Mkuu wa wilaya ya Kilolo Asia Abdallah mwenye kilemba chekundu na kamati yake ya ulinzi na usalama wilaya wakikagua daraja la Ruaha Mbuyuni
Shughuli za kusogeza mawe zikiendelea
Basi likipita daraja la Ruaha Mbuyuni
Viongozi wakitazama daraja la Ruaha Mbuyuni
Meneja wa Tanroads mkoa wa Iringa Daniel Kindole
.............................................................
MENEJA wa TANROADS mkoa wa Iringa mhandisi Daniel Kindole alazimika kukesha katika daraja la Ruaha Mbuyuni linalounganisha mikoa ya nyanda za juu kusini na nchi za kusini mwa Tanzania kulinusuru lisisombwe na mafuriko .
Akizungumza jana baada ya kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya Kilolo ikiongozwa na mkuu wa wilaya ya Kilolo Asia Abdallah kutembelea kukagua usalama wa daraja hilo la Ruaha Mbuyuni alisema kuwa mvua kubwa zinazoendelea mikoa ya Iringa ,Njombe na Mbeya zimeendelea kuhatarisha usalama wa daraja hilo hali iliyopelekea ofisi yake kuhamia katika eneo hilo la daraja la Ruaha Mbuyuni ili kufanya uangalizi wa karibu na kuchukua hatua ya kuanza kuliimarisha zaidi .
Mhandisi Kindole alisema kuwa kasi ya maji inayofika katika daraja hilo ni kubwa sana hivyo yeye na timu yake wameanza ukaguzi na uangalizi wa daraja hilo ambalo ni daraja tegemeo kwa mikoa ya nyanda za juu kusini na nchi za kusini mwa Tanzania kama Zambia ,Malawi, Afrika ya Kusini na nyingine ambazo zinategemea kusafirisha mizigo ama abiria kwa njia ya barabara kwa kupita katika daraja hilo .
Hivyo alisema moja kati ya makakati ambao wanaufanya kunusuru daraja hilo ni kuthibiti maeneo ambayo yaliwa na maji kwa kujaza mawe ili yasiendelee kuchimbika zaidi kama kinga ya kuzuia daraja hilo kusombwa na maji kazi ambayo wamekuwa wakiifanya usiku na machana kila maji yanapopungua wamekuwa wakiendelea na uthibiti wa mmomonyoko wa ardhi kuelekea katika daraja hilo .
Hata hivyo alisema kazi hiyo wamekuwa wakiifanya kwa kuwasiliana na wenzao wa bwawa la Mtera ili pale inapowezekana kupunguza maji kwa kuzuia kidogo katika bwawa hilo wamekuwa wakifanya hivyo ili kupunguza kasi ya maji katika daraja hilo maji ambayo awali yalikuwa yamejaa sana na kutishia usalama wa daraja hilo .
" Mimi na timu yangu tupo hapa kwa zaidi ya siku nne sasa tunafuatilia mwenendo wa maji maana madhara ya daraja hili kama litavunjika ni kubwa sana hivyo tumekuwa tukikishe kufanya kazi usiku na mchana ili kulinda usalama wa daraja hilo na tutaendelea kukesha kulinda daraja ili kuepusha madhara makubwa ambayo yangeweza kujitokeza kwa daraja hilo kama litasombwa na maji haya ambayo kimsingi ni maji mengi yanayoongezeka siku hadi siku "
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Kilolo Aloyce Kwezi alisema kuwa mvua hizo zinazoendelea kunyesha zimeathiri miundo mbinu mingi ya wilaya ya Kilolo na kuwa hali ya uchumi wa wilaya hiyo imeyumba kutokana na kuharibika kwa miundo mbinu ya barabara .
Alisema kuwa awali wilaya hiyo miezi kama hii wawlikuwa wakitegemea makusanyo ya mapato yake ya ndani kupitia usafirishaji wa mazao mbali mbali ambapo kwa siku wilaya hiyo ilikuwa ikisafirisha malori ya mizigo zaidi ya 40 ila kwa sasa wilaya hiyo inasafirisha kwa siku malori yasiyozidi matano jambo ambalo linakwamisha mapato ya wilaya hiyo .
Kwezi alipongeza jitihada mbali mbali zinazochukuliwa na meneja wa TANROADS mkoa wa Iringa kwa kukesha katika daraja hilo la Ruaha Mbuyuni ili kuepusha madhara zaidi na kuwa ni watendaji wacache ambao wamekuwa wakijitolea nguvu zao katika kutatua kero za umma kama hizo na kuwa pasipo umakini wa meneja huyo yawezekana daraja hilo usalama wake ungekuwa mashakani zaidi .
Mkuu wa wilaya ya Kilolo Asia Abdallah alisema kuwa kuwa wakati serikali ikiendelea kuchukua tahadhari mbali mbali dhidi ya wananchi na miundo mbinu ni vizuri wananchi nao kuchukua tahadhari kwa kuepuka kuendelea na shughuli katika maeneo yaliyozungukwa na maji kwani ni hatari kwa usalama wao na si vizuri wananchi kuendelea kuwa wakaidi kuondoka katika maeneo hatarishi na mafuriko .
Mkuu huyo wa wilaya alisema mvua hizo zimeleta madhara makubwa katika kata ya Ruaha Mbuyuni na maeneo mengine baaada ya mashamba ya wananchi kusombwa na maji pia baadhi ya mashamba kuzingirwa na maji hivyo wananchi kushindwa kwenda kuvuna mazao yao kama nyanya ambazo zimeendelea kuharibika na nyingine kusombwa na mafuriko .
Aidha alisema kuwa kamati yake ya ulinzi na usalama ya wilaya imeendelea kutembelea maeneo yote ya wilaya ili kuona athari ambazo zimeletwa na mvua hiyo na maeneo ambayo mawasiliano ya barabara yamekatia watalamu wa TARURA na TANROADS wamekuwa wepesi kwenda kurejesha kwa muda mawasiliano hayo ili yaweze kupitika kwa urahisi .
Hivi karibuni Rais Dkt John Magufuli akikagua maendeleo ya upanuzi wa barabara ya Mbezi jijini Dar es Salaam alionya mameneja wa wakala wa barabara Tanzania (TANROADS) kuwa watakuwa hawana kazi iwapo barabara ama daraja litakatika katika mikoa yao .
Post A Comment: