Mamlaka  ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imevitoza faini ya Sh milioni 30 vyombo vya habari sita, kwa kukiuka kanuni na maadili ya utangazaji ikiwamo redio ya Clouds FM kuzungumzia supu ya pweza kuimarisha tendo la ndoa katika muda ambao wasikilizaji wanaweza kuwa watoto.

Mbali ya Clouds FM, vyombo vingine vilivyoadhibiwa ni East Africa Radio, na televisheni za Star, Sibuka, na Global Tv na Duma Tv.

Akisoma uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui ya TCRA, Joseph Mapunda alisema vyombo hivyo vilikiuka kanuni za mawasiliano kwa nyakati tofauti.

Mapunda alisema redio ya Clouds FM kupitia kipindi chake cha Jahazi, walihamasisha vitendo vya ngono, kwa kutumia supu ya pweza katika kuimarisha tendo la ndoa kwa muda ambao wasikilizaji wanaweza kuwa watoto.

Alisema baada ya kusikiliza utetezi wao, wanatozwa faini ya Sh milioni saba na kupewa onyo kali baada ya kuwatia hatiani kwa kosa hilo.

Katika shauri lingine, kituo cha Duma TV kimetozwa faini ya Sh milioni saba na kufungiwa kuchapisha maudhui kwa muda wa mwezi mmoja ili wajipange na kuzifahamu kanuni na kuzingatia weledi na maadili ya utangazaji.

Mapunda alisema Duma ilikutwa na hatia ya kukiuka kanuni kwa kuchapisha na kutangaza maudhui yenye lugha isiyo na staha na iliyo na udhalilishaji wa kijinsia kwa wanaume na wanawake.

Alisema redio ya East Africa imetozwa faini ya Sh milioni tatu na kupewa onyo kali kwa kukiuka kanuni hiyo, kwa kurusha maudhui ya kukashifu utendaji wa serikali kupitia uteuzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kutumia lugha ya kashfa dhidi ya utendaji wake.

Vilevile Global Tv imetozwa Sh milioni saba na kupewa onyo kali, baada ya kupatikana na hatia ya kuchapisha picha ya mnato na kutangaza maudhui yasiyokuwa na lugha ya staha na yenye kushabikia vitendo vya mahusiano ya kimapenzi ya jinsia moja.

Mapunda alisema maudhui hayo, yangeweza kuwaumiza na kuwakwaza waumini wa dhebebu la Anglikana na Watanzania kwa ujumla. Pia, alisema Sibuka Tv inatozwa faini ya Sh milioni tatu baada ya kupatikana na hatia ya kushabikia mauaji ya kutisha katika muda, ambao watoto wanaweza kuwa sehemu kubwa ya watazamaji.
Share To:

Post A Comment: