mwisho wa Ligi Kuu uliopigwa Uwanja wa Taifa juzi usiku.

Azam iliibamiza Yanga mabao 3-1 na hivyo kumaliza ligi kwenye nafasi ya pili nyuma ya Simba huku Yanga ikimaliza nafasi ya tatu.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Kamusoko, aliweka wazi kuwa hawakuwa wakicheza kama wanataka ushindi.

"Tulikuwa tofauti, hatukuwa kama Azam ambao tangu kuanza kwa mchezo walikuwa wakionekana kusaka ushindi, lakini pia na sisi hatukuwa na bahati," alisema Kamusoko.

Alisema ligi ilikuwa ngumu na walikuwa wakipitia kwenye changamoto na kila mwanachama na shabiki wa Yanga analifahamu hilo.

Akizungumzia mustakabali wake ndani ya timu hiyo kwa msimu ujao, Kamusoko, alisema hajafahamu na asingependa kulizungumzia jambo hilo.

Kamusoko ameshuhudia raia mwenzake wa Zimbabwe kwenye kikosi cha Yanga, Donald Ngoma, akiachana na timu hiyo na kujiunga na Azam FC mapema wiki hii.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: