Ferdinand Shayo,Arusha.

Shirika la Haki  elimu  limetoa kiasi cha shs 20 milioni kwa ajili ya kuchimba kisima  cha maji katika shule ya sekondari Mukulat iliyopo katika halmashauri ya Arusha wilayani Arumeru kilichogharimu shs 25 milioni .

Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi mtendaji  wa shirika hilo ,Dokta John Kalage  wakati akizungumza katika makabithiano  ya kisima hicho kilichojengwa  kwa ufadhili wa ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania.

Dokta Kalage alisema kuwa,ubalozi wa Uingereza umekuwa  ukishirikiana na Haki elimu katika kuboresha mazingira ya elimu, na ufundishaji  hasa kwa mtoto wa kike katika kuhakikisha idadi ya wanafunzi  wanaojiunga katika shule hadi vyuo inaongezeka kwa asilimia  kubwa.

Aliongeza kuwa, wamefikia hatua  ya kusaidia shule hiyo baada ya kuwepo kwa  changamoto  ya wanafunzi wa kike kutembea umbali wa kilometa 8 kufuata huduma za maji.

Alisema kuwa, shirika hilo limekuwa likisaidia  shule 127 ikiwemo shule hiyo na shule ya Ngiresi lengo likiwa ni kusaidia kuboresha mazingira ya mtoto wa kike  ili waweze kuongeza kiwango cha idadi hiyo kuwa kubwa kuanzia elimu ya msingi hadi chuo.

" takwimu zinaonyesha kuwa ,watoto wa kike wamekuwa wakiandikishwa  kwa wingi katika  shule za msingi kuliko wa kiume  lakini ukija kwa masomo ya elimu ya juu mwitikio wa wasichana ni mdogo sana,ambapo kwa kipindi cha miaka mitano hadi sita  iliyopita inaonyesha asilimia 5  hadi 6 ya wasichana wamekuwa wakiendelea na kidato cha tano huku wavulana ikiwa ni asilimia 12 hadi 13."alisema Dokta Kalage.

Naye Mwalimu mkuu wa shule hiyo ,Vitalis Nada alisema kuwa,wamepata fursa ya kutembelewa na Balozi huyo kwa ajili ya kujionea mradi wa kisima cha maji kilichofadhiliwa na ubalozi ambapo kimeweza kuondoa changamoto kubwa ya wasichana wanaolala bwenini kutembea umbali mrefu.

Nada alisema kuwa, pamoja na kuwa shule hiyo inazungukwa na jamii ya wafugaji,wamekuwa wakijitahidi sana kuhakikisha kiwango cha elimu hasa kwa watoto wa kike kinakuwa  juu kwa kuboresha mazingira shuleni hapo,ambapo imesaidia sana kiwango cha  elimu kwa wasichana  kuendelea kupanda kila mwaka.

Alitaja changamoto inayowakabili kuwa ni pamoja na changamoto ya uhaba wa mabweni kwa ajili ya wasichana ambapo wana mabweni mawili tu ambayo yanalaza wanafunzi 84 ,huku shule nzima ikiwa na wasichana 520, hivyo wanafunzi 436 wana uhitaji wa mabweni hayo.

Kwa upande wa Balozi wa Uingereza  nchini Tanzania ,Sarah Cooke alisema kuwa, wamekuwa wakisaidia shule mbalimbali  kuondokana na changamoto mbalimbali katika sekta ya elimu huku  lengo kubwa likiwa ni kusaidia zaidi wasichana  ili waweze kuwa na mwamko wa kupenda  elimu zaidi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: