Mkuu wa wilaya ya Kilolo Asia Abdallah mwenye kilemba chekundu na kamati yake ya ulinzi na usalama wilaya wakikagua daraja la Ruaha Mbuyuni 
Shughuli za kusogeza mawe zikiendelea 
Basi likipita daraja la Ruaha Mbuyuni 
Viongozi wakitazama daraja la Ruaha Mbuyuni 

Meneja wa Tanroads mkoa wa Iringa Daniel Kindole
.............................................................

MENEJA  wa TANROADS mkoa wa Iringa mhandisi Daniel Kindole alazimika  kukesha katika daraja la Ruaha Mbuyuni  linalounganisha  mikoa ya nyanda  za  juu  kusini na nchi  za  kusini mwa Tanzania kulinusuru  lisisombwe na mafuriko .

Akizungumza  jana baada ya kamati ya  ulinzi na usalama  wilaya ya  Kilolo ikiongozwa na mkuu  wa  wilaya ya Kilolo Asia Abdallah  kutembelea  kukagua  usalama wa  daraja  hilo la Ruaha Mbuyuni alisema  kuwa  mvua kubwa zinazoendelea  mikoa ya  Iringa ,Njombe na Mbeya  zimeendelea  kuhatarisha usalama wa  daraja  hilo  hali iliyopelekea  ofisi yake  kuhamia  katika  eneo hilo la daraja la Ruaha Mbuyuni  ili  kufanya uangalizi  wa karibu na kuchukua hatua ya  kuanza  kuliimarisha  zaidi .

Mhandisi Kindole  alisema  kuwa  kasi ya maji inayofika katika  daraja hilo  ni  kubwa sana  hivyo  yeye na timu yake  wameanza ukaguzi na uangalizi wa daraja hilo ambalo ni daraja  tegemeo  kwa  mikoa ya nyanda  za  juu  kusini na nchi  za  kusini mwa Tanzania kama  Zambia ,Malawi, Afrika ya  Kusini na nyingine  ambazo  zinategemea   kusafirisha  mizigo ama abiria kwa  njia ya barabara  kwa  kupita katika daraja hilo .

Hivyo  alisema moja kati ya makakati  ambao wanaufanya kunusuru  daraja  hilo ni  kuthibiti  maeneo  ambayo yaliwa na maji kwa kujaza mawe  ili  yasiendelee  kuchimbika  zaidi  kama kinga ya  kuzuia  daraja hilo  kusombwa na maji kazi ambayo  wamekuwa  wakiifanya usiku na machana  kila maji yanapopungua  wamekuwa  wakiendelea na uthibiti wa mmomonyoko  wa ardhi  kuelekea  katika  daraja hilo .

Hata  hivyo  alisema kazi hiyo wamekuwa  wakiifanya kwa  kuwasiliana na wenzao wa bwawa la Mtera  ili pale  inapowezekana kupunguza maji   kwa  kuzuia  kidogo katika bwawa   hilo  wamekuwa wakifanya  hivyo  ili  kupunguza kasi ya maji katika daraja hilo maji ambayo awali  yalikuwa yamejaa  sana  na kutishia  usalama wa  daraja  hilo .

"  Mimi na  timu yangu  tupo hapa kwa zaidi ya  siku nne  sasa  tunafuatilia  mwenendo wa maji maana madhara  ya daraja  hili kama  litavunjika ni kubwa  sana   hivyo tumekuwa tukikishe  kufanya kazi usiku na mchana   ili kulinda usalama wa daraja  hilo na  tutaendelea  kukesha   kulinda daraja  ili  kuepusha madhara  makubwa ambayo yangeweza  kujitokeza kwa  daraja hilo kama  litasombwa na maji haya ambayo kimsingi ni maji mengi yanayoongezeka  siku  hadi siku "

Mkurugenzi  mtendaji wa Halmashauri ya  Kilolo Aloyce Kwezi alisema  kuwa mvua  hizo zinazoendelea  kunyesha  zimeathiri miundo mbinu  mingi ya  wilaya ya  Kilolo na kuwa hali ya uchumi wa wilaya  hiyo  imeyumba  kutokana na kuharibika kwa miundo mbinu ya barabara .

Alisema  kuwa awali  wilaya   hiyo  miezi kama  hii  wawlikuwa  wakitegemea  makusanyo ya mapato yake ya  ndani  kupitia  usafirishaji wa mazao mbali mbali   ambapo kwa  siku wilaya  hiyo  ilikuwa  ikisafirisha malori ya mizigo  zaidi ya 40  ila kwa sasa  wilaya  hiyo inasafirisha  kwa siku malori yasiyozidi matano  jambo ambalo linakwamisha mapato ya  wilaya  hiyo .

Kwezi  alipongeza   jitihada mbali mbali  zinazochukuliwa na meneja wa TANROADS  mkoa wa Iringa kwa  kukesha  katika  daraja hilo la Ruaha Mbuyuni ili  kuepusha madhara  zaidi na kuwa ni watendaji  wacache  ambao  wamekuwa  wakijitolea  nguvu  zao katika  kutatua kero za  umma kama  hizo na kuwa  pasipo umakini wa meneja  huyo yawezekana  daraja hilo usalama  wake ungekuwa mashakani zaidi .

Mkuu  wa  wilaya ya  Kilolo Asia Abdallah  alisema  kuwa  kuwa  wakati serikali ikiendelea  kuchukua tahadhari  mbali mbali  dhidi ya wananchi na miundo mbinu ni vizuri wananchi nao  kuchukua tahadhari kwa kuepuka  kuendelea na shughuli katika maeneo  yaliyozungukwa na maji  kwani ni hatari kwa usalama wao  na si  vizuri wananchi  kuendelea  kuwa wakaidi  kuondoka katika maeneo hatarishi  na mafuriko .

Mkuu  huyo wa wilaya  alisema mvua hizo zimeleta  madhara makubwa katika kata ya Ruaha Mbuyuni na maeneo mengine  baaada ya  mashamba ya  wananchi kusombwa na maji pia baadhi ya mashamba  kuzingirwa na maji   hivyo wananchi  kushindwa  kwenda  kuvuna mazao  yao kama nyanya ambazo zimeendelea  kuharibika  na nyingine  kusombwa na mafuriko .

Aidha alisema  kuwa kamati yake ya ulinzi na usalama ya  wilaya  imeendelea  kutembelea  maeneo  yote ya wilaya ili  kuona athari  ambazo  zimeletwa na mvua  hiyo na maeneo  ambayo  mawasiliano ya barabara  yamekatia  watalamu wa TARURA na TANROADS  wamekuwa wepesi kwenda  kurejesha kwa  muda  mawasiliano hayo  ili yaweze  kupitika kwa urahisi .

Hivi  karibuni Rais Dkt John Magufuli  akikagua maendeleo ya  upanuzi wa  barabara ya Mbezi jijini Dar es Salaam alionya mameneja  wa wakala wa barabara Tanzania (TANROADS) kuwa watakuwa  hawana kazi iwapo barabara ama daraja  litakatika katika  mikoa  yao .













Share To:

Francis Godwin Mzee wa matukiodaima

Post A Comment: