Asteria Muhozya na Steven Nyamiti, Arusha


Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya, amekitaka Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC)  kutangaza Huduma zinazotolewa kituoni hapo  ikiwemo mafunzo ya Uongezaji thamani madini yanayotolewa ili kukiwezesha kukua na kutambulika kwa wadau wengi zaidi wa ndani na nje ya nchi.


Prof. Manya ameyasema hayo baada ya kukitembelea kituo hicho Desemba 17, 2020 ambapo alionesha kufurahishwa na bidhaa zinazotengenezwa kituoni hapo ikiwemo  za mapambo na hivyo kukitaka kukua kwa kutumia rasilimali zake zilizopo hivi sasa.


Aidha, amesisitiza kituo hicho kutumia vyombo vya habari kujitangaza kwa lengo la kuwezesha mafunzo na huduma zake  kutambulika zaidi kwa walio wengi suala ambalo litawezesha adhma ya Serikali kuchochea shughuli za uongezaji thamani nchini kufanikiwa.


 “Mafunzo yanayotolewa na kituo hiki yanawaandaa vijana ili waweze kuwa na ujuzi wa kuongeza thamani kwenye madini yetu. Lakini pia nimeona kuna wageni kutoka nje ya nchi na wameeleza kabisa hapa wanapata mafunzo mazuri sana,’’ amesema Prof. Manya.


Ameongeza kuwa, kituo hicho kinayo maabara ya kupima madini ya vito, hivyo, hakuna haja ya watanzania kudanganywa kwani ipo sehemu ambayo wanaweza kupata huduma ya kutambua madini halisi na yaliyotengenezwa. 


Katika hatua nyingine Prof. Manya amekipongeza Kituo cha TGC kwa kutoa mafunzo ya muda mfupi katika fani ya Ukataji na ung’arishaji wa madini ya vito, fani ya Usonara, fani ya Uchongaji wa Vinyago vya Vito, Utambuzi wa Madini ya Vito na Utengenezaji wa bidhaa za mapambo na urembo na kueleza kuwa, mafunzo hayo yanalenga katika kuongeza tija kwenye sekta ya madini ikiwemo kutoa nafasi ya ajira kwa watanzania ikiwemo kujiajiri.


Kituo cha TGC kipo jijini Arusha, kwa mujibu wa Mratibu wa Kituo hicho, vijana wengi ambao wamehitimu katika kituo hicho wamepata nafasi ya kuajiriwa katika kampuni zinazofanya shughuli za uongezaji thamani jijini humo kutokana na kuwa na ujuzi wa kiwango cha juu.

Share To:

Post A Comment: