Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida  Mhe.Aysharose Mattembe (wa pili kushoto) akikabidhi  mbegu za alizeti  kwa  vikundi vya wanawake mkoani hapa  ikiwa ni jitihada za  kuunga mkono juhudi za Serikali kuongeza uzalishaji wa zao hilo.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida  Mhe.Aysharose Mattembe (wa pili kushoto) na akina mama wakionesha mifuko ya mbegu alizowakabidhi.

Hafla ya makabidhiano ya mbegu hizo ikiendelea.


Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida  Mhe.Aysharose Mattembe (katikati) akiwa amevikwa vazi la kimila katika hafla hiyo.

Makabidhiano ya mbegu hizo yakiendelea.
Makabidhiano ya mbegu hizo yalikiendelea.
Ni furaha tupu katika hafla hiyo.


Na Dotto Mwaibale, Singida


MBUNGE  wa Viti Maalum Mkoa wa Singida  Mhe.Aysharose Mattembe amegawa tani 10 za mbegu za alizeti  kwa  vikundi vya wanawake mkoani hapa  ikiwa ni jitihada za  kuunga mkono juhudi za Serikali kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

Akizungumza wakati wa hafla ya kugawa mbegu hizo iliyofanyika  Chuo cha Ufundi  Stadi VETA mjini hapa leo Mattembe alisema zoezi hilo limelenga kuongeza uzalishaji wa zao hilo ili kusaidia azma ya Serikali kupunguza uhaba wa mafuta ya kula nchini, ambapo kila mwaka imekuwa ikitumia mabilioni ya fedha kuagiza mafuta hayo nje ya nchi.

Alisema mkakati huo ni endelevu na unalenga kumwezesha mwanamke kujikwamua kiuchumi na  kuwashukuru akina mama hao kwa niamna wanavyoendelea kumuunga mkono kama mwakilishi wao bungeni ambapo ameaahidi  kuendelea kushirikiana nao kuondoa kero zinazowakabili.

Mattembe amewataka wanawake kufanya kazi kwa bidii ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais  Samia,  Suluhu Hassan walime angalau ekari mbili za zao la alizeti ili kuondoa adha ya uhaba wa mafuta ya kula nchini na kuongeza pato la mtu mmoja mmoja na pato la Taifa kwa ujumla.

Mattembe alisema Rais Samia Suluhu Hassan ni kiongozi  makini na mahiri anayepaswa kuigwa na ametumia fursa hiyo kumpongeza kwa kazi nzuri anazowafanyia wananchi wa Mkoa wa Singida ambao umepokea fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya afya, maji, elimu na ujenzi wa barabara na madaraja.

Akitoa mada ya namna ya kulima zao la alizeti kwa tija Mtaalam kutoka Shirika la Farm Afrika,Tumaini Elibariki alisema  mbegu alizotoa Mattembe ni bora na za kisasa na alitumia fursa hiyo kuwaelimisha kanuni za kilimo cha alizeti.

Baadhi ya akina mama waliohudhuria ugawaji huo wa mbegu  za alizeti akiwemo Katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania Mkoa wa Singida Edina Kugulu amempongeza Mattembe na amewataka wanawake waliohudhuria hafla hiyo kwenda kuwa mfano katika Uzalishaji wa zao la alizeti.

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: