Na WAMJW- Kilimanjaro
Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla ameweka wazi kuwa, Tanzania ipo tayari kupokea wageni kutoka sehemu yoyote Dunia kwa ajili ya utalii, kufuatia kuimarisha mifumo ya tahadhari zote za kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

Dkt. Kigwangalla ameyasema hayo leo katika ziara iliyomjumuisha Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel ikiwa na lengo la kukagua utayari wa nchi katika kudhibiti ugonjwa wa Corona katika uwanja wa ndege wa KIA na kupokea magari manne ya kubeba wagonjwa endapo watatokea pindi wawapo nchini kwenye utalii.

Dkt. Kigwangalla amesema kuwa, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kudhibiti maambukizi ya Virusi vya Corona, ikiwemo kuweka miongozo wakati wa kuingia na kutoka uwanja wa ndege, muongozo wa namna ya kusafirisha watalii pamoja na muongozo wa namna ya kuandaa chumba cha wageni

“Katika kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa wa Corona Duniani, tumeweka miongozo kwa pale uwanja wa ndege, tumeweka muongozo wakati wa kuingia na kutoka tumeweka muongozo namna ya kusafisha Watalii kutoka uwanja wa ndege mpaka hotelini, tumeweka muongozo namna ya kuandaa chumba cha mgeni, namna ya kuandaa chakula, kila kitu tumeweka muongozo ” alisema

Aliendelea kusema kuwa, Serikali imechagua baadhi ya vituo vya Afya mahususi kwa ajili ya watalii Mkoani Arusha, Serengeti na Ngorongoro lengo ni kuthibitisha usalama wa afya ya Watalii waingiapo nchini.

Naye Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel amesema kuwa, Serikali imepokea magari manne ya kubeba wagonjwa(ambulance) yaliyokidhi miongozo ambayo yametolewa na wakala wa huduma za utalii nchini ikiwa ni sehemu ya tahadhari katika kuhakikisha usalama wa Watalii wataoingia nchini.

“Tumeona magari ambayo yamezingatia zile taratibu na miongozo yote ambayo inatakiwa kuhakikisha Watalii wetu wapo salama na endapo kutakuwa na tatizo litaweza fanyiwa utatuzi mara moja ” alisema Dkt. Mollel.

Aidha, alisema kuwa, katika kuboresha tahadhari zaidi magari yaliyotolewa yanalenga kuwakinga madereva na Watalii kwa kutenganishwa kwa kioo ili kudhibiti mnyororo wa maambukizi ya virusi vya Corona endapo atatokea.

“Magari yenyewe yatakuwa Dereva anaingia ndani, lakini kunakuwa na kinga inayowatenganisha Watalii na madereva wetu jambo litalosaidia kudhibiti maambukizi endapo yatatokea ” alisema
Share To:

Post A Comment: