Na Mwandishi wetu ,Mbeya



TAASISI  ya Tulia Trust inayoongozwa na Mbunge wa Mbeya Mjini ambaye pia ni Naibu Spika Dkt Tulia Ackson imeanza ujenzi wa soko la Uyole ya Kati Kata ya Iganjo Jijini Mbeya lililoteketea kwa moto.



Meneja wa Tulia Trust ,Jacqueline Boaz amesema wao kama taasisi wametoa msaada huo baada ya kupata taarifa kutoka kwa Katibu wa Mbunge Stephen Chambanenge.



Naye Katibu wa Mbunge Stephen Chambanenge mbali ya kuwapa pole baada ya kufika eneo la tukio amesema Mbunge Dkt Tulia Ackson yupo pamoja nao katika kipindi hiki kigumu.



Aidha amesema kupitia taasisi yake wanaanza ujenzi mara moja ili wafanyabiashara hao waendelee kufanya shughuli zao.



Diwani wa Kata ya Iganjo Eliud Mbogela amemshukuru Mbunge kwa moyo wa huruma na utayari wa kuwasaidia wananchi wake.



Baadhi ya wafanyabiashara wakiwemo Mama Lishe na Baba Lishe wamesema msaada wa Mbunge umekuwa na faraja sana kwao kwani walikuwa hawajui cha kufanya.



Joshua Lufaga ni mmoja wa wakazi eneo hilo amesema walijitahidi kuokoa baadhi ya bidhaa katika vibanda.



Mstahiki Meya Jiji la Mbeya Dour Issah Mohammed amefika kuwapa pole wahanga sambamba na kuchangia misumari kwa ajili ya ujenzi akiungana na wadau mbalimbali kuchangia misumari.



Moto umeanza usiku wa manane oktoba 21,2021 ambapo chanzo cha moto mpaka sasa bado hakijafahamika.

Share To:

Post A Comment: