Na Emmanuel Malegi-DSM


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima ameridhishwa na uzalishaji wa dawa katika kiwanda cha dawa cha Keko Pharmaceutical na kusema kuwa kiwanda hicho kimeanza kutekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi.


Waziri Gwajima amesema hayo baada ya kufanya ziara kiwandani hapo mapema leo ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi kwenye Bohari ya dawa (MSD) na kutembelea maeneo mbalimbali ya kiwanda hicho na kuona jinsi uzalishaji wa dawa unavyoendelea huku katika kipindi cha miezi miwili (Oktoba mpaka Disemba) kimetengeneza vidonge vya Paracetamol Milioni 25. 


"Pamoja na kuwa kwamba MSD mlikua na majukumu matatu, kununua, kutunza na kusambaza lakini kwa kujibu maelekezo ya Serikali na mahitaji ya sasa mmeamua kufanya masuala ya uzalishaji, mmeweza kusimamia na kuhakikisha hisa za Serikali zimeongezeka kwenye kiwanda kwa asilimia 70 ambapo sasa mnazalisha vidonge vya Paracetamol Milioni 25 kwa miezi miwili. "Haya ndo maendeleo ambayo mnatakiwa taasisi kujiongeza kufuata mwelekeo wa nchi". Amesema Waziri Gwajima.


Aidha, Waziri huyo amesema idadi hiyo  ya vidonge inayozalishwa imeokoa fedha za Serikali kwa kiasi kikubwa ambapo kama vingeagizwa nje ya nchi Serikali ingetumia gharama kubwa.


Waziri Gwajima amewataka wakuu wa Taasisi kujiongeza ili waende na mahitaji ya sasa kwa kutekeleza majukumu yake lakini pia iende na mwelekeo wa nchi na kujibu changamoto za kiuchumi duniani pamoja na changamoto za ongezeko la magonjwa ili yaweze kudhibitiwa na kutibiwa.


"Nimefarijika sana na Serikali ipo pamoja na nyie, sio MSD pekee bali hata taasisi nyingine zote ambazo zina uwezo wa kuzalisha kitu fulani ndani ya taaluma na miundombinu yake". Ameongeza Dkt. Gwajima.


Pamoja na hayo Waziri Gwajima amefanya kikao na Menejimenti ya MSD  ili kuweze kupata changamoto mbalimbali zinazowakabili na kupata muafaka wa pamoja


-MWISHO-

Share To:

Post A Comment: