Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeukemea upande wa Jamhuri kwa kushindwa kutekeleza amri ya kumpeleka  mshtakiwa katika kesi ya uhujumu uchumi, Harbinder Sethi kutibiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi imeonyesha kutoridhishwa na kitendo hicho leo Jumatano Aprili 11, wakati kesi hiyo ilipokuwa inatajwa.

“Kila chombo kifanye kazi kwa kuheshimiana kwani haipendezi kila mara amri za mahakama haziheshimiwi.

“Mahakama lazima ifanye kazi yake kwa mujibu wa sheria na haipendezi amri za mahakama kutoheshimiwa. Wala huhitaji kuwa daktari, ukimuangalia kwa macho tu mshtakiwa wa kwanza anaonekana anaumwa, suala la ugonjwa wake tumuachie daktari,” amesema Shaidi akijibu hoja za Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga kwamba lazima daktari wa mshtakiwa huyo awepo.

Katuga amedai kuwa Sethi aliomba wakati anapelekwa Muhimbili Daktari wake wa Afrika Kusini awepo ambapo wanasubiri taarifa kutoka kwa mshtakiwa na kwamba sababu nyingine ya kutotekeleza amri ya mahakama kwa wakati ni kwa mshtakiwa kuhamishwa gereza kutoka Segerea kwenda Ukonga.

Akijibu hoja hizo wakili wa Sethi, Hajra Mungula alidai kuwa mshtakiwa hajaongea chochote na wanashtushwa na maneno yaliyotolewa na upande wa mashtaka.

Kwa upande wake Wakili wa mfanyabiashara James Rugemarila, Cuthbert Tenga amedai amri za mahakama zinachukuliwa kirahisi na kwamba kila siku upelelezi haujakamilika ambapo ameomba Kamishna wa Magereza aitwe mahakamani ili aeleze kwanini amri za mahakama hazitekelezwi. Kesi hiyo omeahirishwa hadi Aprili 25, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: