Hatua ya wakuu wawili wa mikoa, Paul Makonda na Alexander Mnyeti kutoa matamko ya kusimamisha shughuli au kuvunja mabaraza ya kata, Serikali imesema inaandaa mwongozo kuhusu suala hilo.

Jumatatu iliyopita, Makonda ambaye ni mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alitoa tamko la kusimamisha mabaraza hayo katika mkoa wake kabla ya Mnyeti wa Mkoa wa Manyara kutamka kuvunja baraza la Ardhi Kata ya Murray, wilayani Mbulu juzi.

Alipotafutwa jana kuzungumzia hatua za wakuu hao, katibu mkuu Ofisi ya Rais (Tamisemi), Mussa Iyombe alisema, “Tunakamilisha mwongozo kuhusu suala hilo wiki hii, fanyeni subira.”
Uamuzi wa Mnyeti
Mnyeti alitangaza uamuzi huo baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kunyanyaswa, kuombwa rushwa na kunyimwa haki.

Akizungumza katika kata hiyo alisema hawezi kuliacha baraza hilo liendelee kufanya kazi ilihali wananchi wanalalamika kukosa haki.

Alimuagiza mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Anna Mbogo kuanza mchakato wa kupatikana viongozi wapya waadilifu wa baraza hilo la kata ili waendelee kuwatumikia wananchi na kuagiza mikutano ya wananchi kuwachagua wajumbe wengine ianze upya.

“Tafuteni watu waadilifu, wenye weledi na hofu ya Mungu, ambao wanaweza kuwahudumia wananchi ili washike nafasi hizo na kutekeleza majukumu yao ipasavyo,” alisema Mnyeti.

Hatua ya Mnyeti ilitokana na malalamiko kutoka kwa mkazi wa Murray, Michael Amme kwamba baraza hilo halitendi haki na wananchi wanyonge wanaonewa. Amme alidai kwamba familia yake iliporwa eneo kutokana na uamuzi wa baraza hilo.

Mjumbe wa baraza hilo, Verani Anthony alisema wananchi wanapaswa kupatiwa elimu kuhusu utendaji kazi wa baraza hilo kwa kuwa wao hutekeleza wajibu wao ipasavyo.

Kuhusu Makonda

Juzi, Iyombe akizungumza na mwandishi wetu kuhusu tamko la Makonda, alisema mkuu huyo wa mkoa ameshatoa ufafanuzi kwa maandishi akikana kusimamisha mabaraza hayo kufanya kazi

“Tulimtaka atuandikie barua ya kutueleza na tayari ameshafanya hivyo, tumemalizana naye kwa maandishi, hakusimamisha mabaraza hayo kufanya kazi,” alisema Iyombe.

Hata hivyo, katibu mkuu huyo alipoulizwa kama Makonda alitakiwa kuandika barua baada ya kuvunja kipengele kipi cha sheria kutokana na tamko lake, alisema:

“Sitaki kusema alivunja kipengele ni wewe wasema, ninachosema kama kiongozi lazima unachokisema wananchi wakielewe, kulikuwa na maswali watu wanahoji kuhusu suala hilo ndiyo maana tukamtaka atufafanulie na amefanya hivyo kwa maandishi. ”

Source :Mcl
Share To:

msumbanews

Post A Comment: