Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imetoa ushauri kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuongeza uwekezaji katika kuendeleza Sayansi, Teknolojia na Ubunifu nchini baada ya kuridhishwa na utendaji wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela katika eneo hilo.
Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Peter Serukamba wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Chuo cha Sayansi na Teknoloji cha Nelson Mandela kilichopo jijini Arusha.
Mhe Serukamba amesema Chuo cha Nelson Mandela kinafanya vizuri kwenye matumizi ya Sayansi Teknolojia na Ubunifu na kuwa inaridhisha kuona kuna vifaa vya Tehama vinavyoendana na Mapinduzi ya nne ya Viwanda ikiwemo kompyuta kubwa yenye uwezo wa kuchakata taarifa mbalimbali kwa muda mfupi "High Performance Computting sysytem (HPC) au "Super Computer" ikilinganishwa na kompyuta za kawaida yenye gharama ya takribani Dola za kiamarekani milioni 1.3.
"Nimeridhishwa na maendeleo ya kazi za utafiti na ubunifu katika Taasisi hii hasa jinsi mlivyoweza kuingia katika Mapinduzi ya nne ya viwanda, rai yangu kwa Serikali ni uwekezaji zaidi katika eneo hili ili tafiti na ubunifu unaozalishwa uwe na manufaa zaidi kwa wananchi " amesisitiza Mhe. Serukamba.
Kwa upande wake mjumbe wa Kamati hiyo ambae pia ni mbunge wa Biharamulo Magharibi Oscar Mukasa amesema ni vizuri kukaanzishwa chombo katika Chuo hicho ambacho kitasaidia kuhusianisha ufanisi wa tafiti zinazozalishwa na utekelezaji wa Sera.
Nae Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema Serikali ya Awamu ya Tano imetoa kipaumbele katika eneo la Sayansi na Teknolojia kwani ni ndicho kichocheo kikubwa cha uimarishaji Viwanda.
Katika hatua nyingine Prof. Ndalichako amesema Wizara anayoisimamia itatoa fedha kiasi cha sh bilioni 3.9 kwa ajili ya ujenzi wa Hosteli za wanafunzi wa kike katika Chuo hicho ili kuongeza idadi ya wanafunzi wanawake wanasayansi na watafiti nchini.
Nae Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Emmanuel Luoga amesema Chuo kimefarijika sana na ujio wa Kamati na kwamba kitaendelea kujikita katika dhamira yake ya kufanya tafiti katika Sekta mbalimbali ikiwemo kilimo na kupeleka matokeo kwa walaji.
Post A Comment: