Mbunge wa Vunjo kupitia NCCR – Mageuzi James Mbatia, amesema suala la upotevu wa trilioni 1.5 kwenye ripoti ya CAG sio jambo dogo bali ni janga la kitaifa, kwani fedha hiyo ingeweza kufanya mambo makubwa kwa wananchi wake, ikiwemo ujenzi wa barabara.

Akizungumza Bungeni leo Mheshimiwa Mbatia amesema kuna matukio mengi yanayotokea nchini lakini hayapatiwi ufumbuzi, ikiwemo miradi mibovu inayoteketeza pesa za umma ambazo zingeweza kufanya shughuli za maendeleo, lakini masuala hayo yamekuwa hayafanyiwi muendelezo au kupata muafaka wake.

"Leo hii Jangwani maji yaliyofurika pale, mafuriko yaliyotokea juzi, mradi uliotekelezwa pale, nguvu iliyowekezwa pale, investment iliyowekezwa pale nani anawajibika kwa kushauri ujinga huo wa depo ya Dar es salaam Rapid Transport !? Ukisoma ile taarifa ya CAG hili ni janga la kitaifa la 1.5 trilioni, hii ni kashfa juu ya kashfa, hakuna muendelezo, ule mradi wa kutoka DSM mpaka Bagamoyo boat kashfa, hii kashfa, ATCL kashfa nyingine”, amesema James Mabtia.

James Mbatia ameendelea kwa kuitaka serikali kukubali mawazo ya watu tofauti tofauti katika utekelezaji wa miradi mbali mbali na masuala mengine, ili kujiepusha na lawama kama hizo.

“Lazima kukubali mawazo mbadala, tushirikiane vizuri, tufanye kazi vizuri, kwa kuwa Tanzania ni yetu sote, tusipofuata katiba, tusipofuata sheria, Bunge likajua fasi yake, kuangalia kodi za Watanzania kama zinatumika vizuri, la sivyo Bunge hili litakuja kuhukumiwa kwa nini haya yanatokea”,amesema James Mbatia.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: