Leo tarehe 01 Oktoba, 2020 Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila amekutana na watendaji wa Kampuni ya  Madini ya Twiga jijini Dodoma kwa ajili ya kupata taarifa  ya utekelezaji wa kampuni hiyo pamoja na changamoto zake kwenye shughuli za uchimbaji wa madini.

Wengine waliohudhuria katika kiko hicho ni pamoja na Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula, Kamishna wa Tume ya Madini, Dkt. Athanas Macheyeki, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya, Kamishna Msaidizi- Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye Sekta ya Madini kutoka Wizara ya Madini, Terace Ngole na watendaji wengine kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini.

Akizungumza mara baada ya kupokea taarifa ya utendaji wa kampuni hiyo, Profesa Msanjila ameitaka kampuni ya Twiga kuhakikisha inatoa kipaumbele cha ajira kwa watanzania wenye sifa kama Sera ya Ushirikishwaji wa Watanzania kwenye Sekta ya Madini inavyotaka.

“Ni vyema mkahakikisha ajira ambazo watanzania wenye sifa wanaweza kupata zinatolewa, badala ya kutoa ajira kwa wageni pekee,” amesema Profesa Msanjila.

Katika hatua nyingine, Profesa Msanjila ameitaka kampuni ya Twiga  kuhakikisha inatangaza mpango wa manunuzi wa mwaka katika vyombo vya habari kama vile magazeti na tovuti mbalimbali ili kutoa fursa kwa watanzania wengi kujipanga na kuomba zabuni za kutoa huduma kwenye kampuni hiyo.

Aidha, Profesa Msanjila ameitaka kampuni hiyo kuhakikisha kunakuwepo na usawa wa viwango vya mishahara kulingana na sifa na uzoefu wa wataalam wa Tanzania na wa kutoka nje badala ya kuwepo na utofauti kulingana na uraia.

Awali akielezea utendaji wa kampuni hiyo Meneja wake, Benedict Busunzu ameeleza kuwa katika shughuli zake za kila siku kampuni imekuwa ikishirikisha jamii inayozunguka mgodi wake fursa za biashara na kununua bidhaa mbalimbali kutoka katika jamii husika.

Ameongeza kuwa, kampuni inaendelea kubuni teknolojia mbalimbali ili kuhakikisha shughuli za uchimbaji wa madini zinaleta tija huku wakizingatia usalama wa afya na mazingira.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: