Na John Walter- Mbulu

Mgombea Mwenza wa Kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi ambae pia ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiwa katika mwendelezo wa Kampeni za kumuombea mgombea Urais wa Chama hicho Ndugu John Magufuli, Madiwani na Wabunge wa Ccm  katika mkoa wa Manyara amepokelewa kwa Shangwe na Maelfu ya wananchi wa Jimbo la Mbulu mjini huku wakiahidi kukipigia kura chama hicho ifikapo Oktoba 28 mwaka huu.

Akizungumza na Wananchi hao Samia amesema serikali imefanya mengi katika Jimbo la Mbulu Mji kwenye Sekta ya Afya,Elimu na Miundombinu ya bara bara ambapo kwa sasa inakwenda kutekeleza Ujenzi wa bara bara kutoka Karatu-Mbulu-Hydom mpaka Singida Kilomita 190 baada ya kufanya upembuzi yakinifu.

Samia amesema ujenzi wa bara bara hiyo utaanza muda wowote kwa kilomita 50 awamu ya kwanza.

Ameongeza kuwa bara bara ya Mbulu hadi Mbuyu wa Mjerumani kilomita 63 upembuzi yakinifu unakamilika na michoro itakapokabidhiwa itajengwa kwa kiwango cha Lami.

Aidha amesema mbali na kilomita 5 bara bara ya lami ilizoahidwa na Rais Magufuli, wamepokea ombi la Mbunge Zakaria Isaay za kuongezewa Kilomita 20.





Share To:

Post A Comment: