Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtandao wa Viongozi Wanawake Wanaochipukia katika Utumishi wa Umma Tanzania ujulikanao kama Emerging Women Leaders in Tanzania (EWLT) jana umetoa vifaa vya usafi kwa ajili ya kujikinga na ugonjwa wa Corona kwa gereza la Isanga.

Wakikabidhi msaada huo,  mmoja wa Waanzilishi wa mtandao huo, Bi. Beatrice Kimoleta alisema hatua hiyo wameifanya ikiwa ni kuunga mkono kwa vitendo juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali katika kupambana na ugonjwa wa Corona.

“Mhe. Rais na Serikali nzima wamekuwa mstari wa mbele usiku na mchana kuweka mikakati mizuri ya kutuongoza katika  kupambana na ugonjwa huu ambao umeathiri dunia nzima, hivyo tukaona sisi kama Watumishi wa Umma wanawake tunao wajibu wa kushiriki kwa vitendo kuiunga mkono Serikali yetu katika mapambano haya kwa kutoa vifaa vya usafi na kujikinga na ugonjwa huu wa corona kwa gereza la Isanga.

“Tumefanya hivyo tukijua kuwa maeneo ya gereza pia ni maeneo yenye hatari kama yalivyo maeneo mengine, hivyo tumetoa vifaa hivi ili kuhimiza usafi, na visaidie kuwakinga wafungwa na Watumishi wenzetu wa Magereza,” alisema

Naye mwanzilishi mwenza Bi. Sakina Mwinyimkuu, alisema kuwa vifaa vilivyotolewa vina thamani ya Sh milioni 5.5 ambapo fedha hizo zimetokana na michango ya hiari ya wanachama wa mtandano huo na kutoa wito kwa makundi mengine kujitokeza na kuunga mkono jitihada hizi nzuri za Serikali"

Alisema vifaa walivyokabidhi ni baadhi dawa baridi za maumivu, gloves, vitakasa mikono, dawa ya meno, miswaki, sabuni za kufanyia usafi, sabuni za kuogea, sabuni za kufulia, taulo za kike, vifaa vya usafi, mashine za kunawia mikono na barakoa.

Naye Mkuu wa Magereza Mkoa wa Dodoma, Kanneth Mwambije alishukuru mtandao huo kwa vifaa walivyopatia Magereza na kuwa kazi waliyofanya na msaada waliotoa inadhihirisha kuwa wao wanawake ni wazazi na siku zote wapo kuhakikisha jamii inakuwa salama"

Aidha, alitumia fursa hiyo kuuhakikishia Mtandano huo kuwa vifaa vilivyotolewa vitatumika kama ilivyokusudia na si vinginevyo.

MTANDAO huu wa  Watumishi wa Umma Wanawake ujulikanao kama Viongozi Wanawake Wanaochipukia Tanzania (Emerging Women Leaders in Tanzania - (EWLT) ulianzishwa mapema mwezi Novemba, 2019 ukiwa na malengo ya kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo miongoni mwao pamoja na kupata uzoefu (mentoring) kutoka kwa Viongozi Wanawake wastaafu waliokuwa watumishi wa Umma ili kuwafanya wawe Viongozi bora katika Utumishi wa Umma.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: