Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini  Mh. Anthony Mavunde ameanzisha ujenzi wa wodi ya wakinamama katika Zahanati ya Kikuyu Kaskazini ikiwa ni utekelezaji wa ahadi zake katika kuboresha huduma ya Afya ya mama na mtoto.

Ujenzi wa wodi hiyo umeanza rasmi baada ya zahanati hiyo kupokea kiasi cha fedha cha Tsh33,612,800 kutoka katika Mfuko wa kuchochea maendeleo ya Jimbo la Dodoma Mjini.

“Nafurahi leo kuona ndoto ya wakina mama wa Kikuyu kuwa na sehemu nzuri na yenye staha ya kupata huduma ya afya ya uzazi inakamilika.

Mfuko wa Jimbo uliona umuhimu wa kuboresha huduma ya Afya kwa mama na mtoto ndio maana tumetoa fedha hizi milioni 33 ili kufanikisha ujenzi wa wodi hii ya wakina mama.

Niwapongeze Diwani,Daktari Mfawidhi wa Zahanati na kamati ya ujenzi kwa usimamizi mzuri kwa kila hatua,hakikisheni jengo hili linajengwa kwa viwango vya ubora wa juu kwa kuzingatia gharama halisi za mradi.

Najua fedha hizi kupitia Mfuko wa Jimbo hazitakamilisha ujenzi wote wa jengo hili,nataka niwaahidi kwamba tutatafuta vyanzo vingine vya fedha kuhakikisha jengo hili linaanza kutoa huduma mwaka huu 2022”Alisema Mavunde

Akiwasilisha taarifa fupi ya ujenzi,Dr. Azania Omari Silliah amepongeza jitihada za Mbunge Mavunde katika kutatua changamoto za Afya na kwamba wodi hiyo ikikamilika itakuwa na uwezo wa kuwahudumia wakina mama zaidi 800 kwa mwaka kutoka kata ya kikuyu kaskazini na kata jirani.

Naye Diwani wa Kata ya kikuyu kaskazini,Mh. Israel Mwansasu amemshukuru Mbunge Mavunde kwa ambavyo amekuwa chachu ya kuleta maendeleo katika kata hiyo na kuahidi kusimamia ipasavyo ujenzi mpaka ukamilishwaji wa wodi hiyo ili ianze kutumika na wakina mama wa kikuyu.









Share To:

Post A Comment: