Na Hamida Ramadhani Dodoma

WAZIRI wa Nishati Dkt Medard Kalemani amewataka mafundi wa umeme kuunganisha Mifumo ya umeme ,kwa kuzingatia usalama kwani Sekta hiyo imeendelea kukua hadi Vijijini.


Ameyasema hayo leo jijini hapa kwenye mafunzo kwa mafundi wa umeme Kuhusu sheria ya umeme ya Mwaka 2008 na kanuni za ufungaji wa umeme za mwaka 2019.


Amesema Serikali imekuwa  ikifanya Kazi kubwa kuwafikishia wananchi Nishati ya umeme maeneo yote nchini hivyo mafundi wenye weledi wenye kuweza kufanya Kazi ya ufungaji  na uunganishwaji wa umeme majumbani na sehemu zingine.


"Ikumbukwe kwamba Maendeleo ya viwanda nchini yanategemea Sana Nishati ya umeme hivyo mchango wenu wa utaalam kama mafundi umeme au wakandarasi wa umeme ni muhimu ,".


Na kuongeza kuwa "Ni vyema sasa kufahamu wajibu wa kila mdau katika kutekeleza majukumu yenu kwa nijibu wa sheria na kanuni zilizopo," amesema Kalemani.



Pia amesema mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka katika Mikoa ya kanada ya Kati kwa kuzingatia maelekezo wa serikali inayoongozwa na Raisi wa Awamu ya Sita Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akielekeza kila mtu afanye Kazi yake kwa kuzingatia sheria na taratibu za nchi.


Kwa Upande wake Kaimu  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji ( EWURA) Godfrey Chibulunje amesema Tasnia ya wakandarasi wa umeme imekuwa ikikabiliwa na changamoto zikiwemo ,mafundi wasiosajiliwa  na wanafanya Kazi bila usimamizi na kupekekea Kazi nyingi kufanyiwa chini ya kiwango na hata kusababisha ajali za moto  muda mfupi baada ya kukamikika.


" Kutokana na hayo yote ni lazima uwepo utaratibu wa kuwatambua wataalamu mbalimbali  kwa kutumia Leseni ambazo zina madaraja mbalimbali na kiwango Cha uzoefu na weledi,' amesema Chibulunje.


Sambamba na hilo amesema EWURA imeandaa mkutano huo kwa lengo la kutoa elimu Kuhusu sheria na kanuni ambazo mnatakiwa kuzingatia  wakati wa utendaji Kazi wao Ili kuweza kuimarisha Usalama wa Watu na mali zao.


"Matarajio yetu baada ya mafunzo haya utendaji wenu wa Kazi utaboreka kwa kufuatia sheria na kanuni na taratibu zilizopo ," amesema Chibulunje.

Mwisho

Share To:

msumbanews

Post A Comment: