Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo amewataka Wakala wa barabara za vijijini na Mijini(TARURA) wanaosimamia ujenzi barabara ya mzunguko katika Mji wa Serikali Mtumba, Jijini Dodoma kukamilisha ujenzi huo ndani ya muda uliowekwa.


Jafo ametoa agizo hilo wakati alipotembelea eneo la ujenzi wa barabara hizo zinazoendelea kujengwa kwenye  Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma na kubaini ujenzi kuwa nyuma ya muda uliowekwa kwa asilimia mbili (2%).


“Mmeniambia changamoto ni mvua na ugonjwa wa CORONA kwangu mimi sioni sababu ya msingi kati ya hizo mlizotaja sababu mpaka sasa hivi msimu wa mvua bado haujaanza na hakuna mvua kubwa iliyonyesha ya kusababisha ucheleweshaji wa ujenzi huu kwa namna yeyote.


Ugonjwa wa CORONA pia sioni ni kwa namna gani  ulivyoathiri ujenzi huu, ninachotaka ni barabara hii kukamilika kwa wakati uliopangwa” Alisema Jafo


Ninachokiona hapa ni kuwa huyu Mkandarasi ana kazi nyingi kitu kinachompelekea kugawanya vifaa na mitambo yake kwenye site zingine na kusababisha baadhi ya maeneo  kazi kudorora kutokana na uchache wa vifaa aliongeza Jafo.


Akitoa taarifa ya ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa Km 51.2 Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seif amesema ujenzi umefikia asilimia 48 ambapo kwa mujibu wa ratiba ilitakiwa kufikia asilimia 50.


Mhandishi Seif aliongeza kuwa ujenzi wa barabara  hizo unahusisha ujenzi wa barabara za njia nne zenye urefu wa Km 11.2, ujenzi wa njia mbili zenye urefu wa Km 28.8, ujenzi wa kalavati, mifereji ya maji ya mvua, barabara za waenda kwa miguu pamoja na taa za barabarani.


Mradi  wa ujenzi wa barabara za Mji wa Serikali Mtumba unatekelezwa na Mkandarasi China Hainan International Cooperation Co. Ltd (CHICO) kwa gharama ya Tsh Bil 88.1 na muda wa ujenzi ni miezi 18 ambapo utakamilika 31/7/2021.


Mwisho.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: